Burhani Yakub,Tanga
BARAZA la Waislamu Tanzania (Bakwata) limemtaka Katibu Mtendaji wa Baraza la Mitihani (Necta), Dk Joyce Ndalichako kujiuzulu wadhifa huo akimtuhumu kuwafelisha mitihani ya dini ya Kiislamu wanafunzi wa kidato cha sita wa dini hiyo.
Kauli hiyo ya Bakwata imetolewa na Mufti wa Tanzania, Sheikh Issa Bin Shaaban Simba katika mkutano wake na waandishi wa habari jijini Tanga jana kuelezea msimamo wa Waislamu nchini kuhusu matokeo ya kidato cha sita, hujuma inayoandaliwa kufanyika katika zoezi la sensa pamoja na vurugu zilizotokea Zanzibar.
Kuhusu hujuma ya mtihani, Mufti Simba alisema kuwa matokeo ya mtihani ya dini hiyo ya Kidato cha Sita yaliyotangazwa Mei Mosi 2012, yaliwashtua wanafunzi Waislamu waliofanya mtihani wa elimu ya dini ya kiislamu (Islamic Knowledge), ambayo yalionyesha kuwa asilimia 70 walifeli kwa kupata daraja F.
Alisema matokeo hayo yalionyesha kuwa ni asilimia 30 ndiyo waliofaulu kwa kupata daraja D, ambapo waliopata alama za juu kabisa nchi nzima ni wanafunzi saba pekee.“Matokeo haya yaliwashtua wanafunzi na wazazi, taasisi mbalimbali za kiislamu zilimua kukata rufaa kuonyesha kutokubaliana na matokeo hayo, hatimaye baraza hilo
likabaini kuwa lilikosea na likaidhinisha kutolewa matokeo
mapya,” alisema Mufti Simba.
Tayari Ndalichako ametoa ufafanuzi kuwa kosa lililotokea akisema si hujuma bali ni la kiufundi lililotokana na kubadili utaratibu wa kufanya mitihani mitatu ya somo hilo kuwa miwili, lakini mfumo wa ujumlishaji maksi ulisahaulika kubadilishwa.
Ndalichako alilieleza gazeti dada la Mwananchi, The Citizen, kuwa awali matokeo ya mitihani mitatu yalikuwa yanajumlishwa na kugawanywa kwa tatu kwa kutumia mfumo wa kompyuta, ili kupata alama rasmi za mtahiniwa, lakini safari hii zilipojumlishwa alama za mitihani miwili ya somo hilo ziliendelea kugawanywa kwa tatu badala ya mbili kimakosa.
Habari zilizopatikana kutoka Necta zimesema kuwa baada ya kupata malalamiko ya wanafunzi hao, uchunguzi ulifanyika na kubaini kasoro hiyo ambapo ilirekebishwa.Mei 30, mwaka huu Necta ilikutana na Baraza la Wakuu wa Shule za Kiisilamu na kufafanua suala hilo, ambapo ilionekana tatizo hilo si hujuma bali kosa la kiufundi.
Mwenyekiti wa Islamic Education Panel, Pilly H.H alimwandikia barua Katibu Mkuu wa Wizara ya Elimu na Mafunzo ya Ufundi na nakala kwa Katibu Mtendaji wa Necta, Amir, Jumuia na Taasisi za Kiislamu Tanzania akishukuru wizara kwa hatua zilizochukuliwa.
“Tunashukuru kwa jinsi Wizara ya Elimu na mafunzo ya ufundi ilivyopokea suala hili kwa uzito unaostahiki…Tunatoa shukurani za pekee kwa katibu mtendaji wa baraza la mitihani kwa hatua alizochukua ndani ya muda mfupi sana, nashukuru kwa ushirikiano,” ilisema barua hiyo iliyoandikwa na Mwenyekiti wa Baraza la Wakuu wa Shule za Kiislamu.
Hata hivyo, akisistiza hoja yake Mufti Simba alisema kuwa matokeo yaliyotolewa upya yalionyesha kwamba wanafunzi zaidi ya asilimia 70 ya wanafunzi walifaulu, jambo ambalo Waislamu wanaamni kwamba ni hujuma inayolenga kupunguza idadi ya wanafunzi wa Kiislamu wa kujiunga na vyuo vikuu.
Mufti huyo alisema jambo lililomshangaza yeye pia pamoja na Waislamu wote nchini ni tamko lililotolewa na Ndalichako kupitia vyombo vya habari Jumanne iliyopita aliposema kuwa Baraza la Mitihani halikukosea kutoa matokeo hayo kwa kuwa waliosahihisha ni walimu wenye sifa.
“Bakwata inamshangaa Katibu Mtendaji wa Baraza la Mitihani, Ndalichako kwa kauli yake aliyoitoa kupitia vyombo vya habari juzi 5/6/2012 akisema hakuna hujuma na mitihani inasahihishwa na walimu wenye sifa na wanachaguliwa na wakuu wa shule zao,”alisema Mufti Simba.
Alisema hoja iliyotolewa na Ndalichako kwamba wanaosahihisha ni wenye uzoefu haina mashiko kwa sababu Waisalmu wanacholalamikia ni mfumo mzima wa “Conveyor Belt”, aliodai umewekwa kuwahujumu wanafunzi
Waislamu.
Alisema matokeo hayo ya mtihani wa somo la kiislamu umeonyesha kuwa upo wasiwasi kwamba kilichofanyika huko ndicho wanachofanyiwa wanafunzi wa kiislamu katika masomo mengine kuanzia darasa la saba, kidato cha nne na hata vyuo vikuu kwa lengo la kupunguza idadi ya wasomi waislamu.
“Waislamu tunaamini kwamba hila kama hii inafanyika pia kwenye masomo mengine, kwa maana hiyo tunataka Ndalichako na watendaji wengine wajiuzulu ili kuondoa kashfa hii kwa Serikali, pia kuleta imani ya Waislamu kwa Serikali yao, ”alisema Mufti Simba.
Alifafanua kuwa baada ya kujiuzulu, Serikali iunde tume ya kuchunguza hujuma zilizotendeka katika baraza hilo dhidi ya Waislamu kwa kipindi cha miaka 10 iliyopita akieleza kuwa Waislamu wanaamini kwamba wanafunzi wengi
wamefelishwa kwa kusudi maalumu la kuzorotesha kizazi chao.
SUALA LA SENSA YA WATU NA MAKAZI.
Kuhusu Sensa, Mufti Simba alisema kuwa kalenda iliyotolewa na Ofisi ya Waziri Mkuu, takwimu zinaoonyesha kuwa idadi ya Watanzania ni 43 milioni ambapo Wakristo ni asilimia 52, Waislamu asilimia 32 na dini nyingine ni asilimia 16 akieleza kuwa takwimu hizo si sahihi.
Alisema kuwa Bakwata inalaani kitendo hicho alichosema kinapotosha wananchi kwa kuwa sensa iliyofanyika mwaka 2002 kipingele kinachobainisha dini za Watanzania kiliondolewa.
MGOGORO WA ZANZIBAR
Akizungumzia matukio yauvunjifu wa amani vilivyotokea visiwani Zanzibara hivi karibuni Mufti Simba alisema Bakwata inalaani kitendo inalaani kitendo hicho ikiamini kwamba waliofanya vurugu hizo siyo Waislamu bali ni
wahuni.
Alishauri kuundwa kamati ya pamoja kati ya Serikali na kikundi cha Waislamu cha Uamsho ili kuchunguza waliohusika na vurugu hizo na waliohusika kuchukuliwa hatua.
Chanzo: Mwananchi
No comments:
Post a Comment