Habari za Punde

Nusu ya Wazanzibari Wanaishi katika Umasikini'


Na Husna Mohammed
TATIZO la umasikini uliokithiri umeelezwa kuwa ndio chanzo kikubwa cha watoto Chini ya umri wa miaka 18 kujiingiza katika ajira mbaya za watoto hapa Zanzibar.

Katika utafiti uliofanywa mwaka 2004/2005 na ofisi ya Mtakwimu mkuu wa Serikali ya Mapinduzi Zanzibar, umebaini kuwa nusu ya watu wa Zanzibar ni masikini, jambo ambalo baadhi ya familia wamekuwa wakiwategemea watoto wadogo katika kusaidia majukumu ya kifamilia.


Afisa wa Chama cha Waandishi wa Habari wanawake Tanzania Zanzibar (TAMWA), Sheikha Haji Dau, alisema hayo wakati alipokuwa akitoa mafunzo kwa wanawake wa Mkoa wa Kusini Unguja huko Dunga, kuhusu mapambano juu ya ajira za watoto katika mkoa huo.

Alifahamisha kuwa Mkoa wa Kusini ni moja ya mkoa wenye ajira nyingi za watoto hasa kutokana na mazingira ya bahari hivyo watoto wengi wamekuwa wakijishughulisha na sekta ya uvuvi ambapo pamoja na mambo mengine lakini familia zao zimekuwa zikiwategemea kutokana na kipato kidogo wanachokipata.

Alifahamisha kuwa watoto wengi wamekuwa wakifanyishwa kazi za hatari na kukoseshwa haki yao ya msingi ya elimu jambo ambalo linamjengea mazingira mabaya kwa maisha yake ya baadae.

Alizitaja baadhi ya ajira mbaya kwa watoto kuwa ni pamoja na kuwaingiza watoto katika biashara haramu ya madawa ya kulevya, kufanyishwa kazi katika sekta ya kilimo, ufugaji, viwanda nakadhalika.

"Kuwatumia kuwakuwadia au kuwatoa kwa ajili ya kufanya ukahaba na utengenezaji wa picha za ngono au katika maonesho ya picha za ngono, uuzaji na usafirishaji haramu wa watoto, kuweka rehani kwa ajili ya deni na kuwafanya vijakazi ni moja ya utumikishwaji wa watoto ulioshamiri nchini," alisema Ofisa huyo.

Aidha alisema pamoja na mambo mengine lakini Tanzania imekuwa ikiwatumikisha watoto kazi ya uyaya (majumbani) kutoka sehemu moja kwenda nyengine jambo ambalo wakati mwengine linahatarisha ustawi wa ukuaji wa watoto kutokana na kazi za ndani.

Sheikha alifahamisha kuwa watoto hao wamekuewa wakipata madhara makubwa ikiwa ni pamoja na madhara ya kimwili, kiakili na hata kimaadili.

Nao baadhi ya washiriki wa mkutano huo kutoka katika vijiji vya Chwaka, Marumbi, Uzini na Charawe walikiri kuwepo kwa watoto wanaotumikishwa katika familia zao ikiwa ni pamoja na kufanyishwa kazi za uvuvi, kilimo, ufugaji na ukataji wa kuni jambo ambalo watoto wengi wanakosa fursa ya kupata elimu ya lazima.

Mradi wa kuwatoa watoto katika ajira mbaya umefadhiliwa na Jumuiya ya Ulaya (EU), ambao unasimamiwa na Mfuko wa kuwasaidia watoto ulimwenguni Save the Children na watekelezaji wa mradi huo ni Chama cha Waandishi wa Habari wanawake TAMWA Zanzibar wakishirikiana na Jumuiya ya kuwaendeleza wanawake Zanzibar (COWPZ)

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.