Habari za Punde

Suala la Kodi Wafanyakazi SMT Walioko Zanzibar Kutatuka


 Na Mwantanga Ame

KODI za mishahara ya wafanyakazi wa Utumishi wa umma wa Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, wanaofanya kazi zao Zanzibar, itaingizwa katika mfuko mkuu wa Hazina wa Serikali ya Zanzibar.

Hatua hiyo imekuja baada ya Serikali ya Zanzibar na Serikali ya Jamhuri ya Muungano kukubaliana katika vikao vya kutatua kero za Muungano vilivyopita ya kutaka fedha za kodi za watumishi wa Serikali ya muungano waliopo Zanzibar kubakia Zanzibar.


Wafanyakazi hao ni pamoja na Taasisi za Jeshi la Wananchi Tanzania (JWTZ), Jeshi la Polisi, Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA), Shirika la Simu Tanzania (TCCL), Shirika la Posta Tanzania, Benki Kuu Tanzania (BOT) na Taasisi za kibenki zilizofungua matawi Zanzibar ikiwemo NMB, CRDB, Exim Bank na KBC.

Taasisi nyengine ambazo zitaingia katika mkumbo huo ni pamoja na Idara ya Mambo ya Nje, Idara ya Muungano, Ofisi ya Bunge, Makampuni ya simu pamoja na taasisi binafsi ambazo zimefungua matawi yake Zanzibar baada ya kusajiliwa Tanzania Bara yakiwemo Mashirika ya Bima.

Serikali itachukua hatua hiyo kutokana na mfumo uliopo hivi sasa kodi hizo zimekuwa zikiingia katika mfuko Mkuu wa Hazina wa Tanzania bara jambo ambalo limeonekana haliko sahihi utekelezaji wake.

Hapo awali, Waziri wa Fedha, Uchumi na Mipango ya Maendeleo Zanzibar, Omar Yussuf Mzee, akielezea suala hilo alisema tayari limeshamaliza mjadala wake na hivi sasa limo katika vikao vya watendaji kwa ajili ya kufanyiwa mabadiliko ya sheria ya fedha ya Serikali ya Muungano ili kuwezesha fedha hizo kuingia Zanzibar.

Akijibu masuala ya waandishi wa habari Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Dk. Ali Mohamed Shein, alisema tayari Serikali ya Muungano imeshatayarisha sheria hiyo na inatarajiwa kupelekwa bungeni kwa hatua za kisheria.

Alisema kuja kwa fedha hizo ni sehemu ya muendelezo wa kutatua kero za Muungano ambapo tayari mambo kadhaa yameshafanyika na hivi sasa baadhi yake yanasubiri mabadiliko ya kisheria.

Akitaja mambo hayo alisema ni pamoja na suala la mafuta na gesi asilia baada ya serikali ya Zanzibar kutaka kutolewa katika mambo ya Muungano ambapo sasa lipo katika hatua za kisheria na Kamati ya Fedha ya Pamoja (JFC).

Sambamba na hilo, masuala mengine ni Jumuiya ya Afrika Mashariki kuhusu vipi Zanzibar inaingia ambapo mjadala wake unaendelea katika upande wa kisiasa, Uvuvi wa Bahari Kuu ambao Zanzibar imeamuliwa kuwa ndio Makao Makuu ambapo linasubiri kutatuliwa kisheria.

Mambo mengine aliyoyataja Dk. Shein ni suala la ajira kwa wazanzibari kwenye taasisi za muungano, ushirikiano wa taasisi za Nje katika mambo ya mikopo, Bodi na Mapato Zanzibar (ZRB) na Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA), Usajili wa vyombo vya moto kutoka Zanzibar ambao umefikia katika hatua nzuri, ongezeko la bei ya umeme kwa Zanzibar kutoka TANESCO, uharamia, mfuko wa maendeleo ya Jimbo.

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.