Habari za Punde

Upepo Wasababisha Familia 11 Kukosa Makaazi Pemba



 Na Haji Nassor, Pemba

JUMLA ya familia 11 zenye wakaazi zaidi ya 70 huko Shehia ya Kangagani Wilaya ya Wete Mkoa wa Kaskazini Pemba, wamelazimika kuzihama nyumba zao baada ya kukumbwa na upepo mkali na kuezua mapaa na kupasuka kwa kuta.

Upepo huo uliotokea jana wakati waumini wa dini ya kiislamu wakiendelea na sala ya Ijumaa, ambapo ulisababisha kuwahamisha wakaazi hao kutokana na dhoruba hiyo iliyowapa hofu kubwa juu ya usalama wao.

Akizungumza na Gazeti hili kwa njia ya simu, Sheha wa shehia hiyo Fakih Omar Yussuf alisema wakati wakiendelea na sala, ndipo upepo huo ambao alidai uliodumu kwa dakika 10, ulipovuma na wao baada ya sala kukimbilia eneo hilo.


Alisema walipofika eneo ambalo nyumba hizo 11 zilikumbwa na zahma hiyo, waliona mapaa ya  nyumba yakiwa yako mbali na nyumba na baadhi ya kuta za nyumba za tofali zimepasuka vibaya.

‘’Kwa kweli tulipofika wengi hatukuamini kwamba hasara hiyo imesbabishwa na upepo,maana kuta za nyumba tena za tofali zimeharibika vibaya mno, na mapaa yako mbali sana na nyumba zenyewe’’,alieleza kwa masikitiko Sheha huyo.

Akizitaja familia hizo alisema ni pamoja na nyumba ya Khamis Ali Shehe, Juma Faki Hassan, Fatma Juma Salehe, Haji Fakih Kombo, Mgeni Amour Shaame,  Shaali Muhidin Juma, Saleh Ali Hassan na Said Juma Bakar.

Sheha huyo alisema kwa sasa taratibu zinazoendelea, ni kuwatafuta Polisi pamoja na kitengo cha maafa ili wafanye taratibu nyengine za kuwasaidia waathirika hao ili wapate makaazi ya kujihifadhi wakati huu wakiwa wamekumbwa na kadhia hiyo.

Alisema kuwa kwa sasa baadhi ya wananchi waliokaribu na waaathirika hao wamekuwa wakiwasaidia wenzao waliopata athari hiyo, kwa kuwakusanyia vitu vyao karibu na makaazi yao ikiwa ni pamoja na bati na vitu vya matumizi ya ndani.

Alisema hili ni tukio la mwanzo kuwahi kutokezea katika kijiji chao katika siku za hivi karibuni na hadi anazungumza na mwandishi wa habari hizi hasara kamili haijambulika.

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.