Na Asya Hassan
WATOTO 10 wamefariki dunia kwa maradhi ya matumbo ya kuharisha wakipatiwa
matibabu katika hospitali kuu ya Mnazimmoja.
Akizungumza na mwandishi wa habari hizi, katibu wa hospitali ya Mnazi
mmoja, Dk. Omar Abdalla, alisema kuwa idadi hiyo ya vifo imeripotiwa ndani ya
mwezi uliopita baada ya kuongezeka kwa maradhi ya matumbo ya kuharisha kwa
watoto kutoka maeneo mbalimbali ya Zanzibar.
Katibu huyo alisema kuwa chanzo cha maradhi hayo kinasababishwa na
kukithiri kwa uchafu katika maeneo mbalimbali ya mji wa Zanzibar.
Alisema wananchi wa Zanzibar hawana
utamaduni wa kuchemsha maji, kusafisha mazingira yao wanayoishi pamoja na
kunawa mikono mara kwa mara hivyo, jambo linalopelekea mripuko wa maradhi hayo
hasa kwa watoto.
Katibu huyo alifahamisha kuwa ugonjwa uliopo hivi sasa ni matumbo ya
kuharisha na sio kipindupindu ambapo watoto ndio waathirika wakubwa wa maradhi
hayo kutokana na idadi ya wagonjwa wanaofikishwa hospitalini hapo idadi kubwa ni
watoto.
Katibu Omar, alisema kutokana na idadi ya watoto kuwa ipo juu kwa
kuathirika na maradhi hayo ipo haja kwa wazazi kuchukuwa juhudi za makusudi za
kuwadhibiti watoto hao kutochezea maji machafu yanayo toka katika makaro pamoja
na kuwepo kwa mvua zinazoendelea kunyesha.
"Wananchi wa Zanzibar hatuna tabia ya kusafisha mazingira yetu,hatuchemshi
maji na watoto wetu tunawaacha wanacheza katika mazingira ambayo
hayaridhishi,wanacheza katika maji machafu ambayo yanatoka katika karo,ndio maana
watoto wengi wameathirika na matumbo ya kuharisha na kupelekea kupoteza
maisha,"alisema.
Kwa upande wa Muuguzi dhamana wodi ya watoto, Khadija Muombwa Ame, alisema
mwezi uliopita, idadi ya watoto walipokelewa kwa wingi katika wodi yao kwa siku
imeongezeka na kufika watoto kumi hadi 15 huku ikiwa hakueleza kuwa ni jumla ya
wagonjwa wangapi wamepokewa hospitalini hapo.
Alisema wagonjwa hao wanatoka katika sehemu mbali mbali za mjini na
mashamba Unguja na kusema kuwa watoto wanaofika hapo wengi wao ni chini ya umri
wa miaka miwili.
"Siku za nyuma tulikuwa tunapokea wagonjwa wa aina hii lakini idadi
yao ilikuwa ndogo sana, toka kuanza kwa mwezi wa tano idadi imekuwa kubwa sana
kwani watoto kumi hadi 15, hali inatisha na watoto wenyewe wadogo ambao hawajui
wajikinge vipi,hivyo wazazi wawe na tahadhari juu ya hili,"alisema.
Muuguzi huyo akizungumzia juu ya dawa wanazotumia katika kipindi hicho
alisema dawa zinakuwepo na ikiwa hawana wanamuandikia mwenyewe mgonjwa na
kwenda kununua nje,hivyo hakuna msaada wa aina yoyote juu ya dawa wanazotumia
kwa maradhi hayo.
Khadija alisema ni vizuri kwa wazazi kuchukuwa tahadhari kwa watoto hao
pale wanapowakuta kuanza dalili hizo kwa kuwachemshia maji na kutia chumvi ili
kunusuru pomoja na kudhibiti hali hii.
Kwa upande wa mdhamini wa wodi ya watoto wa kiume, Raya Nassor Issa,
alisema hali ya wagonjwa kwa mwezi wa Mei ilikuwa kubwa kwani kwa siku walikuwa
wanapokea idadi ya wagonjwa watatu hadi wanne.
Aidha alisema kuwa maradhi ya kipindupindu yamepungua baada ya kupatiwa
chanjo za kuzuia kuharisha iliyotolewa miaka iliyopita,hivyo wagonjwa
wanaowapokea sasa ni wa maradhi ya kuharisha.
Alisema changamoto kubwa inayowakabili juu ya wagonjwa
hao ni kucheleweshwa kufikishwa hospitali hapo kwa kupatiwa matibabu kwa haraka
No comments:
Post a Comment