Habari za Punde

CUF Yamlilia Musobi



Na Asya Hassan

CHAMA cha CUF kimesema kimepokea kwa masikitiko na mshtuko mkubwa taarifa ya kifo cha aliyekuwa Mwenyekiti wa Taifa wa chama hicho,Musobi Mageni Musobi kilichotokea Mei 30 mwaka huu.

Taarifa kutok a Makao Makuu ya CUF Mtendeni Zanzibar imesema Musobi ambaye ameugua kwa muda mrefu alifariki majira ya saa 2:00 usiku nyumbani kwake, Ngudu wilaya ya Kwimba Mkoa wa Mwanza.

Kwa mujibu wa taarifa zilizotolewa na chama hicho kupitia vyombo vya habari, zimesema Chama hicho kimesema kimepokea kwa huzuni msiba wa kiongozi huyo shupavu,ambaye alibeba jukumu la uongozi,wakati mgumu chini ya misingi ya nidhamu,umoja,uwazi,uadilifu na demokrasia ya kweli.


Taarifa hiyo ilisema kuwa marehemu huyo alikiongoza chama hicho akiwa mwenyekiti wa pili tangu alipochaguliwa kushika wadhifa huo Julai 13, 1995 nafasi ambayo aliitumikia hadi kustaafu kwake Disemba 1999.

Taarifa hiyo ilibainisha kuwa pamoja na uongozi huo pia Mwenyekiti huyo katika uhai wake aliwahi kushika nafasi mbalimbali za uongozi,ikiwa ni pamoja na Waziri wa Ardhi,nyumba na Maendeleo ya Miji ya Serikali ya awamu ya kwanza ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania,ambapo aliongoza kuanzia mwaka 1972 hadi 1975.

Chama cha CUF kwa niaba ya watendaji,wanachama,wafuasi na wapenzi wake,wakiwemo wilaya zote 10 na majimbo yote 50 ya uchaguzi na matawi ya Zanzibar wanatoa salamu za rambirambi kwa Mwenyekiti wa chama Taifa, Profesa Ibrahim Haruna Lipumba pamoja na familia ya marehemu na kushikamana nao wakati huu mgumu wa msiba. 

Taarifa hiyo ilibainisha kuwa maziko ya marehemu huyo yanatarajiwa kufanyika Jumatatu Juni 4 mwaka huu kijijini kwake Ngudu,ambapo marehemu huyo amezaliwa, Aprili 1, 1931,marehemu huyo ameacha vizuka wawili,watoto 15 na wajukuu kadhaa,Mungu amlaze mahala pema peponi.



No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.