Habari za Punde

Wakimbizi waungana na familia zao. UNHCR kuwapa mtaji,chakula


Na Bakar Mussa, Pemba
FAMILIA a 7 za wananchi wa kisiwa cha Pemba, ambao walikimbilia nchini Somalia na kuhifadhiwa  katika kambi za wakimbizi , zimewasili kisiwani Pemba na kuunganishwa na familia zao  baada ya kupotea kwa muda wa miaka 12.

Familia hizo ni miongoni mwa familia 12 za wananchi wa Zanzibar , ambao walikuwepo nchi Somalia kama wakimbizi tokea mwaka 2000, na kuamuwa kurejea makwao ilikuungana na ndugu zao ambapo familia sita zimebaki kisiwani Unguja.

Wakiwasili katika bandari ya Mkoani Pemba na kupokelewa na jamaa zao   na maafisa mbali mbali wa serikali na  vyombo vya dola huku wakiongozwa na Mkuu wa Mkoa wa Kusini Pemba , Meja (mstaafu) , Juma Kassim Tindwa, walisema kwamba wamefarajika na kufurahishwa sana kwa kitendo hicho kilichofanywa na serikali ya Jamhuri ya Muungano kwa kushirikiana na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar na Shirika la Kuhudumia Wakimbizi la Umoja wa Mataifa ( UNHCR).



Walieleza kwamba fursa hiyo walioipata walikuwa wana isubiri kwa hamu na kwamba sasa imewafikia na hivyo wamejiona kama ni watu ambao wamezaliwa upya , kwa vile wamewasili wakiwa na familia nyengine ambazo walizipata wakiwa huko.

Mmoja kati ya wananchi hao, Ali Jaffar Othman (46)mzaliwa wa Mchanga Mrima Ole, katika wilaya ya Wete, aliliambia gazeti hili kwamba amefarajika sana kuona kwamba amerejea katika nchi yake na ana imani kuwa  Zanzibar  kwa sasa imeshatulia.

“ Najisikia raha sana leo, nikiwa katika nchi yangu naamini sasa imetulia ni tafauti na vile tulivyoiacha,” alisema.

Mwananchi mwengine, Ahmed Khatib Omar (30) mzaliwa wa Shengejuu , Wilaya ya Wete, alisema pamoja na kwamba alikuwa anawasiliana na jamaa zake , lakini anajisikia raha zaidi baada ya kuungana nao tena baada ya miaka 12.
Wakati alipokimbilia Somalia alikuwa na umri wa miaka 18.

Ali Haji Ali (37) mzaliwa wa Mtoni Chake Chake,  alisema anajisikia yuko katika hali ya furaha kubwa kwa kufika nchini kwake kwani alikuwa ana wasiliana na jamaa zake kwa njia ya simu tu.

“Mimi najihisi kama nimezaliwa upya kwa vile nimefika kisiwani Pemba na kupokelewa na jamaa zangu nikiwa na afya njema. Ila nasikitika sana kwa sababu baba yangu amefariki wakati mimi nikiwa Somalia, sikupata nafasi ya kumzika,” alisema.

Alawi Ali Abdalla (36) mzaliwa wa Kisiwani kwa Bint Abeib, katika Wilaya ya Wete-Pemba, alisema kuwa: “mimi sijisiki raha sana mpaka pale nitakapoungana na familia yangu ilioko kisiwani na kunipokea hapo nitajisikia na kujiona niko nchini mwangu”.

Nae , Rashid Abdalla Said  (32) mzaliwa wa Msingini Chake Chake aliishukuru Serikali ya Tanzania kwa mashirikiano makubwa na serikali ya Somalia hali iliyowafanya warudi nyumbani wakiwa salama.

Aliomba kuhakikishia usalama wao ,na iwapo watapatiwa hilo basi watakuwa na ushawishi mkubwa kwa wale wenzao ambao kwa sasa hawajaamuwa kurejea Tanzania.

Mkuu wa Mkoa wa Kusini Pemba, Meja (mstaafu) , Juma Kassim Tindwa, akiwapokea wananchi hao aliwataka warejee makwao kwa amani na utulivu na waendelee kushirikiana na familia zao katika ujenzi wa taifa.

Alisema: “ Zanzibar mulioiacha sio hii iliopo sasa , imebadilika kwa kiasi kikubwa , ina utulivu na iko shwari kila mmoja nalitenda analolitaka alimradi havunji sheria, hivyo navyi karibuni na musijiingize katika makundi ambayo hayaitakii mema Zanzibar”.

Alisema mjenga nchi ni mwananchi mwenyewe , na mvunja nchi na mwananchi mwenyewe hivyo wawe tayari kuishi kwa amani  na kujiletea maendeleo na kuwa tayari kushirikiana na wananchi wengine kwa ajili ya kuilinda na kuitetea amani iliopo kwani ndio njia pekee ya kuleta maendeleo ya haraka.

Afisa wa Shirika linalowahudumia wakimbizi  kanda ya Somali na Kenya, Bruno Geddo , alisema kuwa anashukuru sana kuona kwamba tatizo la wakimbizi hao kuwarejesha makwao limepatiwa ufumbuzi na sasa wamesha wafikisha katika familia zao ambazo wamepoteana nazo kwa muda mrefu .

Alisema kuwa UNHCR, inaamini kuwa wananchi hao ambao wamerejea makwao watapokelewa na jamaa zao na kushirikiana nao kwa kila hali na juhudi za kuwarejesha wale ambao wamebakia huko Somalia zitaendelea.
Alisema UNHCR itazipatia familia hizo chakula kwa muda wa miezi minne pamoja na mtaji wa kuanza maisha mapya.

Nae  Msaidizi Kamishna  wa Uhamiaji Zanzibar, Abdi Bulushi Juma, alisema kuwa wakimbizi hao wamekubali kwa hiari yao kurejea nyumbani  baada ya kuweko Somalia kwa muda mrefu.
Wakimbizi hao wamewasili kisiwani Pemba, wakiwa na familia zao wakiwemo wake na watoto ambao waliwapata wakiwa Somalia miongoni mwao wakiwa  wanawake wa Kisomali.

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.