Habari za Punde

Wakulima Morogoro Wapewa Mafunzo Kilimo Hai


Na Rose Chapewa, Morogoro
WAKULIMA 30 kutoka katika kijiji cha Konga kata ya Mzinga Manispaa ya Morogoro wamepata mafunzo mbalimbali ya kilimo hai, ikiwemo namna ya kudhibiti wadudu waharibifu na magonjwa, pamoja na kutengeneza  dawa zitokanazo na mimea.

Mafunzo hayo  ambayo yaliyokuwa ya siku kumi yalitolea na Shirika lisilokuwa la kiserikali linalojishughulisha na Kilimo Endelevu Tanzania SAT mkoani Morogoro, huku lengo likiwa ni kutoa mafunzo hayo kwa wakulima 100 hadi kumalizika kwa mwaka huu.

Akizungumza na Zanzibar Leo, Mkurugenzi wa Shirika hilo Jeneth Maro alisema lengo la mafunzo hayo ni kuchangia  kuongeza uhakika wa chakula na kupunguza umasikini kwa kutoa
na kuelekeza njia nzuri ya teknolojia katika kilimo.

Alisema  pia kutoa mwongozo na ushirikiano kwa wakulima, ili kuendana katika njia ya kilimo endelevu na kuweza kuongeza uzalishaji wa  mazao kwa kutumia mbinu ambazo ni rafiki wa mazingira.

Aliyataja masomo waliyofundisha kuwa ni kilimo endelevu, kanuni za kilimo hai, rutuba ya udongo, kupandikiza miche, mboji, na mboji iliyoboreshwa (double super), namna ya kutayarisha shamba ama bustani, kitalu na matunzo yake.

Nyingine ni kilimo mseto, mtandazo, teknolojia ya EM, shamba mfuko, teknolojia ya sukuma - vuta, bustani kichunguu, marafiki wa mkulimna, chai ya samadi na mimea, kilimo cha mbogamboga, wadudu waharibifu, magongwa,magugu na namna ya kuthibiti wadudu waharibifu,  magonjwa na dawa zitokanazo na mimea.

Mmoja wa washiriki aliyejitambulisha kwa jina la Abdu Kondo alisema kutoka na mafunzo hoyo amejifunza kuepuka matumizi ya vyakula vitokanavyo na mazao yaliyowekwa kemikali.

Alisema   mafunzo hayo yamemwezesha kutambua athari za utumiaji vyakula vyenye kemikali, na kwamba yanaathiri afya ya mlaji na kuharibu mazingira, na kwamba kwa sasa atalima mazao ambayo hatatumia kemikali wala kula vyakula vya aina hiyo.

Naye Mshiriki Pantaleo Martin alisema amejifunza namna ya kuandaa dawa za mimea pamoja na mbolea, ambazo hazina kemikali na hazina madhara kwa mlaji na kwamba kwa sasa hatatumia tena dawa za dukani.

Alisema amejifunza kuandaa dawa za mazao zenye kutumia miti ambayo aliitaja baadhi kuwa alizeti pori, papai na alovera, na kwamba atalima kwa kutunza mazingira ili kuhakikisha yanakuwa endelevu.

Aidha Mkurugenzi wa shirika hilo alisema, katika maonesho ya Kilimo Nane nane anatarajia kualika wakulima 150 kutoka katika meneo mbalimbali mkoani hapa.

Alisema lengo ni kusambaza kilimo endelevu kwa wakulima wengi nchini  kwa kuwa hawafahamu, ambapo wanatakiwa kujua athari zinazoendelea kutokana na kilimo kinachotumia kemikali, ili wachukue tahadhari kunusuru mazingira.

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.