Habari za Punde

Sita kizimbani wakishukiwa ghasia Bububu

Na Khamisuu Abdallah

WATU sita  wanaoshukiwa kufanya vurungu katika uchaguzi mdogo wa  jimbo la Bububu wamefikishwa  mahakamani kujibu mashtaka yanayowakabili.

Watu hao wamefikishwa mbele ya Hakimu Mdhamini wa mahakama ya Wilaya Mwanakwerekwe, Janet Nora Sekihola kujibu mashitaka ya shambulio la hatari.

Washitakiwa hao ni Mohammed Ali Amour (39) , Juma Omar Juma (44) wote wakaazi wa  Beitras na Mohammed Yussuf Ali (28) mkaazi wa Kinuni.

Wengine ni Omar Bakar Faki (40), Khamis Ruwekh Khamis (25)  na Khelef Mohammed Juma (18) ambao wote ni wakaazi wa Mwanyanya Wilaya ya Magharibi Unguja.

Wote hao kwa pamoja wameshtakiwa kwa makosa matatu tofauti ya shambulio la hatari chini ya kifungu cha 225 cha kanuni ya adhabu sheria namba 6 ya mwaka 2004 sheria za Zanzibar.


Mahakama iliambiwa kuwa washtakiwa hao waliwashambulia watu watatu tofauti katika maeneo mbalimbali ya miili yao na kuwasababishia maumivu makali.

Waliodaiwa kushambuliwa ni Ashura Machano Makame, aliepigwa kisu cha mkono wa kushoto kwenye kiganja, Salum Khamis Bakar aliepigwa kisu kwenye kalio la mkono wa kulia na Hassan Haji Pili aliepigwa magongo kichwani na mgogoni na sehemu nyengine za mwili wake.

Matukio yote hayo yamedaiwa kutokea Kibweni Wilaya ya Magharibi Unguja majira ya saa 3:45 asubuhi ya Septemba 16 mwaka huu.

Licha ya washitakiwa hao kukana mashitaka hayo upande wa mashitaka uliongozwa na Mwanasheria wa Serikali Said Mohammed Ahmed kutoka ofisi ya Mkurugenzi wa Mashitaka (DPP) ulidai mahakamani hapo kuwa upelelezi wake bado haujakamilika.

Hivyo uliiomba mahakama kuiharisha kesi hiyo na kuipangia tarehe nyengine kwa ajili ya kutajwa ambapo Hakimu Janet aliiharisha hadi Oktoba 1  mwaka huu.

Washitakiwa wametakiwa kusaini dhamana ya shilingi 500,000 za maandishi pamoja na mdhamini mmoja kila mshitakiwa mdhamini ambae atawasilisha kima kama hicho cha fedha taslim pia wawe na vitambulisho vinavyotambulika pamoja na barua za Sheha wa Shehia wanazoishi. 
           

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.