Habari za Punde

JK azindua barabara Msata-Bagamoyo·Imegharimu bilioni 89.6/=



Na John Gagarini, Bagamoyo


RAIS Jakaya Kikwete amesema barabara ni mshipa wa fahamu wa uchumi wa nchi .

Aliysema hayo jana katika kijiji cha Kiwangwa wilayani Bagamoyo mkoani Pwani wakati wa uzinduzi wa barabara ya Msata- Bagamoyo yenye thamani ya shilingi bilioni 89.6.

Alisema kutokana na umuhimu huo nchi yoyote ambayo haina barabara nzuri haiwezi kuwa na uchumi bora kwani hicho ni kichocheo cha kuboresha huduma za maendeleo kwa wananchi.

"Barabara ni kiungo muhimu katika kuleta maendeleo ya nchi yoyote ile hivyo kuzinduliwa barabara hii kutasaidia nchi kujiletea maendeleo na kwa wakazi wa mkoa wa Pwani ni fursa pekee ya kujiletea maendeleo kwa kutumia rasilimali zilizopo," alisema Rais Kikwete.
 

Aliongeza kuwa serikali yake imeweka mikakati mbalimbali kuhakikisha barabara zinajengwa katika kiwango kinachostahili ili maendeleo yaweze kukua.

"Wakazi inapopita barabara hii ni vyema mkatumia fursa iliyopo kujiletea maendeleo yao kwani magari yote kutoka mikoa ya Kasakazini yatakuwa yakipita hapa hivyo itakuwa ni nafasi yenu kuzalisha mazao ya chakula na matunda kwa kutumia soko litakalokuwepo," alisema.

Aliwataka wananchi watakaotumia barabara hiyo kuitunza kwani serikali imetumia gharama kubwa kuijenga hasa ikizingatiwa fedha hizo ni za ndani na si za wafadhili.

Awali akimkaribisha kuzindua barabara hiyo, Waziri wa Ujenzi Dk. John Magufuli alisema  barabara hiyo ina urefu wa kilomita 64 ambapo jumla ya kilometa zaidi ya 20 ndizo zilizobakia na inatarajiwa kukamilika ifikapo Juni 2013.
Dk. Magufuli alisema barabara za kiwango cha lami zilizojengwa kwa awamu ya nne ni kilomita 11,154 ambapo nchi ilipokuwa inapata uhuru ilikuwa ni kilomita 1,330 na baada ya miaka 50 ilikuwa ni kilomita 6,500 za lami.

"Nitashangaa kusikia watu wakisema kuwa serikali haijafanya lolote tuwe wakweli  haya yaliyofanyika ni maendeleo hivyo lazima tuipongeze serikali yetu kwa kupiga hatua na tusimsifie mtu anapokufa tumsifu hata kabala hajafa kwani kama kafanya jambo zuri lazima tumpongeze," alisema Dk. Magufuli.

Alisema anashangaa kusikia watu wakibeza safari za nje za rais lakini ndizo zilizozaa matunda kama hayo na kusisitiza kuwa  mtu anapoomba lazima akutane na yule anayemwomba.

Alitoa wito kwa wale wote waliolipwa kupisha barabara hiyo kuondoka kwenye eneo la hifadhi ya barabara na wale watakaojenga sasa hawatalipwa fidia yoyote.

Ujenzi wa barabara hiyo ulianza mwaka 2008 ambapo kampuni ya kwanza ya Tacopa ilinyang’anywa ujenzi huo mwaka mmoja baadaye baada ya kushindwa kutekeleza makubaliano.

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.