Habari za Punde

Wawakilishi wataka TBC, ZBC kushirikiana



Na Juma Mmanga, Dar

  WAJUMBE wa Kamati ya Mifugo, Utalii, Uwezeshaji na Habari ya Baraza la Wawakilishi la Zanzibar, wameshauri kuongezwa ushirikiano kati ya Shirika la Utangazaji Tanzania (TBC) na Shirika la Utangazaji la Zanzibar (ZBC) ili kusaidia harakati za maendeleo nchini kwa vile vyombo hivyo ni mali ya umma.

Wajumbe hao walieleza hayo walipotembelea Ofisi za TBC 1 na TBC Taifa, katika ziara ya kikazi iliyoandaliwa na Wizara ya Habari, Utamaduni, Utalii ili kuwajengea uelewa Wajumbe hao kuhusiana na uendeshaji wa vyomb vya habari nchini.

Akitoa shukurani kwa uongozi wa TBC, Mjumbe wa Kamati hiyo, Asaa Othman Hamad, alisema kuna umuhimu mkubwa wa vyombyo hivyo kusaidiana kwani malengo yake yanafanana ambayo ni kutoa taaluma na kuwaelimisha wananchi kushiriki katika mipango ya maendeleo nchini.


Mapema Kamati hiyo ilitembelea Ofisi za Wizara ya Habari, Utalii na Michezo Zanzibar zilizoko jengo la Wizara ya Fedha Zanzibar Mjini Dar es Salaam, kuona studio ya ZBC na kuzungumza na wafanyakazi wa ofisi hiyo.

Mbali ya kupongeza juhudi zinazochukuliwa na wafanyakazi wa Ofisi hiyo, Kamati hiyo ilipongeza hatua ya Wizara kuanzisha ofisi Dar es Salaam, ambayo itasaidia kuimarisha ushirikiano pamoja na kuchangia kuongezeka mapato ya Serikali.

Jioni Kamati hiyo ikifuatana na Uongozi wa Wizara ya Habari, chini ya Naibu Waziri wake Bihindi Hamad Khamis na Naibu Katibu Mkuu, Issa Mlingoti, ilitembelea Chuo cha Utalii Dar es Salaam, ili kuona namna chuo hicho kinavyoendeshwa ili kupata cha kushauri katika uendeshaji wa Chuo cha Maendeleo ya Utalii Zanzibar.

Kamati hiyo iliongozwa na Makamu Mwenyekiti wake, Mohammed Said Dimwa na Wajumbe Ali Mzee Ali, Asaa Othman Hamad, Salim Abdalla Hamad, Abdi Mosi Kombo, Kazija Khamis Kona, Viwe Khamis Abdalla na Bihindi Hamad Khamis, ambae pia ni Naibu Waziri wa Habari, Utamaduni, Utalii na Michezo Zanzibar.

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.