MELI kubwa ya abiria kutoka kampuni ya Azam Marine
imewasili visiwani Zanzibar jana tayari
kwa kuanza safari zake kati ya Unguja, Pemba na Dar es Salaam.
Meli hiyo iliyowasili bandari ya Malindi saa 8
mchana ikitokea nchini Ugiriki, ambapo ilitumia muda wa siku 14 hadi kuwasili
kwake inatarajiwa kuanza kazi siku za hivi karibuni.
Akizungumza na waandishi wa habari bandarini hapo,
Mkurugenzi Mkuu wa Kampuni hiyo, Hussein Mohammed Said alisema kuwasili salama
kwa meli hiyo ni moja ya hatua muhimu ambayo kampuni yake ilikuwa ikitarajia
katika azma yake ya kuwaondolea adha ya
usafiri wananchi wa Zanzibar.
Alisema meli hiyo inayojulikana kwa jina la Azam
Sea Link 1 ni meli kubwa ya kisasa katika
ukanda wa Afirka Mashariki, ambayo itakuwa na uwezo wa kuchukua abiria
1500,mizigo, gari 240 yakiwemo malori 40 kwa wakati mmoja bila ya usumbufu wa
aina yoyote.
Aliongeza kuwa kutokana na meli kuwa na viwango
vinavyokidhi kimataifa ana imani kubwa kuwa hivi sasa wananchi wanaofanya
safari kati ya visiwa hivyo, wataweza kuondokana na adha ya usafiri ambayo kwa
muda mrefu umekuwa ukiwakabili.
“Lengo la kampuni ni kuhakikisha wananchi wa
Zanzibar wanaondokana na adha ya usafiri, hivyo tumaini langu kubwa ni kuwa
kilio cha wananchi kitaweza angalau kuondoka baada ya kuwasili kwa meli hii,” alisema.
Akizungumzia kuhusu nauli kwa abiria watakaosafiri na meli hiyo,
Hussein alisema kampuni hiyo mara nyingi imekuwa ikiangalia hali za wananchi
wake hivyo, atahakikisha inaweka nauli ambayo kila mwananchi ataweza kumudu,
kwa vile hali ya wananchi wengi ni maskini.
Hivyo amewataka wananchi kuwa tayari kwa ajili ya
kuitumia meli hiyo mara tu itakapoanza kufanya kazi katika kipindi kifupi
kijacho, kwa kutoa ushirikiano kwa kampuni yake ambayo imedhamiria kuwekeza
zaidi katika usafiri wa bahari.
Aidha aligusia ujio wa boti mpya ya Kilimanjaro 4
ambayo alisema tayari mipango imefanyika ya kuhakikisha kuwa boti hiyo inafika Zanzibar nchini si muda
mrefu ujao.
No comments:
Post a Comment