Na Othman
Khamis, OMPR
ZANZIBAR itaendelea kuwa mshirika mkubwa wa Jamuhuri ya
Watu wa Cuba kutokana na historia ya muda mrefu kati ya mataifa hayo mawili
rafiki tokea Mapinduzi ya Zanzibar ya mwaka 1964.
Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar, Balozi Seif Ali
Iddi alitoa kauli hiyo wakati alipokuwa akizungumza na Balozi wa Jamuhuri
ya Watu wa Cuba nchini Tanzania, Ernesto Gomez Diaz aliyefika nyumbani kwake
Mazizini nje kidogo ya mji wa Zanzibar kumuaga baada ya kumalizika muda
wake wa utumishi Tanzania.
Balozi Seif alisema wananchi wa Zanzibar kwa muda mrefu
wameshuhudia juhudi kubwa za Cuba katika kuunga mkono maendeleo na ustawi wa jamii
wa wananchi wa Zanzibar .
Aliitaja sekta ya afya kuwa ni miongoni mwa maeneo
yaliyopata fursa ya kuimarika kitaalamu na utendaji kufuatia mpango wa wataalamu
wa mabingwa wa afya wa Cuba kuwafundisha madaktari wazalendo nchini.
Balozi Seif alimueleza Balozi wa Cuba kwamba mpango
huo unaonyesha ishara njema ya kupata wataalamu wazalendo wanaotarajiwa
kutoa huduma za afya mara wamalizapo mafunzo yao.
“Kwa muda mrefu tulikuwa tukishuhudia vijana wetu wengi
wanaopata fursa za masomo ya juu nje ya nchi hutoweka mara wamalizapo masomo
yao bila ya kujali kuwa wanaitia hasara nchi yao kwa tamaa ya maisha
mazuri zaidi,”alisema.
Alimpongeza Balozi Diaz kwa juhudi zake za kuendelea
kuunganisha nguvu ya uhusiano uliopo kati ya Zanzibar na Cuba.
Mapema Balozi huyo Cuba alielezea matumaini yake kwamba mpango
wa kufundisha madaktari wazalendo chini ya usimamizi wa madaktari mabingwa wa
Cuba utasaidia kupunguza uhaba wa madaktari Zanzibar.
BaloziErnesto alisema katika kuimarisha uhusiano wa pande
hizo mbili Cuba inakusudia kuongeza fursa za masomo kwa vijana wa Kitanzania
hatua ambayo hata Zanzibar itafaidika.
No comments:
Post a Comment