Habari za Punde

Wafanyabiashara Pemba kupatiwa elimu kwa mtandao

Na Masanja Mabula, Pemba
WIZARA ya Biashara, Viwanda na Masoko Pemba, imekusudia kutoa elimu ya biashara kwa wafanyabiashara wa Pemba ili waweze kuimarisha biashara zao kwa mfumo wa kutumia mtandao.
Akizungumza na mwandishi wa habari hizi huko ofisini kwake Wete, Ofisa Mdhamini Wizara hiyo Pemba, Hemed Suleiman Abdalla, amesema kuwa mfumo huo utawarahisishia utendaji wa kazi kwa wafanyabiashara kwani watakuwa na uwezo wa kuagizia bidhaa kutoka nje ya nchi wakiwa kisiwani Pemba.
Alisema utaoji wa elimu hiyo utafanywa na watendaji wa Wizara hiyo kwa kushirikiana na taasisi nyingine ambazo zinahusiana na masuala ya fedha ikiwemo Bodi ya Mapato Zanzibar (ZRB), Halmashauri, Mabaraza ya miji pamoja na jumuiya ya wafanyabiashara na wakulima Zanzibar  (ZNCIA).

Alifahamisha kuwa uamuzi wa kuwapa elimu ya biashara wafanyabiashara wa Pemba ni kutaka kuimarisha hali zao za biashara sambamba na kuwafanya waingie katika biashara ya kisasa jambo ambalo linawafanya waweze kuongeza kipato na kuimarika kwa mitaji yao.
“Ni utaratibu mzuri, kwani wafanyabiashara watakuwa na uwezo wa kuagizia bidhaa wakiwa kisiwani hapa na hivyo kupunguza gharama za kufuatilia bidhaa ambapo hutumia fedha nyingi kusafiri na kusafirisha mizigo yao," alifahamisha.
Katika hatua nyingine, Hemed aliwataka wafanyabiashara kisiwani Pemba kutumia fursa hiyo kuagizishia bidhaa kutoka nje ya nchi  na kusisitiza kuwa uingizaji wa vyakula hauna kizuwizi isipokuwa kila mmoja ana uhuru kuingiza alimradi afuate sheria na taratibu.
Akizungumzia suala la kuimarisha kilimo cha mikarafuu, ofisa huyo, alisema kwa sasa wana mpango wa kupita kila wilaya na kuzungumza na wakulima ili kuwaelimisha juu ya mkataba ulioingiwa na serikali wa kuitangaza karafauu kwenye soko la dunia.
Alisema mkataba huo utawanufaisha wakulima na serikali kwani karafuu wa Zanzibar itakuwa na inajulikana katika soko la dunia na hatatokea mtu kuisafirisha kwa njia ya magendo.
Hivyo aliwaomba wakulima kuunga mkono juhudi za serikali za kuitangaza karafuu kwenye soko la dunia ili lengo lililokusudiwa liweze kufikiwa.

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.