Habari za Punde

Msichana juu kidato cha pili Zanzibar · Wavulana watesa darasa la 7



Na Hafsa Golo

MWANAFUNZI Ruwaida Mohmoud Ramsa  anaesoma skuli ya Mtoni ameibuka mwanafunzi bora kitaifa katika mitihani ya kidato cha pili iliyofanyika Novemba mwaka uliopita.

Ruwaida amechaguliwa kuwa mwanafunzi bora kati ya wanafunzi 19,676 waliofanya mitihani hiyo.

Nafasi ya pili imechukuliwa na mvulana Saleh Abdalla Juma kutoka skuli ya Mwanakwerekwe  ‘B’  huku nafasi ya tatu ikichukuliwa na mvulana mwengine, Khalid Muhidini Haji kutoka skuli ya Mwembemakumbi.

Kwa upande wa mitihani ya darasa la saba, mwanafunzi bora kitaifa ni Abdulsalami Juma Khamis kutoka skuli ya Mtopepo ‘A’, akifuatiwa na Said Mkubwa Salum kutoka skuli ya Kiembesamaki na nafasi ya tatu kitaifa ikichukuliwa tena na mvulana, Abdulrazak Machano Hassan kutoka skuli ya Mtopepo B.


Akitangaza matokeo hayo jana, Waziri wa Elimu na Mafunzo ya Amali, Ali Juma Shamuhuna alisema wanafunzi 12 wote wa kidato cha pili wamefutiwa matokeo baada ya kubainika kufanya udanganyifu, ambapo ni upungufu wa kesi 5 ikilinganishwa na mwaka 2011 ambapo waliofutiwa matokeo walikuwa 17.

Alisema kati ya wanafunzi waliofanya udanganyifu, wanane wanatoka skuli ya Donge.
Wengine ni kutoka skuli ya Regeza Mwendo (3) na Mwembeladu  mwanafunzi mmoja.

Kwa upande wa watahiniwa wa kidato cha pili, wanafunzi 11,195 wamechaguliwa kujiunga kidatu cha tatu katika skuli mbali mbali, kati yao wasichana ni 6,768 na wavulana 4,427, ambapo ni sawa na asilimia 56.9 ya watahiniwa wote.

Katika ngazi hiyo kulikuwa na watahiniwa 19,679 kati yao wasichana 11,045 na wavulana 8,644.

Takwimu hizo zinaonesha wanafunzi  8,484 wameshindwa kabisa kuendelea na masomo ya kidato cha tatu.

Aidha wanafunzi walioandikishwa kufanya mitihani ya kidato cha pili walikuwa 21,019 lakini waliofanya mitihani hiyo walikuwa 19,679 hivyo wanafunzi 1,340 hawakufanya mitihani hiyo kutokana na sababu mbali mbali ambazo hata hivyo hazikutajwa.

Shamuhuna alisema kiwango cha ufaulu kwa mitihani ya kidato cha pili kimeongezeka kwa asilimia 0.8 ikilinganishwa na mwaka 2011.

Alizitaja skuli za Bwefum, Umbuji, Uzi,Ubago,Pongwe Pwani, Michamvi na Mtende, kwa Unguja kuwa ndio skuli zilizofanya vibaya zaidi kwa kupasisha wanafunzi kidogo na kwamba madarasa yao yatafungwa.

Kwa Pemba alizitaja skuli tatu za tiro kuwa ni Kisiwa Panza, Makoongwe na Ndagoni ambazo zimepasisha wanafunzi wanane, saba na sita na hivyo madarasa yao pia yatafungwa.

Kwa upande wa watahiwa wa darasa la saba,  wanafunzi 17,511 wamefaulu kujiunga na kidato cha kwanza , kati yao wasichana 9652 na wavulana 7859 sawa na asilimia 76, ambapo kuna upungufu wa asilimia 5.2 ikilinganishwa na mwaka 2011.

Aidha alisema wanafunzi wa darasa la saba waliopata asilimia 60 hadi 100 ni 1,501.

Wanafunzi walioandikishwa kufanya mitihani hiyo walikuwa 24,940 ambapo wasichana 12,960 na wavulana 11,980.

Waziri huyo alisema waliofanya mitihani ni 23,039 ambapo wanafunzi 1901 hawakufanya mitihani hiyo kutokana na sababu mbali mbali.

Matangazo rasmi ya majina ya waliofaulu yatatangazwa baada ya taratibu kukamilika

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.