Habari za Punde

Warka wa Maalim Seif kwa tume ya kuratibu maoni ya katiba


ZANZIBAR NA MUSTAKBALI WA MUUNGANO

 

Maoni Binafsi ya Maalim Seif Sharif Hamad, Makamu wa Kwanza wa Rais wa Zanzibar na Katibu Mkuu wa The Civic United Front (CUF – Chama Cha Wananchi)

 

 

 

UTANGULIZI

 

Nina heshima kubwa ya kuwasilisha maoni yangu binafsi kwa Tume ya Mabadiliko ya Katiba kuhusiana na namna na jinsi nchi zetu mbili, Zanzibar na Tanganyika, zinazounda Jamhuri ya Muungano zinavyopaswa kuongozwa kupitia mfumo mpya wa kikatiba utakaopatikana baada ya kukamilika mchakato unaoendelea sasa wa kupata Katiba Mpya.

 

Nafasi iliyopo mbele yetu ni adhimu sana kwa wananchi wa Zanzibar na Tanganyika kutoa maoni yao juu ya katiba mpya wanayoitaka ili kuamua khatima ya nchi zao, wanataka ziwe na mahusiano ya aina gani na ziongozwe katika utaratibu upi.

 

Kwa muktadha huo basi ni wazi Katiba inayokusudiwa kutoa muongozo kwa wananchi wake inajengwa na mambo mengi ambayo kimsingi yanapaswa kujadiliwa kwa kina na baadaye kufikia muwafaka wa kitaifa katika kupata Katiba Mpya.

 

Pamoja na ukweli huo, ni ukweli pia kuwa kwetu sisi Wazanzibari ni fursa pekee ya kuangalia upya uhusiano kati ya Zanzibar na Tanganyika, ni aina gani ya muungano tunaoutaka na utakaoweza kukabiliana na changamoto zilizopo na kwa hivyo basi maoni yangu yatajikita katika eneo hilo tu.

 

Tume ya Mabadiliko ya Katiba imetoa mwongozo ambao unawataka watoa maoni wajikite katika maeneo makuu tisa (9). Maeneo hayo ni kama ifuatayo:

 

(a)                       Misingi na Maadili ya Kitaifa;

(b)                      Madaraka ya Wananchi;

(c)                       Muundo wa Nchi na Taifa ndani ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania;

(d)                      Haki za Binadamu na Wajibu wa Wananchi;

(e)                       Ardhi, Maliasili na Mazingira;

(f) Mihimili ya Nchi:-

(i)             Ardhi;

(ii)          Watu; na

(iii)       Utawala.

(g)                       Mihimili ya Utawala:-

(i)             Serikali;

(ii)          Bunge; na

(iii)       Mahkama.

(h)                      Serikali za Mitaa, Muundo na Mamlaka yake;

(i) Vyombo vya Ulinzi na Usalama.

 

Yanapotazamwa kwa undani maeneo hayo itaonekana kwamba takriban mengi si mambo ya Muungano na hivyo hayawahusu wananchi wa Zanzibar ambao kwa mujibu wa Mkataba wa Muungano wa 1964 yanasimamiwa na Zanzibar yenyewe ambayo ina mamlaka kamili (exclusive jurisdiction) kuhusiana na mambo yote yasiyo mambo ya Muungano. Hata yale maeneo ambayo yanaweza kuwahusu Wazanzibari kwa mfano misingi na maadili ya kitaifa, madaraka ya wananchi, mihimili ya utawala (Serikali, Bunge na Mahkama) na vyombo vya ulinzi na usalama, kuhusika kwao kutakuwa ni kwa kiasi kile yanapohusika na uendeshaji wa Muungano. Ndiyo kusema kwamba jambo lililo katikati ya mjadala kwa Wazanzibari katika mchakato huu ni Muungano wenyewe.

 

Kwa msingi huo, maoni yangu binafsi ninayoyatoa hapa yatajikita kwenye kile ambacho Wazanzibari walio wengi wamekuwa wakikizungumzia mbele ya Tume ya Mabadiliko ya Katiba – Muungano wa Zanzibar na Tanganyika. Sehemu kubwa ya waraka wangu huu wa maoni ninayoyawasilisha mbele ya Tume ya Mabadiliko ya Katiba msingi wake ni waraka wangu nilioutoa mwaka 2008. Nimeamua kuutumia waraka huo kwa sababu kwa kiasi kikubwa bado maoni yangu na sababu zake yanabaki kama yalivyokuwa. Kilichobadilika ni kile kinachohusu nini naamini unapaswa kuwa ufumbuzi wa matatizo ya Muungano huu ambayo hayo ninayaeleza mwishoni mwa waraka huu pamoja na sababu zilizopelekea mabadiliko hayo ya fikra.

 

 

MISUKOSUKO KATIKA MUUNGANO

 

Muungano wa Zanzibar na Tanganyika umepita katika masaiba kadhaa tokea kuasisiwa kwake takriban miaka 49 iliyopita lakini mtikisiko ulioukumba katika siku za karibuni ni mkubwa sana. Ni mkubwa kwa sababu umegusa kiini cha Muungano huu ambapo suala linaloulizwa ni iwapo kwa kule kukubali kushirikiana katika baadhi ya mambo, je, Zanzibar na Tanganyika zimejifuta na hivyo kupoteza hadhi zake kama nchi? Hilo limekuwa ndiyo suala kubwa linaloulizwa na Wazanzibari hasa baada ya Waziri Mkuu Mizengo Pinda kutamka Bungeni kwamba Zanzibar si nchi.

 

Hakuna awezaye kubisha kwamba tokea kuasisiwa kwake, Muungano huu umejengeka kutokana na misingi ya khofu, kutiliana shaka na kutokuaminiana baina ya pande mbili zinazouunda, ambako wakati mwengine kumepelekea hata kutishia uhai wa Muungano wenyewe.

 

Muungano umekuwa gumzo kuu katika takriban kila mjadala wa katiba na siasa katika nchi yetu. Umejitokeza na kujionyesha hivyo katika mwaka wa mwanzo wa Muungano kuhusiana na sakata la kuwa na Ubalozi wa iliyokuwa Ujerumani Magharibi kwa upande wa Tanganyika na Ubalozi wa iliyokuwa Ujerumani Mashariki kwa upande wa Zanzibar, kuhusiana na uwakilishi wa Zanzibar katika Bodi ya Sarafu ya Afrika Mashariki na uanzishwaji wa Benki Kuu ya Tanzania (BOT) mwaka 1964 – 1966, wakati wa kuunganisha vyama vya ASP na TANU kuunda Chama Cha Mapinduzi (CCM) mwaka 1977, katika mjadala wa marekebisho ya Katiba wa 1983/84 na hatimaye kujiuzulu kwa Rais wa pili wa Zanzibar Sheikh Aboud Jumbe, wakati wa kuondolewa katika Uwaziri Kiongozi kwa mwandishi wa maoni haya na hatimaye kufukuzwa katika CCM na wenzake 6 mwaka 1988, katika harakati za madai ya kutaka kura ya maoni kuhusiana na Muungano huo mwaka 1989/90, wakati wa mjadala wa kuanzishwa vyama vingi mwaka 1991, katika sakata la Zanzibar kujiunga na Umoja wa Nchi za Kiislamu (OIC) mwaka 1993, wakati wa mjadala wa G-55 kudai kuanzishwa kwa Serikali ya Tanganyika ndani ya Muungano mwaka 1994, katika mjadala wa marekebisho ya 11 na 14 ya Katiba ya Muungano mwaka 1994/95, wakati wa kampeni za uchaguzi mkuu wa 1995 na ule wa 2000 na karibuni kabisa kuhusiana na suala la matarajio ya ugunduzi wa mafuta visiwani Zanzibar, harakati za kuanzisha Shirikisho la Afrika Mashariki na pia baada ya kupitishwa kwa Marekebisho ya Kumi ya Katiba ya Zanzibar ya 1984 yaliyofanywa mwaka 2010.

 

Ukiondoa kuibuka kwake katika mijadala mikubwa ya kikatiba na kisiasa nchini, kwa upande mwengine katika uendeshaji wa shughuli za Serikali za kila siku, “matatizo na vikwazo kadhaa ya kiutawala na kiutendaji” vimekuwa vikiripotiwa kila mara kwamba vinakwamisha uimarishaji wa Muungano.

 

Tume na Kamati kadhaa zimeundwa kuainisha matatizo ya Muungano na kupendekeza njia za kuyatatua. Serikali ya Jamhuri ya Muungano imeunda Tume na Kamati zifuatazo, miongoni mwa nyingi, kuhusiana na masuala haya:

 

1.     Kamati ya Mtei

2.   Tume ya Jaji Francis Nyalali (1991)

3.   Kamati ya Shellukindo (1994)

4.   Kamati ya Shellukindo 2 ya kuandaa Muafaka juu ya Mambo ya Muungano baina ya SMZ na SMT.

5.    Kamati ya Jaji Mark Bomani (1995)

6.   Kamati ya Jaji Robert Kisanga (1998)

7.    Kamati ya 'Harmonization'

8.   Kamati ya Masuala ya Simu (Kamati ya Kusila)

 

Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar (SMZ) nayo kwa upande wake iliunda Kamati zifuatazo kwa madhumuni hayo hayo:

 

1.     Kamati ya Baraza la Mapinduzi (Kamati ya Amina) ya 1992

2.   Kamati ya Rais ya Kupambana na Kasoro za Muungano (Kamati ya Shamuhuna)  ya 1997

3.   Kamati ya Rais Kuchambua Ripoti ya Jaji Kisanga (Kamati ya Salim Juma Othman)

4.   Kamati ya Kuandaa Mapendekezo ya Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar juu ya Kero za Muungano (Kamati ya Ramia) ya 2000

5.    Kamati ya Baraza la Mapinduzi juu ya Sera ya Mambo ya Nje

6.   Kamati ya Rais ya Wataalamu juu ya Kero za Muungano ya 2001

7.    Kamati ya Baraza la Mapinduzi ya Jumuiya ya Afrika Mashariki

8.   Kamati ya Mafuta

9.   Kamati ya Madeni baina ya Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar na Serikali ya Muungano wa Tanzania

10.                      Kamati ya Suala la Exclusive Economic Zone (EEZ)

11.Kamati ya Masuala ya Fedha na Benki Kuu

12.                       Kamati ya Rais ya Masuala ya Simu (1996 –1999)

13.                       Kamati ya Baraza la Mapinduzi juu ya matatizo na kero za Muungano na taratibu za kuyaondoa (2004)

 

Ukiacha Tume, Kamati na Ripoti hizo, kuanzia mwaka 1985 kulianzishwa utaratibu wa Kamati ya Pamoja ya Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano na Waziri Kiongozi wa Zanzibar pamoja na Mawaziri wa Serikali zetu mbili ambao ulitarajiwa uwe ndiyo jukwaa la kuzungumzia matatizo kutoka kwa washiriki wakuu wa Muungano huu na kuyapatia ufumbuzi unaofaa. Utaratibu huu uliachwa kwa muda mrefu lakini sasa umerejeshwa upya kufuatia agizo la Rais Jakaya Kikwete alilolitoa katika mkutano na mawaziri na watendaji wakuu wa Serikali yake huko Ngurdoto, Arusha mwezi Februari, 2006. Mikutano hiyo sasa imebadilishwa utaratibu wake na inaongozwa na kusimamiwa na Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano na timu za pande mbili zikiongozwa na Waziri Mkuu kwa upande wa Serikali ya Muungano na Makamu wa Pili wa Rais kwa upande wa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar.

 

Mikutano, Makongamano, Semina na Warsha vimefanywa kujadili masuala haya na kupendekeza hatua za kuchukuliwa. Wasomi na wanafunzi wamefanya tafiti kadhaa na kujipatia shahada na stashahada hadi ngazi ya Ph.D juu ya Muungano lakini bado matatizo yako pale pale na yanaongezeka kila kukicha.

 

Yanayoonekana na kuelezwa kama matatizo, mapungufu, dosari, kasoro na, kwa msamiati wa sasa, kero yamekuwa ndiyo yale kwa yale. Nini basi kiini cha haya? Na vipi tutayatatua?

 

Mimi nimeamua kutoa changamoto kupitia waraka huu kwa kuitazama historia ya Muungano, jinsi ulivyoundwa, matatizo yanayoukabili, nafasi na hadhi ya Zanzibar katika Muungano na nini khatima ya Zanzibar na mustakbali wa Muungano katika mchakato huu tunaoendelea nao wa kupata Katiba Mpya ya Jamhuri ya Muungano. Nitakayoyaeleza yanaweza yakaonekana ni machungu kwa wakati huu lakini yanaweza yakawa ndiyo ufumbuzi mujarab kwa siku zijazo.

 

 

ASILI NA SABABU ZA MUUNGANO

 

Maoni yanayotolewa kuhusu asili na sababu za Muungano yamekuwa yakitofautiana mno. Wapo wanaouleza Muungano huu kuwa ni wa pekee katika bara la Afrika, kwani ndiyo pekee ulioweza kudumu katika kutimiza azma na malengo ya kuleta umoja wa Afrika (Pan-Africanism),[1] na pia wapo wanauona kuwa ni “jaribio la kusisimua la ukoloni mdogo wa nchi moja ya Kiafrika kuiteka na kuitawala nchi nyengine ya Kiafrika.”[2]

 

Kutokana na maelezo na hoja nyingi na zinazokinzana kuhusu asili na sababu za Muungano, si rahisi kusema moja kwa moja kuwa maelezo yepi au hoja ipi ni sahihi. Utangulizi (Preamble) wa Mkataba wa Muungano wa 1964 wenyewe unataja sababu kuu ya kuunganisha nchi za Zanzibar na Tanganyika kuwa ni “maingiliano ya muda mrefu ya watu wa nchi mbili hizi na mahusiano yao ya kidugu na kirafiki … na … kuendeleza umoja wa watu wa Afrika.” Lakini miaka 49 sasa baada ya uzoefu wa Muungano huu, Wazanzibari wanajiuliza kweli haya yalikuwa ndiyo madhumuni ya Muungano huu?

 

Wazo la kuungana linaweza kurudishwa nyuma tokea zama za harakati za ukombozi wa nchi za Afrika. Waasisi na wakuu wa harakati za kupigania Uhuru waliiona mipaka ya nchi zao iliyowekwa na wakoloni kuwa ni ‘mbinu za kibeberu’ zilizotekelezwa kwa ajili ya manufaa na maslahi yao. Kutokana na hisia hizo, mazungumzo ya kuanzisha aina fulani ya umoja miongoni mwa nchi huru za Afrika yalitawala duru za siasa katika miaka ya 5o na 60.

 

Nadharia mbili zilijichomoza. Ya kwanza, ikishadidiwa na Kwame Nkrumah wa Ghana, ilikuwa ikitaka kuasisiwa kwa nchi moja tu ya Afrika nzima iliyoungana ikiwa na Serikali moja kwa bara zima. Nadharia hii ilipingwa na baadhi ya viongozi, wakiongozwa na Mwalimu Julius Nyerere wa Tanganyika, ambao walisisitiza haja ya kuanza na miungano ya maeneo (regional unions) chini ya mfumo wa Shirikisho badala ya kuwa na mpango wa Serikali moja.[3]

 

Katika kulifikia lengo hilo, viongozi wa kisiasa wa nchi tatu za Afrika Mashariki – Kenya, Uganda na Tanganyika – walikuwa wakifanya mikutano ya mara kwa mara kipindi chote cha kati ya mwaka 1961 na 1963 kuona jinsi gani wanaweza kutimiza ndoto hiyo. Mfumo wa Muungano uliokuwa ukiandaliwa ulikuwa ni ule wa Shirikisho. Tamko la Pamoja la viongozi hao lilisema:

 

“Sisi, viongozi wa wananchi na Serikali za nchi za Afrika Mashariki … tunayakinisha nia zetu kuhusu kuwepo kwa Shirikisho la Kisiasa la Afrika Mashariki. Mkutano wetu wa leo unasukumwa na hisia za umoja wa Afrika (Pan-Africanism), na siyo tamaa za maslahi binafsi ya eneo hili. …

 

Ijapokuwa Zanzibar haikuwakilishwa katika mkutano huu, tunapaaswa kuweka bayana kwamba nchi hiyo inakaribishwa kushiriki kikamilifu katika mikutano yetu kwa ajili ya uundwaji wa Shirikisho .”[4]

 

Lakini Umoja wa Afrika (Pan-Africanism) hauonekani kuwa ndiyo dhamira pekee au kama ndiyo dhamira halisi ya Muungano. Wengi wanaamini, na mimi nikiwa mmoja wao, kwamba dhana hiyo ilitumiwa tu kuficha njama za muda mrefu za Mwalimu Nyerere kutaka kuimeza na kuitawala Zanzibar. Katika mwaka 1961, wakati Tanganyika inakaribia kupata Uhuru wake, Mwalimu Nyerere alinukuliwa akisema:

 

“If I could tow that island [Zanzibar] out in the middle of the Indian Ocean, I would do it … I fear it will be a very big headache for Tanganyika.”[5]

 

Yaani, “Kama ningekuwa na uwezo wa kuvikokota visiwa vile [Zanzibar] na kuvitupa nje kabisa, katikati ya Bahari ya Hindi, basi ningefanya hivyo … Nakhofia vitakuja kuiumiza kichwa sana Tanganyika”.

 

Wakati juhudi za kuanzisha Shirikisho la Afrika Mashariki zikiwa zinafifia, Mwalimu Nyerere aliona Zanzibar kama fursa ambayo hakutaka kuipoteza. Katika mazungumzo ya siri kati yake na Rais Abeid Amani Karume wa Jamhuri ya Watu wa Zanzibar, wakakubaliana kuziunganisha nchi mbili hizi. Hakukuwa na ushirikishwaji wa aina yoyote ule wa wananchi wa nchi hizi mbili katika maamuzi haya makubwa. Usiri uliogubika hatua hii kubwa unafichuliwa na si mwengine bali Mwalimu Nyerere mwenyewe pale aliposema:

 

“[Tanganyika] tulipeleka polisi wetu Zanzibar. Baada ya kuyashinda matatizo kadhaa tukaungana. Sisi wenyewe kwa khiyari zetu tulikubaliana kuungana. Karume na mimi tulikutana. Peke yetu wawili tu tulikutana. Nilipomtajia wazo la Muungano, Karume hakufikiri hata mara mbili. Pale pale alinitaka kuita mkutano wa waandishi wa habari kutangaza azma yetu. Nilimshauri asubiri kidogo kwani ilikuwa bado ni mapema mno kuweza kuviarifu vyombo vya habari.”[6]

 

Taarifa hizi ziliendelea kubaki kuwa siri hadi tarehe 26 Aprili, 1964 pale Redio ya Tanganyika ilipotangaza kwamba siku hiyo Marais wawili hao watakutana katika Bunge la Tanganyika kubadilishana Hati za Muungano ambazo zimeunganisha Zanzibar na Tanganyika kuwa Jamhuri moja. Hivyo inaonekana wazi kwamba tokea awali Muungano huu ulikosa ridhaa ya watu. Haukuwa Muungano wa watu, ulioundwa na watu, kwa maslahi ya watu. Bali ulikuwa na umeendelea kuwa ni Muungano uliosimamishwa kwa ridhaa ya watawala pekee.

 

Jambo jengine muhimu kulitaja kuhusiana na mazingira ya uundwaji wa Muungano ni kutokuwepo kwa usawa baina ya wakuu wa nchi mbili hizi wakati wa kuandaliwa Mkataba wa Muungano. Inajulikana wazi kuwa Rais wa Jamhuri ya Tanganyika, Mwalimu Julius Nyerere, alipata fursa ya kushauriwa na kusaidiwa na wataalamu waliobobea wa fani ya sheria waliorithiwa kutoka Serikali ya Kikoloni ya Kiingereza ambao ni Mwanasheria Mkuu wake, Bw. Roland Brown, na Mwandishi Mkuu wa Sheria wa Bunge la Tanganyika (Chief Parliamentary Draftsman) ambaye pia alikuwa Kaimu Mshauri Mkuu wa Sheria wa Serikali (Solicitor General), Bw. P.R. Nines-Fifoot. Kwa upande mwengine, Rais wa Jamhuri ya Watu wa Zanzibar, Mheshimiwa Abeid Amani Karume, hakupata fursa kama hiyo. Mwanasheria Mkuu wa Zanzibar wa wakati huo, Bw. Wolfgang Dourado, amenukuliwa hadharani na hata kuandika waraka akieleza jinsi alivyofichwa habari za maandalizi ya kuundwa Muungano. Mtu mwengine aliyekuwa karibu na Mzee Karume alikuwa Mzee Aboud Jumbe, na yeye pia ameandika kitabu kueleza kuwa hakuwa akijua chochote juu ya mipango ya kuunganishwa Zanzibar na Tanganyika hadi alipoitwa kutoka safarini Pemba na kujulishwa kuwa tayari Mkataba wa Muungano ulishatiwa saini tarehe 22 Aprili, 1964.

 

 

KIINI CHA MATATIZO YA MUUNGANO

 

Kama tulivyokwisha kuona kwamba Muungano wa Tanganyika na Zanzibar uliundwa kupitia Mkataba wa Muungano wa 1964 (Articles of Union). Mkataba huu, kwa kutumia ushahidi wa picha, ulitiwa saini na Rais wa Jamhuri ya Tanganyika, Mwalimu Julius Nyerere, na Rais wa Jamhuri ya Watu wa Zanzibar, Sheikh Abeid Amani Karume, kwa niaba ya nchi zao mbili katika Ikulu ya Zanzibar, tarehe 22 Aprili, 1964.

 

Mkataba wa Muungano wa 1964 (Articles of Union between the Republic of Tanganyika and the People’s Republic of Zanzibar) ni Mkataba wa Kimataifa (an international treaty) na ndiyo maana kwa kuzingatia matakwa ya sheria za kiingereza (English Common Law System) zilizokuwa zikifuatwa na Zanzibar na Tanganyika wakati huo na hadi leo uliweka sharti katika kifungu cha (viii) kwamba unapaswa kuthibitishwa na Bunge la Tanganyika na Baraza la Mapinduzi la Jamhuri ya Watu wa Zanzibar likishirikiana na Baraza lake la Mawaziri ili kuupa nguvu za kisheria ndani ya nchi mbili hizo.

 

Hoja ya kwanza inayojitokeza hapa na ambayo imeshindwa kupatiwa majibu hadi leo ni kushindwa kupatikana kwa nakala halisi (original copy) ya Mkataba huo ikiwa na saini za Rais Nyerere wa Jamhuri ya Tanganyika na Rais Karume wa Jamhuri ya Watu wa Zanzibar. Hoja hii imeibuliwa ndani ya Bunge la Jamhuri ya Muungano na pia katika Mahkama Kuu ya Zanzibar ambako Serikali zote mbili, Serikali ya Jamhuri ya Muungano na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar, zimeshindwa kutoa nakala hiyo licha ya kuahidi kufanya hivyo. Nusura pekee iliyobaki ni kutegemea nakala halisi (iwapo ipo) inayoelezwa kwamba ilikabidhiwa kwa Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa kwa ajili ya kumbukumbu za Umoja huo kujiridhisha kwamba nchi mbili hizi zimeungana. Kuonekanwa kwa nakala halisi ya Mkataba huo ni muhimu sana katika kujiridhisha uhalisia wa kile kilichokubaliwa baina ya nchi zetu mbili.

 

Hoja ya pili ni ile inayohusu utekelezwaji wa matakwa ya uthibitishaji (the want of ratification) wa Mkataba huo kwa upande wa Zanzibar. Upo ushahidi wa kutosha kwamba Bunge la Tanganyika lilikutana na kuuridhia Mkataba huo tarehe 25 Aprili, 1964. Kwa upande mwengine, hakuna ushahidi wowote kwamba Baraza la Mapinduzi likishirikiana na Baraza la Mawaziri la Zanzibar lilikaa kuuridhia Mkataba huo kwa kupitisha Sheria ya Kuthibitisha (Ratification Decree) kama ilivyotakiwa na Mkataba wenyewe. Kwa hakika ushahidi ulioibuliwa na Prof. Issa Shivji katika kitabu chake cha karibuni kabisa, Pan-Africanism or Pragmatism? Lesssons of Tanganyika-Zanzibar Union umeweka wazi pasina chembe ya wasiwasi kwamba Mkataba huo haujaridhiwa na upande wa Zanzibar hadi hii leo.

 

Ukiachilia mbali hoja hizo, na kwa msingi wa hoja tukichukulia kwamba Mkataba huo ni halali, bado ukitazama kwa jicho la sheria, utaona kiini cha matatizo ya Muungano kinatokana na tafsiri ya Mkataba wa Muungano (Articles of Union) wa 1964. Suala kubwa lililoumiza na linaloendelea kuumiza vichwa vya wengi na hivyo kuendelea kuulizwa ni mfumo gani wa Muungano ulikusudiwa kuwekwa na Mkataba huu? Ni muungano wa moja kwa moja (unitary) au wa shirikisho (federal)?

 

Mfumo uliopo sasa ambao ulianza kutekelezwa 1964 ni ule wa serikali mbili – ile ya Jamhuri ya Muungano na ile ya Zanzibar. Tanganyika haikuwekewa serikali yake tofauti; madaraka yake kwa yale mambo yasiyo ya Muungano yalielezwa kwamba yatasimamiwa na kuendeshwa na Serikali hiyo hiyo ya Jamhuri ya Muungano. Hata hivyo, uhalali wa kisheria wa muundo huu umeendelea kuhojiwa na hata kupingwa kwamba hauwakilishi ipasavyo makusudio yaliyomo katika Mkataba ulioanzisha Muungano wenyewe.

 

Mkataba wa Muungano wenyewe hauelezi bayana aina au mfumo wa muungano inaouanzisha lakini uko wazi kuhusiana na mgawanyo wa madaraka (distribution of power) inaouweka na idadi ya mamlaka (number of jurisdictions) zitakazokuwepo. Ibara ya (iii) (a) ya Mkataba huo inaanzisha ‘Baraza la Kutunga Sheria na Mamlaka ya Utendaji’ (Legislature and Executive) ndani ya na kwa ajili ya Zanzibar ikiwa na mamlaka kamili (exclusive authority) kuhusiana na mambo yote yasiyo mambo ya Muungano kwa Zanzibar. Kwa upande mwengine, Ibara ya (iv) ya Mkataba huo inaanzisha ‘Bunge na Mamlaka ya Utendaji’ (Parliament and Executive) ya Jamhuri ya Muungano ikiwa na mamlaka kamili katika eneo lote la Jamhuri ya Muungano kuhusiana na mambo ya Muungano na, pia, ikiwa na mamlaka kamili ndani ya, na kwa ajili ya Tanganyika kuhusiana na mambo yote yasiyo mambo ya Muungano kwa Tanganyika. Kwa hivyo, katika sehemu ya pili, mamlaka mbili tofauti zimechanganywa pamoja.

 

Mjadala mkubwa na mkali umekuja kuhusiana na tafsiri ya Ibara hiyo ya (iv) na kule kuchanganya kwake mamlaka mbili hizo.

 

Haya si masuala ya kisheria tu kama ambavyo baadhi yetu wanataka tuamini (ingawa nayo ni muhimu mno kama ilivyodhihirika hivi karibuni), bali pia ni masuala ya kisiasa kwa vile yanahusisha uwezo wa maamuzi, madaraka na mamlaka, na zaidi mchango wa gharama za uendeshaji na mgawanyo wa rasilimali na mapato kati ya wahusika wakuu. Mambo haya, katika uzoefu wa nchi za wenzetu, ndiyo yaliyopelekea kuvunjika kwa miungano yao kwani huzaa kutiliana shaka na kutokuaminiana. Kwa vile yanachukua sura ya kisiasa (kutokana na sababu nilizozitaja), haya hayana chama wala itikadi kama nitakavyoonyesha huko mbele. Kama alivyowahi kusema Prof. Issa Shivji:

 

“Ultimately, the question of the Union is primarily a political question and no amount of rhetoric about blood and cultural ties will matter when it comes to realpolitik.”[7]

 

Yaani, “Mwisho wa yote, suala la Muungano linabakia kimsingi kuwa ni suala la kisiasa, na inapofikia kwenye siasa hasa, hotuba na kauli kali za jazba kuhusiana na mahusiano ya damu na ya kidugu, zote hazitafaa kitu.”

 

Kwa hakika, kinyume na inavyojaribiwa kuonyeshwa na wengi kwamba Tanganyika imepoteza kila kitu katika muundo huu wakati Zanzibar imekabidhi sehemu tu ya madaraka yake, muundo wa Serikali mbili umepelekea wengi kuamini kwamba kilichofanyika ni kiini macho tu kwani ni Zanzibar iliyokabidhi sehemu muhimu ya mamlaka yake (mahusiano ya nchi za nje, ulinzi na usalama, uraia, kodi na ushuru, sarafu, nguvu kuu za kuendeshea uchumi na mengineyo) kwa Tanganyika na kisha Tanganyika ikajigeuza jina na kujiita Jamhuri ya Muungano. Na haya si maoni ya ngumbaru (kwa lugha ya Mwalimu Julius Nyerere) bali ni maoni ya watu wazito wakiwemo aliyekuwa Spika wa Bunge na baadaye akawa Makamu Mwenyekiti wa CCM, Mheshimiwa Pius Msekwa ambaye alisema kwa jinsi mambo yalivyofanyika, Zanzibar inaonekana kama vile ni ‘invited guest’ (mgeni aliyealikwa) katika Muungano.[8] Naye msomi mashuhuri ulimwenguni, Prof. Ali Mazrui alisema baada ya Muungano Zanzibar imepoteza kila kitu muhimu wakati Tanganyika imebadilika jina tu na kuwa Tanzania huku ikiwa na mamlaka zaidi lakini ikibaki na Rais wake, nembo yake ya Taifa, wimbo wake wa Taifa na hata kiti chake katika Umoja wa Mataifa.[9]

 

 

MKATABA WA MUUNGANO HAUJAFUTA SERIKALI YA TANGANYIKA

 

Katika makubaliano ya kimataifa yaliyounda Muungano, ambayo hata hivyo katika muda wote wa uhai wa Muungano yamekuwa hayafuatwi, hakuna kifungu hata kimoja kilichotoa au kuagiza kwamba Serikali ya Tanganyika ifutwe kwa mujibu wa makubaliano hayo. Serikali ya Tanganyika, kama ilivyo ile ya Zanzibar, imelindwa na kifungu cha (v) kinachosomeka kwamba: “The existing laws of Tanganyika and of Zanzibar shall remain in force in their respective territories…”. Kinachosemwa hapa ni kwamba “Sheria zilizopo za Tanganyika na za Zanzibar zitaendelea kufanya kazi na kuwa na nguvu katika maeneo yao.”

 

Wataalamu wa katiba na sheria wanafahamu kwamba katiba ndio sheria mama ya sheria zote za nchi. Hivyo Katiba ya Tanganyika imelindwa na inapaswa kuwepo na Serikali yake iwepo, pamoja na viongozi wake kuwepo na kusimamia mambo yasiyo ya Muungano. Katiba na sheria za Tanganyika ndizo zilizotakiwa zitumike katika eneo la Tanganyika kwa yale mambo yaliyokuwa hayamo kwenye Muungano kama ambavyo Katiba (au kabla ya hapo Dikrii za Kikatiba – Constitutional Decrees) na sheria za Zanzibar zinavyotumika katika eneo la Zanzibar kwa yale mambo ambayo si ya Muungano. Hiyo ndio tafsiri ya ‘maeneo yao’.

 

Wazanzibari wanafahamu kwamba Katiba na Serikali ya Tanganyika vimefutwa kwa makusudi na Bunge la Tanganyika ili kujipa nafasi kuitumia Serikali ya Muungano, kama kwamba ndio Serikali ya Tanganyika. Lengo ni hatimaye kuiuwa Serikali ya Zanzibar na kufanya Tanganyika mpya ikiwa na jina jipya la Tanzania lenye mipaka mipya, yaani kuwa nchi moja yenye Serikali Moja.

 

Hiyo ndio ghilba iliyofanywa na viongozi wa Tanganyika mara baada ya kuwekwa saini makubaliano. Kwa kusaidia kufichuwa ukweli wa hadaa hii, ni vyema ikaangaliwa Sheria Na. 22 ya mwaka 1964 inayoitwa “Union of Tanganyika and Zanzibar Act, 1964.”

 

Sheria hii ilipitishwa na Bunge la Tanganyika Aprili 25, 1964, siku moja kabla Muungano kuanza kufanya kazi. Ilikusudiwa kuthibitisha kukubalika Muungano huo wa Tanganyika na Zanzibar upande wa Tanganyika (ratification). Kifungu cha (viii) cha Makubaliano ya Muungano kinaagiza ifanyike hivyo kwa pande zote mbili za Muungano.

 

Inasikitisha kusoma katika kifungu Na. 2 cha sheria hiyo kwamba:

 

“existing law” means the written and unwritten law as it exists immediately before Union Day … but does not include the Constitution of Tanganyika insofar as it provides for the Government of the Republic of Tanganyika or any declaration or law, or any provision thereof, which expires with effect from commencement of the Interim Constitution”.

 

(“Sheria iliyopo maana yake ni sheria iliyoandikwa na isiyoandikwa kama ilivyo kabla tu ya siku ya Muungano… lakini haijumuishi Katiba ya Tanganyika kwa mintaraf ya kuiweka kwake Serikali ya Jamhuri ya Tanganyika au tamko au sheria, au kifungu chochote ambacho kinafutika kwa kuanza kufanya kazi Katiba ya Muda (ya Muungano)).”

 

Kwa hivyo, wakati Bunge la Tanganyika linapitisha sheria ya kuridhia (ratify) kuwepo kwa Muungano kwa upande wa Tanganyika, sheria hiyo ilianza kupinga vifungu vya makubaliano hayo. Mfano mwengine ni kifungu Na. 7 cha sheria hiyo kinachosema:

 

“On the commencement of the Interim Constitution of the United Republic, the Constitution of Tanganyika shall cease to have effect for the government of Tanganyika as a separate part of the United Republic”.

 

(“Itapoanza kufanya kazi Katiba ya Muda ya Jamhuri ya Muungano, Katiba ya Tanganyika itasita kuwa na nguvu kwa ajili ya Serikali ya Tanganyika kama sehemu mbali ya Jamhuri ya Muungano.”)

 

Kwa maneno mengine, sheria ambazo zilitakiwa zitumike kwa Tanganyika kwa mambo ambayo si ya Muungano zilipewa maana mpya kwamba eti zisijumuishe Katiba ya Tanganyika.

 

Jambo moja lililo wazi, pamoja na hatua hii ya kuifuta Katiba ya Tanganyika, ni kwamba kule kuendelea kutambua kuwepo kwa sheria nyengine za Tanganyika bado kunamaanisha kuwepo kwa mamlaka ya Tanganyika ambako sheria hizo kwa mambo yote yasiyo mambo ya Muungano ziliendelea na zinaendelea kutumika hadi leo.

 

Zaidi, inapaswa ifahamike kwamba kufuta Katiba ya Tanganyika kulikofanywa na vifungu vya sheria hii hakukubadilisha makubaliano yaliyokwishatiwa saini kati ya Serikali mbili zilizounda Muungano, yaliyosema kwamba sheria za nchi mbili hizi zitaendelea kutumika katika maeneo yao. Bunge la Tanganyika, na hata hili la Muungano, halikuwa na mamlaka kutafsiri vifungu vya Mkataba wa Muungano ambao ni mkataba wa kimataifa.

 

Utaratibu wa kisheria ni kwamba kama Mkataba ulitakiwa kutafsiriwa basi walioandika rasimu ya mkataba huo ndio walipaswa kutoa tafsiri ya vifungu vyake, tafsiri ambayo ingepaswa iwe sehemu ya Mkataba huo. Na wala makubaliano yale hayakufuta wadhifa wa Rais wa Tanganyika. Si hivyo tu, bali pia Katiba ya Muungano ambayo ilitakiwa iwe ya muda tu kwa mwaka mmoja (interim) ilikuwa ni ile ya Tanganyika iliyofanyiwa marekebisho kwa ajili ya kutumika kwa Serikali ya Muungano.

 

Haikuruhusiwa kutumika kuiongoza Tanganyika kwa sababu Tanganyika ilikuwa na Katiba yake na Rais wake. Mwalimu Nyerere alikuwa na vyeo viwili, Rais wa Jamhuri ya Muungano kwa mujibu wa Makubaliano na Katiba ya Muungano na Rais wa Tanganyika kwa mujibu wa Katiba ya Tanganyika, kama alivyokuwa Mzee Karume ambaye alikuwa Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano kwa mujibu wa Makubaliano na Katiba ya Muungano na akaendelea kubaki kuwa Rais wa Zanzibar kwa mujibu wa Dikirii za Katiba ya Zanzibar (Constitutional Decrees).

 

Hivyo ndivyo makubaliano yalivyokuwa na ndivyo yalivyopaswa yawe hadi hii leo. Waliobadilika ni watu tu. Kufanya vyenginevyo ni kinyume na makubaliano yale na ndio sababu ya migogoro ya Muungano. Yaliyofanyika ni ujanja uliokuwa hauna nia njema kwa Zanzibar kama alivyosema Prof. Issa Shivji, mtaalamu wa Katiba wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam.

 

Hatua zote ya kuepusha Serikali ya Tanganyika kuwepo zilifanywa kwa makusudi kabisa, ili itumike Serikali ya Muungano kama ndio Tanganyika. Katika Sheria ile Na. 22 ya 1964, Rais wa Tanganyika amejipa madaraka ya kutunga na kutoa maagizo yanayohusu Muungano kwa kutumia amri (Decrees) za Sheria ya Tanganyika.

 

Siku ile ile ilipopitishwa Sheria Na. 22 ya 1964 zilipitishwa pia Decrees mbili zilizotokana na vifungu Na. 6 (3), cha 8 na cha 5 cha sheria hiyo Na. 22 ya 1964, yaani The Provisional Transitional Decree 1964, na ile ya Interim Constitution Decree 1964 ambazo zilifanya mabadiliko makubwa ya Muungano nje ya yale makubaliano yaliyokuwemo katika Mkataba wa Muungano. Sheria zile zote hazikuwa halali maana ni Decrees zilizopitishwa na Bunge la Tanganyika zilizotokana na Sheria Na. 22 ya 1964 ya Tanganyika kabla hata ya Muungano wenyewe kuanza kufanya kazi tarehe 26 Aprili, 1964.

 

Miongoni mwa mambo yaliyodhihirisha kuwa hakukuwa na nia njema katika Muungano huu tokea awali ni pale wafanyakazi wa Serikali ya Tanganyika wote walipopandishwa vyeo kwa pamoja na kuwa wafanyakazi wa Muungano kama kifungu cha 3 (1) cha Provisional Transitional Decree kinavyosema:

 

“Every person who holds office in the service of the Republic of Tanganyika immediately before the Union Day, shall on Union Day be deemed to have been elected, appointed or otherwise selected to the corresponding office in the service of the United Republic.”

 

Yaani kila mfanyakazi aliyekuwa wa Serikali ya Tanganyika mara kabla ya siku ya Muungano kufumba na kufumbuwa anakuwa mara moja mfanyakazi wa Serikali ya Muungano kuanzia siku ya Muungano. Huu tuuiteje kama si ujambazi wa kikatiba (constitutional banditry)?

 

Vivyo hivyo, kifungu cha 6 (i) cha Decree kinasema mara tu baada ya kuanza Muungano, Mahkama ya Tanganyika na Majaji wake wote nao watakuwa ndio Mahkama na Majaji wa Jamhuri ya Muungano kinyume na Makubaliano ya Muungano. Mpaka leo Katiba zote mbili hazitambuwi Mahkama (ukiondoa Mahkama ya Rufaa) kama ni suala la Muungano. Nembo ya Tanganyika inatumika kama nembo ya Serikali ya Muungano na Idara ya Mwanasheria Mkuu wa Tanganyika inachukuliwa kama Idara ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali ya Muungano.

 

Haya yote hayamo na ni kinyume na Makubaliano ya 1964. Yote haya na kile kifungu cha 7 cha Sheria Na. 22 ya 1964 kinachofuta kuwepo kwa Serikali ya Tanganyika hayakubadilisha na wala hayana mahusiano na Makubaliano ya Muungano ya 1964. Yote haya yalifanywa na Bunge la Tanganyika kwa maslahi ya Tanganyika nje ya Mkataba wa Muungano.

 

Aliyekuwa Spika wa Bunge na baadaye akawa Makamu Mwenyekiti wa CCM, Mheshimiwa Pius Msekwa, analifahamu vyema suala hili. Katika waraka wake alioutoa kwenye Semina kuhusu Muungano hapo Hoteli ya Mkonge, Tanga tarehe 25—27 Februari 1994 anasema:

 

“The Transitional Decree, 1964 published on 01/05/64, transferred persons who were holding office in the public service of the Republic of Tanganyika to the corresponding office in the public service of the United Republic of Tanzania. By the same decree the High Court of Tanganyika also became the High Court of United Republic of Tanzania and the public seal of Tanganyika became public seal of the United Republic.”

 

Athari za hatua hizi kwa Zanzibar ziko wazi. Tanganyika imejigeuza Tanzania na imechukua mamlaka ya mambo muhimu ya Zanzibar huku ikijipa hadhi ya kuwa juu ya Serikali ya Zanzibar kinyume na Mkataba wa Muungano.

 

Hii ndiyo siri ya viongozi wa Tanganyika wanaoongoza Serikali ya Jamhuri ya Muungano kung’ang’ania mfumo wa Serikali mbili na kukataa kata kata mabadiliko yoyote ya mfumo huo kwani Tanganyika inanufaika nao kwa kuwa yenyewe ndiyo imekuwa ‘Muungano’. Kukubali muundo wa Serikali tatu ni kuzifanya Tanganyika na Zanzibar ziwe na hadhi na fursa sawa katika Muungano, jambo ambalo Tanganyika hailitaki maana kulikubali ni kukubali kupoteza fursa zote inazozipata hivi sasa kwa kujikweza kwake na kujifanya kuwa ndiyo ‘Muungano’.

 

Ushahidi wa wazi wa hoja yangu hii ni kwamba mtu anapoangalia taasisi zote za Muungano zilizoundwa chini ya Katiba au sheria za Muungano ambazo zinazikutanisha Serikali mbili zilizopo sasa, ataona kuwa wajumbe wanaowakilisha upande wa Serikali ya Muungano wote ni kutoka Tanganyika. Hoja inayojitokeza ni kwamba Serikali ya Muungano ni ya shirika ambapo Zanzibar ni sehemu ya ushirika huo, kwa nini basi wajumbe wanaowakilisha Serikali hiyo ya Muungano watoke upande wa Tanganyika peke yake? Jawabu ni rahisi. Serikali ya Muungano kwa hakika ni Serikali ya Tanganyika iliyojivika joho la Muungano.

 

Rais Jakaya Kikwete amekaririwa hadharani akisema matatizo ya Muungano hayatokani na muundo bali yanasababishwa na viongozi. Hoja, maelezo na mifano niliyoitoa hapo juu inatosha kumuonyesha Rais kwamba kauli yake si sahihi. Vyote viwili – muundo na pia kukosekana kwa nia njema upande wa viongozi – ni sababu za kuwepo kwa matatizo yasiyokwisha ya Muungano.

 

 

UVUNJWAJI WA MKATABA WA MUUNGANO

 

Mbali na suala la muundo wa Muungano, maeneo mengine mengi yanayogusa msingi wa Mkataba wa Muungano yaliendelea kuvunjwa na Tanganyika ikivaa joho la Serikali ya Muungano.

 

Kifungu cha (iv) cha Mkataba wa Muungano kiliorodhesha mambo 11 tu ambayo ndiyo yaliyokubaliwa na Jamhuri ya Watu wa Zanzibar na Jamhuri ya Tanganyika kuwa mambo ya Muungano. Hata hivyo, kipindi cha miaka 49 ya Muungano kimeshuhudia mambo hayo yakiongezwa isivyo halali kwa kutumia chombo kisicho na mamlaka ya kufanya hivyo yaani Bunge la Muungano na sasa kufikia 22 lakini ukiyanyumbua yanafikia 37. Mfano unakuta kifungu kimoja cha 11 kinayaweka pamoja mambo manne ambayo ni Bandari, Usafiri wa Anga, Posta na Simu. Kwa lugha ya Mwanasheria Mkuu wa Zanzibar, Mhe. Othman Masoud Othman, anasema ni makontena 22 yenye mambo 37 ya Muungano. Ikumbukwe kwamba kila hatua ya kuongeza mambo ya Muungano maana yake ni kuchukua mamlaka ya Zanzibar na kuyahaulisha kwa Serikali ya Muungano ambayo kama tulivyokwisha onyesha kwa hakika hasa ni Serikali ya Tanganyika iliyojivika joho la Muungano.

 

Mambo hayo yaliyoongezwa juu ya Makubaliano ya Muungano ya asili, yaani, yale kumi na moja (11) ni haya, kama yanavyoelezwa katika Nyongeza ya Kwanza ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano:- 

 

(xii)      Mambo yote yanayohusika na Sarafu na Fedha kwa ajili ya malipo yote halali (pamoja na noti); mabenki; fedha za kigeni na usimamizi juu ya mambo yanayohusika na fedha za kigeni.

(xiii)   Leseni za Viwanda na Takwimu.

(xiv)    Elimu ya Juu.

(xv)       Maliasili ya Mafuta, pamoja na mafuta yasiyochujwa ya motokaa na mafuta aina ya petroli na aina nyinginezo za mafuta au bidhaa za mafuta, na gesi asilia.

(xvi)    Baraza la Taifa la Mitihani Tanzania na mambo yanayohusika na kazi za Baraza hilo.

(xvii) Usafiri na Usafirishaji wa Anga.

(xviii)                                                                                                                                                                    Utafiti.

(xix)    Utabiri wa Hali ya Hewa.

(xx)       Takwimu.

(xxi)    Mahkama ya Rufaa ya Jamhuri ya Muungano.

(xxii) Uandikishaji wa vyama vya siasa na mambo mengine yanayohusiana nayo.

 

Ukiondoa mambo hayo, yapo pia mambo mengine ya ziada ambayo yameingizwa katika Muungano kwa Bunge tu kutunga sheria na kutangaza kwamba zitatumika hadi Zanzibar. Mfano wa masuala kama hayo ni Uvuvi wa Bahari Kuu na Tume ya Utawala Bora na Haki za Bianadamu. Yapo baadhi yake kwa mfano Usafiri wa Baharini ambapo Zanzibar ilikataa kutekeleza sheria iliyopitishwa na Bunge (The Merchant Shipping Act) na hatimaye ikatunga sheria yake yenyewe kuhusiana na suala hilo (The Maritime Transport Act).

 

Kifungu cha (vii) cha Mkataba huo kinataka Rais wa Jamhuri ya Muungano kwa mashauriano na makubaliano na Makamu wa Rais ambaye pia ni Rais wa Zanzibar kuunda Tume ya Katiba kwa lengo la kutayarisha rasimu ya Katiba ya Kudumu ya Muungano na baadaye kuifikisha rasimu hiyo mbele ya Bunge la Katiba (Constituent Assembly) litakalokuwa na wajumbe kwa idadi watakayokubaliana kutoka Zanzibar na Tanganyika. Hatua hii muhimu sana kikatiba ilitakiwa itekelezwe ndani ya kipindi cha mwaka mmoja tokea tarehe ya Muungano. Hadi ilipokuja hatua hii ya sasa ya kuunda Tume ya Mabadiliko ya Katiba, hakuna Tume ya Katiba iliyoundwa wala Bunge la Katiba lililoundwa na kuitishwa kwa madhumuni ya kupitisha Katiba ya Kudumu ya Muungano. Kilichofanyika ni kuwa mwezi mmoja kabla ya kumalizika mwaka mmoja uliotakiwa, Bunge la Muungano lilitakiwa na Mwalimu Julius Nyerere kupitisha sheria ya kuahirisha kwa muda usiojulikana tarehe ya kutekelezwa kwa hatua hii.

 

Lakini mbali na dhoruba hizo dhidi ya Mkataba wa Muungano, rungu kubwa zaidi ambalo ndilo lililotumika kuimaliza Zanzibar lilikuwa ni kule kuunganishwa kwa vyama vya TANU na ASP na kuzaliwa CCM huku chama hicho kipya kikijipa madaraka juu ya vyombo vyengine vyote vya maamuzi katika nchi ikiwemo Serikali na Bunge na Baraza la Wawakilishi. Chini ya dhana ya Chama kushika hatamu (Party Supremacy) iliyoasisiwa na Mwalimu Nyerere kwa lengo la kujilimbikizia madaraka yeye na Chama alichokuwa akikiongoza kama milki yake binafsi, CCM iliweza kutoa maagizo na maamuru mazito bila ya kujali madaraka ya Serikali ya Zanzibar yaliyotolewa kupitia Mkataba wa Muungano na hivyo kujinyakulia uwezo wote wa kuitawala Zanzibar ipendavyo huku viongozi wa Zanzibar wanaohoji wakituhumiwa kwamba wanapinga nidhamu ya Chama.

 

 

MATATIZO YATOKANAYO NA KIINI CHA TATIZO

 

Kiini cha tatizo la msingi la Muungano ambalo kwa mtazamo wangu ni muundo wake unaotokana na tafsiri potofu ya Mkataba wa Muungano (Articles of Union) ndicho kimepelekea kujitokeza kwa matatizo mengine katika miaka 49 hii na ambayo yanaongezeka kila uchao.

 

Mtu anapoangalia matatizo au hizi zinazoitwa kero atagundua kuwa karibu yote yanatokana ama na mshirika mmoja (mara nyingi Zanzibar) kutokuuamini au kuutilia shaka upande mwengine, au mshirika wa pili (mara nyingi Tanganyika ikivaa joho la Muungano) kuamini kwamba ina haki ya moja kwa moja kuamua na kutekeleza mambo fulani bila ya kulazimika kupata ridhaa ya upande wa pili ambao inahisi kama imeubeba tu. Ukiangalia kwa undani utagundua kuwa tatizo linarudi kwenye muundo. Zanzibar haifahamu mamlaka ya Muungano katika Serikali ya Muungano yanaishia wapi ambapo mamlaka kwa mambo yasiyo ya Muungano kwa ajili ya Tanganyika yanaanza. Tanganyika nayo kwa kuwemo kwake katika Serikali ya Muungano kunaifanya ishindwe kufahamu ni vipi na wapi Zanzibar inapata mamlaka ya kuhoji mambo ambayo yameshatamkwa kwamba ni ya Muungano hata kama hayakuwemo katika Mkataba wa asili wa Muungano.  Hali hii inaonekana katika kila kile kinachoitwa “kero” za Muungano.

 

Mifano inaweza kutolewa kwa takriban mambo yote, lakini kwa madhumuni ya waraka huu tuchukue mifano ya mambo matatu yafuatayo yanayozusha malalamiko:

 

1.     Umilikaji wa Mafuta na Gesi asilia.

 

2.   Uchangiaji katika gharama za Muungano na mgawanyo wa mapato yanayotokana na Muungano.

 

3.   Uwakilishi wa Zanzibar katika Bunge la Muungano.

 

 

Umilikaji wa Mafuta na Gesi asilia

 

Kwanza, kuingizwa kwake katika orodha ya mambo ya Muungano (kama ilivyo kwa mambo mengi yaliyoongezwa baadaye) hakukufuata taratibu za Serikali ya Muungano (ambayo pia ni Serikali ya Tanganyika kwa mambo yasiyo ya Muungano) kuishauri na kupata ridhaa ya Zanzibar. Pili, Zanzibar inataka kujua ikiwa mafuta yanapaswa kuwa suala la Muungano na hivyo mapato yatakayopatikana yanufaishe pande zote mbili, kwa nini madini mengine yanayopatikana Bara kama vile dhahabu, almasi au tanzanite hayakufanywa pia kuwa ya Muungano na hivyo kunufaisha pande mbili pia? Kwa hivi sasa, ambapo si mambo ya Muungano, mapato yake yanaponufaisha Tanganyika peke yake, yanaingia katika mfuko (account) upi wa matumizi? Tatu, kwa miaka isiyopungua tisa (9) sasa, Tanganyika imekuwa ikivuna gesi asilia huko Songosongo na Mnazi Bay na kwa miaka miwili sasa imekuwa ikivuna gesi asilia kwa wingi katika maeneo ya bahari iliyopakana na Mtwara lakini pamoja na kutajwa suala hilo kuwa la Muungano, Zanzibar haijafaidika na chochote kutokana na mapato yake. Nne, ikiwa mapato yatakayopatikana kutokana na mafuta na gesi asilia yataingia katika mfuko wa Muungano, kuna uhakika gani wa kutumika kwa shughuli za Muungano tu wakati hakuna mifuko tofauti ya fedha kwa shughuli za Muungano na zile za Tanganyika zisizo za Muungano?

 

Uchangiaji katika gharama za Muungano na mgawanyo wa mapato yanayotokana na Muungano

 

Je, mtu anaposema Zanzibar haichangii gharama za uendeshaji wa vyombo na taasisi za Muungano kwa sababu tu Serikali ya Zanzibar haitoi fungu la fedha na kuliingiza katika Serikali ya Muungano, Tanganyika ambayo hata Serikali haina inachangia vipi na kiasi gani? Ikiwa mchango wake unatolewa na Serikali ya Muungano, kwani hii siyo serikali ya shirika ambapo Zanzibar ni mbia? Vipi basi Zanzibar itakiwe ichangie mara mbili kwa kutumia hadhi mbili tofauti? Na ikichangia (iwapo itachangia), ina uhakika upi kwamba itakachotoa hakitatumiwa na Serikali ya Muungano kwa shughuli za Tanganyika zisizo za Muungano ikitumia mamlaka yake kwa madhumuni hayo? Vivyo hivyo kwa mapato yatokanayo na vyombo na taasisi za Muungano, tunajua Zanzibar inapata mgao wake na kiasi chake kimewekwa wazi (ingawa kwa sasa ni mapato ya TRA yanayokusanywa Zanzibar; na pia gawio kutoka Benki Kuu (BOT) ambalo nalo kiwango chake hakikubaliki kwa Wazanzibari). Zipo mamlaka nyengine za Kimuungano zinazoingiza mapato na ambazo Zanzibar haipewi chochote kutoka kwake zikiwemo TCRA, TCAA, TPC, TTCL, na TPDC kwa kutaja chache. Masuala zaidi yanakuja: Yale mapato yanayobaki katika Serikali ya Muungano, kuna kipi cha kuonyesha mpaka wa matumizi yake kwa Muungano na kwa shughuli za Tanganyika zisizo za Muungano? Uadilifu na uwajibikaji wa matumizi yatokanayo na mgao huu wa mapato utaonekana vipi?

 

Ukweli hasa kuhusiana na suala la uchangiaji katika gharama za Muungano na mgawanyo wa mapato yanayotokana na Muungano ulipatikana kufuatia kuundwa kwa Tume ya Pamoja ya Fedha (Joint Finance Commission) ambayo iliajiri wataalamu (consultants) kutoka taasisi inayoheshimika duniani ya PriceWaterhouseCoopers kuangalia suala hilo. Ripoti ya Wataalamu ilitolewa Agosti 2006 na kufanyiwa kazi na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar lakini hadi leo imekaliwa na Serikali ya Muungano bila shaka baada ya kutoa picha isiyopendeza kwa upande wa Tanganyika kuhusiana na hali halisi ya vipi uendeshaji wa Muungano ulivyo. Wataalamu wa Kampuni ya PriceWaterhouseCoopers walifanya uchambuzi halisi wa mambo yepi ni ya Muungano na yepi ni ya Tanganyika na yepi ni ya Zanzibar na gharama za uendeshaji wa kila moja. Baada ya orodha kupatikana, watafiti wakatafuta matumizi halisi ya bajeti ya vifungu hivyo kwa muda wa kiasi cha miaka 10 iliyopita. Watafiti hao walikwenda mbali zaidi ya hapo na kukusanya mapato yote kwa kila kifungu cha mambo ya Muungano halisi. Mwishowe, wakalinganisha iwapo mapato yanakidhi matumizi au yana nakisi (upungufu)?

 

Kilichojitokeza ni kwamba kwa mwaka wa fedha 2003/2004 pekee,  matumizi halisi kwa vifungu vya Muungano yalikuwa Shs. 537,258.4 bilioni ambayo ni aslimia 20 tu ya bajeti yote ya Serikali ya Muungano kwa mwaka huo. Mapato halisi ya vyanzo vya mapato vinavyotokana na mambo ya Muungano kwa mwaka huo yalikuwa ni Shs. 1,030,826.1 bilioni. Tofauti ya vifungu hivyo vimetoa ziada ya ya Shs. 493,567.7 bilioni kwa mwaka huo. Ziada hii haiingizi mapato yanayotokana na misaada kutoka nje au mikopo. Ziada hii hutumika kwa shughuli za Tanganyika zisizo za Muungano.

 

Ukweli huu unaonyesha hata kama kungekuwa na Serikali tatu kusingekuwa na haja yoyote kwa Serikali ya Zanzibar na ile ya Tanganyika kulipia fedha za ziada kama wahusika watatunza na kuweka kumbukumbu sahihi za mapato na matumizi ya mambo ya Muungano halisi badala ya yale ya Tanganyika kuchanganywa na ya Muungano.  Mambo yasiyokuwa ya Muungano ya Tanganyika yalipotengwa nje ya yale ya Muungano, gharama za mambo ya Muungano zimejidhihirisha wazi bila ya kujificha na kuonesha kwamba zinaweza kulipiwa kupitia mapato ya mambo ya Muungano pekee na ziada kubaki. Lakini hili limekuwa rahisi kwa kukubali ukweli kwamba kuna mafungu matatu ya mapato na matumizi katika Serikali zetu mbili. Mafungu hayo ni la SMZ kwa mambo yake yasiyo mambo ya Muungano, la Serikali ya Muungano kwa mambo ya Muungano, na la Serikali ya Muungano inayofanya kazi za Tanganyika kwa mambo yasiyokuwa ya Muungano.

 

Uwakilishi wa Zanzibar katika Bunge la Muungano

 

Wananchi wengi wa Tanganyika wanahoji vipi Zanzibar iliyo ndogo na ambayo ina watu milioni 1.3 inawakilishwa na wabunge wa kuchaguliwa 50 wakati Dar es Salaam yenye wananchi wengi zaidi ina wabunge wa kuchaguliwa 7 tu? Wabunge hawa wanashiriki mijadala yote ya Bunge ikiwemo ya mambo yasiyo ya Muungano (ambayo kwa usahihi yatakuwa ni mamlaka ya Tanganyika kwa mambo yasiyo ya Muungano yanayosimamiwa na Serikali ya Muungano). Wanapata wapi uhalali wa kufanya hivyo wakati Wazanzibari hawapangiwi shughuli hizo (kwa mfano elimu, afya, kilimo, maji, umeme, habari, michezo, biashara, viwanda, serikali za mitaa n.k.) na Serikali ya Muungano wala hawasimamiwi katika mambo hayo na Bunge la Muungano? Uko wapi mpaka wa mamlaka ya Wazanzibari katika ushiriki wa Bunge hilo wakati wao wana Serikali yao inayopanga na Baraza la Wawakilishi lao linalosimamia mambo yao kama hayo yasiyo ya Muungano?

 

Mifano hii inatosha kuonyesha kwamba takriban matatizo yote, kama si yote, yanatokana na mkanganyiko na mgongano wa maslahi kati ya pande mbili ambao nao unasababishwa na mfumo usio wazi kuhusiana na mgawanyo wa madaraka kati ya mamlaka tatu za Muungano zinazotambuliwa katika Mkataba wa Muungano.

 

NAFASI YA ZANZIBAR KATIKA MUUNGANO


 

Baada ya kuangalia kiini cha matatizo ya Muungano kinachotokana na muundo wa Muungano, sasa tuangalie nafasi ya Zanzibar katika Muungano huu, hasa kufuatia kauli za kuidhalilisha Zanzibar zilizotolewa na wanasiasa wa Tanganyika hivi karibuni wakiongozwa na Waziri Mkuu Mizengo Pinda.

 

Kutokana na kule kule kujaribu kujisahaulisha kuwepo kwa Mkataba wa Muungano ambao ndio sheria kuu (grundnorm) ya Muungano na kuifanya Katiba inayoitwa ya Jamhuri ya Muungano ionekane kuwa ndiyo Katiba mama na hivyo kuikweza kwamba eti iko juu ya Katiba ya Zanzibar, zimetolewa kauli kwamba kufuatia hatua ya kuungana na Tanganyika, Zanzibar imepoteza hadhi na sifa ya kuwa nchi.

 

Waliosema hivi wanasahau kwamba Zanzibar ina Katiba yake ambayo ina hadhi sawa na Katiba ya Jamhuri ya Muungano, na kwamba zote mbili zinapaswa kutafsiri kisawa sawa Makubaliano ya Muungano.

 

Katiba ya Zanzibar inatamka wazi wazi kwamba Zanzibar ni nchi. Utangulizi (Preamble) wa Katiba hiyo ambao unaeleza dhamira ya Wazanzibari wakiwa ndiyo wenye Katiba hiyo (sponsors of the Constitution) unabainisha wazi wazi dhamira ya Wazanzibari kulinda na kudumisha nchi yao na yale yote yanayoitambulisha Zanzibar kama nchi. Sehemu ya Utangulizi huo inasomeka:

 

"NA KWA KUWA tunazingatia na kuthamini kazi nzuri ya Kimapinduzi iliyofanywa na Viongozi wa Mapinduzi, wakiongozwa na Mwasisi wa Chama cha ASP na Mapinduzi ya Zanzibar ya 1964, Marehemu Mzee Abeid Amani Karume, ambaye fikra zake zitaendelezwa na kudumishwa daima, kizazi baada ya kizazi katika kupambana na Ukoloni, Ubepari Unyonge, Uonevu na Dharau, na badala yake kudumisha Uhuru na Umoja, Haki na Usawa, Heshima na Utu;"

 

Huko nyuma kabla ya Marekebisho ya Kumi ya Katiba ya Zanzibar ya 1984 yaliyopitishwa mwaka 2010, ni bahati mbaya kwamba baadhi ya watu walikuwa wakinukuu vibaya kifungu cha (1) cha Katiba ya Zanzibar kilichokuwa kikisomeka kwamba, “Zanzibar ni sehemu ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania” kumaanisha kwamba kwa kuwa kwake sehemu ya Jamhuri ya Muungano kunaiondolea na kuipotezea Zanzibar hadhi yake ya kubakia kuwa nchi. Tafsiri hiyo haikuwa sahihi kama ilivyofafanuliwa na Jaji Abdullahi D. Zuru kutoka Nigeria, ambaye alikuwa Mwenyekiti wa Tume ya Kupitia Sheria (Law Review Commission) Zanzibar.

 

Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar ilimuagiza Jaji Zuru kuipitia Katiba ya Zanzibar na kupendekeza marekebisho ikibidi. Jaji Zuru alisema katika ripoti yake kuhusu kifungu cha (1) cha Sura ya Kwanza, Sehemu ya Kwanza ya Katiba ya Zanzibar kuwa:

 

"Mtu akisoma kwa makini Utangulizi (Preamble) na Katiba yote kwa jumla, ataelewa kwamba Zanzibar ni dola yenye mamlaka yake kamili (sovereign state) na kwamba wale waliotunga Katiba hii hawakuwa na nia ya kusalimisha na kuachia mamlaka (sovereignty) ya Zanzibar wakati wa kuundwa Muungano baina ya Tanganyika na Zanzibar, ambao ulizaa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Hata hivyo, mtu akisoma maelezo ya kifungu cha (1) cha Katiba anapigwa na butwaa na kushangaa kwa nini kifungu hicho cha kwanza kwa kinyemela (surreptiously) kimesalimisha au kimepuuza mamlaka hayo."

 

Jaji Zuru anaendelea kusema kuwa anaamini kwamba waanzilishi wa hatua ya kuzileta pamoja Zanzibar na Tanganyika kuwa Jamhuri moja, hawajakusudia kuwa hatua hiyo ipoteze (erode) uhuru wa nchi yoyote kati ya nchi mbili kamili zilizohusika.

 

Kinyume na hayo, maoni yake ni kwamba nia ilikuwa kuimarisha uhuru wa  kila moja ya nchi hizo mbili sambamba na ule wa Muungano utakaozaliwa. Mtaalamu huyo anafahamisha kwamba kisheria, "Haki mbili zikikutana ndani ya mtu mmoja, ni sawa na kusema kwamba ziko ndani ya watu wawili."

 

Labda niinukuu kwa Kiingereza, kama alivyoandika mwenyewe, kwa kufahamika zaidi: "It is a trite law that when two rights meet in one person, it is the same as if that were in two persons."

 

Anaendelea kusema kwamba ni imani ya Tume yake kabisa kuwa ulipoundwa Muungano, Zanzibar ilikusudia na ilisisitiza juu ya kuendeleza mamlaka yake ndani ya utaratibu wa Muungano. Anafafanua:

 

"Kutokana na haya, tunaamini kwamba hadhi ya Zanzibar kama inavyoelezwa katika kifungu cha (1) imepotoshwa kwa sababu (kifungu) hakielezi nia ya wenye katiba (sponsors of this constitution) na madaraka yaliyotolewa na watu wa Zanzibar..."

 

Labda turudi nyuma kidogo tufahamishe kuwa Tume ya Jaji Zuru imeeleza mwanzoni kuwa madaraka waliyo nayo Baraza la Wawakilishi, ambalo ndilo lililotunga Katiba hiyo mwaka 1984, yanatokana na wananchi na kwamba Baraza linayashikilia madaraka hayo kama amana (trust) kwa niaba ya wananchi hao. "Kwa hiyo, kushindwa kwa Serikali kusimamia misingi ya katiba ni sawa na kwenda kinyume na amana waliyokabidhiwa na watu wa Zanzibar.”

 

Haya yanaelezwa wazi katika kifungu cha 9 cha Katiba ya Zanzibar kinachosema,

 

"9.-(1) Zanzibar itakuwa ni nchi ya kidemokrasia na haki za kijamii.

      (2) Kwa hiyo hapa inaelezwa rasmi kwamba:-

(a) Mamlaka ya kuendesha nchi ni ya wananchi wenyewe ambapo nguvu na uwezo wote wa Serikali kufuatana na Katiba utatoka kwa wananchi wenyewe."

 

Tukiendelea na hoja, Jaji Zuru anasema maelezo ya kifungu cha (1) cha Katiba kabla ya kurekebishwa, ambacho ndicho kama mlango wa kuingilia kwenye Katiba yenyewe, yanampa msomaji wa nje sura ya kwamba Zanzibar si nchi yenye mamlaka yake wenyewe. "Kwa hiyo, tunachukulia maelezo haya kama ni kwenda kinyume na nia ya watu wa Zanzibar ambayo iko wazi na bayana katika Utangulizi (Preamble) na sehemu nyengine zinazohusika katika Katiba."

 

Kutokana na haya Tume ya Kurekebisha Sheria ikapendekeza kifungu hiki kiandikwe upya ili kuwakilisha nia ya watu wa Zanzibar. Jaji Zuru alipendekeza kisomeke kama ifuatavyo:

 

"Zanzibar ni, na itabaki dola yenye mamlaka, na itakuwa ni sehemu ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa mujibu wa matakwa na masharti yaliyotajwa katika Mkataba wa Muungano baina ya Dola ya Zanzibar na Jamhuri ya Tanganyika.”

 

Kwa madhumuni ya uelewa zaidi tutanukuu tena kwa Kiingereza kama alivyoandika mwenyewe Jaji Zuru:

 

"Zanzibar is and shall remain a sovereign state, and shall exist as an integral part of the United Republic of Tanzania, in accordance with the terms and conditions stipulated in the Articles of Union between the State of Zanzibar and the Republic of Tanganyika.”

 

Mapendekezo ya Tume ya Jaji Zuru yalipelekwa kwa Mwanasheria Mkuu wa Zanzibar Disemba 19, 2001, lakini kwa muda mrefu yakawa hayakufanyiwa kazi na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar mpaka pale hatimaye mwaka 2010 ilipoyafikisha mbele ya Baraza la Wawakilishi ili kurekebisha mapungufu ya kiuandishi ya Katiba ya Zanzibar na kutafsiri kisawasawa dhamira ya wananchi wa Zanzibar. Vifungu vilivyorekebishwa vya 1 na 2 sasa vinasomeka kama ifuatavyo:

 

“1. - Zanzibar ni miongoni mwa nchi mbili zilizounda Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.

2. - Zanzibar ni Nchi ambayo mipaka yake ni eneo lote la Visiwa vya Unguja na Pemba pamoja na visiwa vidogo vilivyoizunguuka bahari yake ambayo kabla ya Muungano wa Tanganyika na Zanzibar ikiitwa Jamuhuri ya Watu wa Zanzibar.”

 

Tukiachana na mapendekezo hayo, tuangalie Sura ya Kumi na Tatu ya Katiba ya Zanzibar. Kifungu cha 132 (1) kinachosema:

 

"132. - (1) Hakuna sheria yoyote itakayopitishwa na Bunge la Muungano ambayo itatumika Zanzibar mpaka sheria hiyo iwe ni kwa ajili ya mambo ya Muungano tu na ipitishwe kulingana na maelezo yaliyo chini ya vifungu vya Katiba ya Jamhuri ya Muungano.

 (2) Sheria kama hiyo lazima ipelekwe mbele ya Baraza la Wawakilishi na Waziri anayehusika.

 (3) Pale sheria ndogo inapoundwa kwa mujibu wa uwezo uliowekwa chini ya vifungu vya (1) na (2) sheria hii itatumika tu pale itapotimiza shuruti zote zilizowekwa kwa matumizi ya Sheria mama kama ilivyoamrishwa katika kifungu hiki."

 

Hapa kuna mambo mawili yanajitokeza. Kwanza kati ya mambo yote ya Muuungano, zaidi ya yale kumi na moja ya asili, yaliyoongezwa katika orodha ya mambo ya muungano (xii –xxiii) ni moja tu, kuhusu uandikishwaji wa vyama vya siasa, ambapo mswada ulipelekwa Baraza la Wawakilishi, ukajadiliwa na kupitishwa. Hivi karibuni sharti hili lilitekelezwa kuhusiana na Sheria ya Mabadiliko ya Katiba (Sura ya 83).

 

Mambo mengine yote sheria zake hazikuwahi kufikishwa mbele ya Baraza la Wawakilishi.

 

Kifungu kinachofuata yaani 133 (1) kinasema:

 

"133.-(1) Hakuna kodi ya aina yoyote itakayotozwa isipokuwa kwa mujibu wa sheria iliyotungwa na Baraza la Wawakilishi au kwa utaratibu uliowekwa kisheria na uliotiliwa nguvu ya kisheria iliyotungwa na Baraza la Wawakilishi.

 (2) Masharti yaliyomo katika kijifungu hiki hayatalizuwia Bunge kutumia mamlaka ya kutoza kodi ya aina yoyote inayohusiana na mambo ya Muungano kwa mujibu wa madaraka ya Bunge hilo, kwa kujuwa kwamba mashauriano baina ya Serikali ya Mapinduzi Zanzibar na Serikali ya Jamhuri ya Muungano yamefanywa na kukubalika sehemu zote mbili kabla kupitishwa sheria." 

 

Si jambo la siri kwamba kulikuwa na mvutano mkubwa kati ya Serikali ya Awamu ya Tano ya Dk. Salmin Amour na Serikali ya Jamhuri ya Muungano kuhusiana na Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) na suala zima la uoanishaji wa viwango vya ushuru na kodi (harmonisation of tariffs). Hadi leo wananchi wa Zanzibar wanaiona TRA kama ndiye adui mkubwa wa uchumi wao, iliyoua biashara visiwani na kuwatia Wazanzibari katika ufukara usiosemeka.

 

Ni wazi basi kwamba uundwaji wa TRA haujatimiza masharti ya kifungu cha 133 (2) cha Katiba ya Zanzibar kwa maana ya kuwepo na mashauriano baina ya Serikali ya Mapinduzi Zanzibar na Serikali ya Jamhuri ya Muungano na kukubalika sehemu zote mbili kabla kupitishwa sheria.

 

Inawezekana kukazuka hoja kwamba pale Katiba ya  Zanzibar inapopingana na Katiba ya Muungano ni ile ya Muungano ndio yenye nguvu. Ndiyo! Hii ni kuhusu vifungu vinavyowiana na Mkataba wa Muungano kama yalivyokuwa yamekubaliwa na Jamhuri ya Watu wa Zanzibar na Jamhuri ya Tanganyika hapo mwaka 1964. Vyengine vyote ni batili na hapo moja kwa moja Katiba ya Zanzibar ndiyo itakayosimama.

 

Kwa msingi wa hoja hizi, ni ukweli usio na ubishi kwamba Zanzibar imeendelea kubaki na hadhi yake kama nchi hata baada ya kuingia katika Muungano na Tanganyika na ndiyo maana Katiba yake, pamoja na mapungufu madogo madogo, bado imelinda kwa nguvu zote hadhi hiyo.

 

Naelewa kwamba kuna watu wanatumia uamuzi wa Mahkama ya Rufaa ya Jamhuri ya Muungano katika kesi maarufu ya Machano Khamis Ali na wenzake 18 dhidi ya SMZ uliotamka kwamba Zanzibar si nchi na kwamba kosa la uhaini haliwezi kutendeka Zanzibar kuwa ni msingi wa hoja kwamba vifungu nilivyovitaja vya Katiba ya Zanzibar vinakuwa havina maana yoyote pale vinaposititiza hadhi ya Zanzibar kama nchi.

 

Ni muhimu kueleweka kwamba uamuzi huu wa Mahkama ya Rufaa umejaa utatanishi. Kwanza, ulitolewa wakati Serikali ikiwa tayari imeondosha mashtaka dhidi ya watuhumiwa na kuwaachia huru. Kwa msingi huo, mtu anajiuliza uamuzi huo wa Mahkama ya Rufaa wakati unatolewa ulikuwa na uhalali upi kisheria na ulikuwa unahusu kesi ipi wakati kesi ilishaondolewa na Jamhuri mbele ya Mahkama. Lakini pili, mtaalamu wa masuala ya katiba anayeongoza hapa Tanzania, Prof. Issa Shivji amefanya mapitio ya uamuzi huo na kubainisha makosa mengi sana ya kisheria yaliyomo. Kubwa katika makosa hayo ni kule Majaji wanaohusika kudharau na kutoitumia kabisa Katiba ya Zanzibar katika kufikia uamuzi wao. Katika hitimisho lake, Prof. Shivji anasema:

 

The conclusion from this quick examination of the Zanzibar Constitution is that Zanzibar is a sovereign and a state, albeit its sovereignty is limited and the jurisdiction of the Executive and the Legislature is limited to non-Union matters in Zanzibar while its Judiciary, as epitomised by the High Court, has unlimited jurisdiction. A Mzanzibari owes allegiance to the State of Zanzibar and therefore an offence of treason can be committed against the state of Zanzibar. This is irrespective of the fact that treason may be stipulated as an offence in the union law; nevertheless it can be tried in the courts of Zanzibar.” [10]

 

“Hitimisho la upembuzi huu wa haraka wa Katiba ya Zanzibar ni kwamba Zanzibar ni dola na ni nchi, ijapokuwa nguvu yake ya kidola ina mipaka na uwezo wa Mamlaka ya Utawala na Mamlaka ya Kutunga Sheria umewekewa mipaka kwa mambo yasiyo ya Muungano ndani ya Zanzibar wakati Mamlaka ya Utoaji Haki, ikiwa inaongozwa na Mahkama Kuu, ina uwezo kamili usio na mipaka. Mzanzibari ana utii kwa Dola ya Zanzibar na hivyo kosa la uhaini linaweza kutendeka dhidi ya Dola ya Zanzibar. Hii ni bila ya kujali kwamba uhaini unaweza kuainishwa kuwa ni kosa kupitia sheria ya Muungano; lakini bado kosa hilo linaweza kuhukumiwa katika Mahkama za Zanzibar.”

         

 

 

VIPI TUTOKE HAPA TULIPO?

 

Inakaribia miaka 49 sasa tangu uundwe Muungano wa Tanganyika na Zanzibar. Kulikuwa na wakati wa kutosha kurekebisha kasoro zilizopo. Hilo halikuwezekana kutokana na ubabe wa Mwalimu Nyerere ambaye aliamua kuwatia shemere Wazanzibari na kuhakikisha Muungano unakwenda kama alivyotaka yeye hata baada ya “kuondoka madarakani”.

 

Si jambo la kuficha kwamba wananchi wa pande zote mbili za Muungano wamechoshwa na unafiki uliopo na wanadai mfumo na muundo mpya wa Muungano utakaoweka misingi mipya ya ushirikiano.

 

Katika mijadala mbali mbali inayoendelea katika ukusanyaji wa maoni ya wananchi, vyama vya siasa na taasisi nyengine za kijamii kumetolewa hoja kwamba suluhisho la matatizo niliyoyafafanua hapo juu na mengine mengi yanayoukabili Muungano huu, kumejitokeza mapendekezo yanayoelekeza kwamba ufumbuzi wake ni muundo wa Serikali Moja, Serikali Mbili zilizopo sasa pamoja na marekebisho kadhaa au Serikali Tatu. Kwa upande wa Zanzibar, wananchi walio wengi wamependekeza kuwepo kwa Muungano wa Mkataba (Treaty based Union) kama njia bora ya kudumisha mahusiano makongwe kati ya Zanzibar na Tanganyika.

 

Kwa upande wangu, siamini kama Serikali Moja, Mbili au Tatu zitaweza kumaliza matatizo yaliyopo ya Muungano na hasa kule kutokuaminiana kukubwa kulikojengeka kutokana na matatizo hayo kuachwa muda mrefu bila ya kushughulikiwa au kushughulikiwa kwa njia za hotuba za kisiasa  zaidi zisizofuatiwa na utekelezaji wowote. Sababu zangu za kutoiona mifumo hiyo kama njia sahihi ya ufumbuzi wa matatizo yanayotukabili ni hizi zifuatazo:

 

Serikali Moja:

 

Mfumo wa Serikali moja umekuwa ukitajwa kuwa utaondoa manung’uniko na kelele zote kuhusu matatizo ya Muungano lakini bado unaonekana kuwa na matatizo yafuatayo:

 

                                                            i.            Mfumo huu utazifuta kabisa nchi za Tanganyika na Zanzibar na kuwa na nchi moja yenye mamlaka moja inayosimamiwa na Serikali moja.

 

                                                         ii.            Ingawa mfumo huu unaweza kuungwa mkono na Watanganyika walio wengi, Wazanzibari hawawezi kuukubali kabisa mfumo huu kwa sababu utafuta utambulisho wao na historia yao.

 

                                                      iii.            Katika mfumo huu wa kuwa na nchi moja yenye mamlaka moja, Zanzibar itachukuliwa kama eneo jengine lolote la Tanzania na hivyo kutokuwa na uwezo wa kujiletea maendeleo yake na badala yake itategemea maendeleo yatakayopangwa na Serikali kuu kulingana na rasilimali zitakazotengwa kwa ajili ya eneo la Zanzibar kama inavyopangwa kwa maeneo mengine.

 

 

Serikali Mbili:

 

Mfumo wa serikali mbili uliopo hivi sasa una mkanganyiko wa mambo kadhaa kwa mfano:

 

(a)             Kutokuwepo kwa mshirika mmoja wa asili wa Muungano yaani Tanganyika. Hivyo linapotokea tatizo la Muungano badala ya kukutana pande mbili za Muungano na kujadiliana kwa misingi ya usawa sasa majadiliano yanakuwa baina ya Serikali ya Muungano na Serikali ya Zanzibar. Majadiliano ya namna hii yanakosa misingi ya haki na usawa.

 

(b)            Mabadiliko ya Katiba yaliyomuondoa Rais wa Zanzibar kuwa Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano yalikwenda kinyume kabisa na makubaliano ya awali ya Muungano. Mabadiliko haya yanamuondoa mmoja wa washirika wakuu katika Serikali ya Muungano. Mkataba wa Muungano, ibara ya (iii) (b) ulitamka bayana kwamba Rais wa Zanzibar atakuwa ndiye msaidizi mkuu wa Rais wa Muungano. Jee hivi sasa nani msaidizi mkuu? Makamu wa Rais kwa mfumo wa sasa kwa mfano anatoka Zanzibar sio kiongozi mwenye dhamana ya kiutendaji Zanzibar na hivyo hawezi kuwakilisha matakwa ya Zanzibar katika Muungano.

 

(c)             Kumekuwa na mkanganyiko vile vile kwa mambo ya Zanzibar ambayo siyo ya Muungano lakini mambo hayo yanashughulikiwa na Serikali ya Muungano katika ngazi zote za kimataifa. Kwa mfumo huu, Tanganyika inatumia jina la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kujifaidisha kwa mambo yote yasiyo mambo ya Muungano katika nyanja za kimataifa. Mifano michache ya maeneo haya ni elimu, afya, kilimo, mazingira, michezo, utamaduni, mawasiliano, miundombinu, usafiri baharini na angani ambapo katika jumuiya zote za kimataifa Tanganyika inashiriki ikitumia jina la Tanzania huku Zanzibar ikiachwa bila ya faida yoyote au ikiwepo basi ni ile inayotegemea hisani ya Tanganyika.

 

(d)            Mfumo uliopo wa Serikali mbili hautoi fursa ya wazi kwa upande mmoja wa Muungano (Tanganyika) kutetea maslahi yake ndani ya Muungano.

 

(e)             Wabunge wa Zanzibar wanashiriki katika Bunge la Muungano kujadili mambo ambayo siyo ya Muungano.

 

(f)              Mfumo uliopo unaochanganya mamlaka mbili (ile ya Serikali ya Muungano kwa mambo yote ya Muungano na ile ya Tanganyika kwa mambo yake yasiyokuwa ya Muungano) unaleta mkanganyiko mkubwa katika suala la kujua mipaka ya gharama za uendeshaji wa Muungano na mapato yanayotokana na taasisi za Muungano. Hali hiyo inaleta kutoaminiana kuhusiana na jinsi ya kuchangia gharama za uendeshaji na jinsi ya kugawana mapato baina ya nchi mbili zinazounda Muungano huo.

 

(g)            Ushahidi wa wazi wa kwamba mfumo uliopo umeshindwa kufanya kazi na wala hauwezi kurekebishika ni kwamba katika miaka 20 iliopita kumeundwa Tume na Kamati 8 kwa upande wa Serikali ya Jamhuri ya Muungano na Tume na Kamati 13 kwa upande wa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar mbali na kuwepo kwa Kamati ya Kudumu ya Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano ikiwajumuisha Waziri Mkuu wa Serikali ya Muungano na Makamu wa Pili wa Rais (zamani Waziri Kiongozi) wa SMZ lakini zote zimeshindwa kutatua matatizo ya Muungano na badala yake yamekuwa yakizidi kila uchao.

 

Serikali Tatu:

 

Baadhi ya vyama vya siasa na hata wasomi wa sheria wamekuwa wakipendekeza mfumo wa Serikali tatu (Serikali ya Muungano, Serikali ya Tanganyika na Serikali ya Zanzibar) kama suluhisho la matatizo ya Muungano. Hata hivyo, mfumo huu nao kwa sasa unaonekana bado hautaondoa manung’uniko kwa upande wa Zanzibar:

 

(a)           Mfumo wa Shirikisho la Serikali Tatu utatoa mamlaka ya ndani kwa nchi mbili zinazounda Muungano huu na kuwa na Serikali zake za kusimamia mamlaka hayo lakini bado mamlaka ya kidola (sovereignty) yatabaki katika Serikali ya Muungano. Madai makubwa yanayotolewa na Zanzibar hivi sasa yanahusu kurejesha ‘sovereignty’ ili kuifanya Zanzibar, serikali yake na viongozi wake wawe na hadhi ya kutambuliwa kitaifa na kimataifa. Hilo halitapatikana katika mfumo wa Serikali tatu.

 

(b)          ‘Sovereignty’ inayoshikiliwa na Serikali ya Muungano ambayo ndiyo itakayoziwakilisha nchi mbili kimataifa bado ina nafasi kubwa ya kuweza kutumika kumfaidisha mshirika mkubwa zaidi katika Muungano huo (Tanganyika) kuliko kwa mshirika mdogo (Zanzibar) kwa kule tu kujiona kwake ni mkubwa (big brother attitude).

 

(c)           Upo uwezekano wa kuendelea kuwepo kwa kutoaminiana kutokana na kila nchi kuwa na Serikali yake na hivyo kuwa na chombo cha kupanga mambo yake, hali inayoweza kuifanya Serikali ya Muungano ijikute haina uwezo wa kuzisimamia Serikali hizo za mamlaka ya ndani na hivyo kupoteza uhalali wake wa kisiasa.

 

(d)          Iwapo mambo ya Muungano yatabaki kama yalivyo au yatarekebishwa kwa uchache, kuwepo kwa mfumo wa Serikali tatu hakutorudisha mamlaka ya Zanzibar kupanga na kusimamia uchumi wake.

 

MFUMO MPYA WA MUUNGANO WA MKATABA:

 

Kama nilivyotangulia kueleza, tumedumu na Muungano wa Katiba kwa miaka 49 ambao pamoja na mafanikio ya kuziweka nchi zetu mbili pamoja katika kipindi chote hicho, bado umeshindwa kutujengea kuaminiana kwa dhati na zaidi umeshindwa kuyatatua matatizo ya msingi yanayotokana na maumbile ya mfumo huo.

 

Ulimwengu wa sasa umeshuhudia aina mpya ya mahusiano kati ya nchi huru ambao hutoa nafasi ya mashirikiano kwa maeneo yanakayokubaliwa na nchi husika huku kila nchi ikibaki na mamlaka yake kama nchi kamili (sovereign status). Mfumo huu kisheria unaitwa ‘CONFEDERATION’ ambao kimsingi ni Muungano wa Mkataba (Treaty based Union). Katika mfumo huu, yale maeneo ya ushirikiano huwekwa katika mkataba au mikataba baina ya nchi zilizoamua kushirikiana na hutoa fursa ya kurekebishwa kila mahitaji yanapojitokeza kwa kadiri na kwa mujibu wa makubaliano yaliyomo kwenye mkataba au mikataba hiyo.

 

Umoja wa Ulaya (European Union - EU) ni mfano mzuri wa muungano wa aina hii ambapo nchi wanachama zinashirikiana katika maeneo mengi yaliyomo katika Mikataba tofauti lakini kila nchi mwanachama imebaki kuwa na hadhi yake kama nchi na kubaki na uanachama wake katika Umoja wa Mataifa (UN) na hata katika mashirika mengine ya kimataifa. Katika Umoja wa Ulaya (EU), miongoni mwa maeneo wanayoshirikiana ni pamoja na:

 

(a)                       Sarafu moja;

(b)                      Uhamiaji;

(c)                       Uratibu wa sera za mambo ya nje za nchi wanachama;

(d)                      Ulinzi;

(e)                       Soko la pamoja la bidhaa, ajira na huduma;

(f) Uratibu wa sera za uchumi na fedha za nchi wanachama;

(g)                       Hifadhi ya mazingira;

(h)                      Viwango vya usalama na afya (health and safety standards).

 

Mfano mwengine wa ushirikiano kwa nchi za Ulaya nje ya EU ni ule unaohusu kuwa na visa ya pamoja kwa wageni wanaoingia katika nchi zilizo katika Mkataba wa Schengen ambao hutoa visa inayoitwa ‘SCHENGEN VISA’. Baadhi ya nchi wanachama wa EU na wasio wanachama wa EU (kwa mfano Norway) ni wanachama wa utaratibu huu.

 

Kwa upande mwengine, Jumuiya ya Afrika Mashariki (EAC) ni mfano mwengine mzuri wa ushirikiano wa aina hii. Mkataba wa Jumuiya ya Afrika Mashariki (East African Community Treaty) unatambua maeneo 17 ya ushirikiano miongoni mwa nchi wanachama. Maeneo hayo ni:

 

(a)                       Ushirikiano katika Masuala ya Sarafu na Fedha;

(b)                      Ushirikiano katika Biashara Huria na Maendeleo ya Biashara;

(c)                       Ushirikiano katika Uwekezaji na Maendeleo ya Viwanda;

(d)                      Ushirikiano katika Uwekaji Viwango, Kuhakikisha Ubora wa Bidhaa, Utabiri wa Hali ya Hewa na Vipimo;

(e)                       Ushirikiano katika Mahusiano na Jumuiya nyengine za Kikanda na za Kimataifa pamoja na ushirikiano na nchi washirika wa maendeleo;

(f) Ushirikiano katika Miundombinu na Huduma;

(g)                       Ushirikiano katika Kukuza Rasilimali Watu, Sayansi na Teknolojia;

(h)                      Ushirikiano katika Kilimo na Uhakika wa Chakula;

(i) Ushirikiano katika Utunzaji Mazingira na Usimamizi wa Maliasili;

(j) Ushirikiano katika Utalii na Usimamizi wa Wanyamapori;

(k)                       Ushirikiano katika Afya, Ustawi wa Jamii na Utamaduni;

(l) Ushirikiano katika Kukuza Ushiriki wa Wanawake katika Maendeleo ya Kijamii na Kiuchumi;

(m)                   Ushirikiano katika Masuala ya Sheria na Mahkama;

(n)                      Ushirikiano katika Mambo ya Kisiasa;

(o)                       Ushirikiano katika Sekta Binafsi na Asasi za Kiraia;

(p)                      Ushirikiano katika Uhuru wa Watu kwenda watakapo, Huduma za Kazi, Haki ya Kuishi na Ukaazi; na

(q)                      Ushirikiano katika Maeneo Mengine.

 

Lililo dhahiri katika miungano ya mikataba ya aina zilizotajwa hapo juu ni kuwa misuguano kwa kiasi kikubwa hupungua kwani kila nchi hubaki na mamlaka yake na uhuru wa kujiamulia na wakati huo huo kujenga misingi mizuri ya ushirikiano na nchi wanachama.

 

MUUNGANO WA MKATABA KATI YA ZANZIBAR NA TANGANYIKA:

 

1.     Kutokana na hoja nilizozieleza hapo juu, mimi ninapendekeza kuwa baada ya uzoefu wa miaka 49 wa Muungano wa Katiba (Constitutional Union) kati ya Zanzibar na Tanganyika ambao baadhi ya matatizo yake ya kimaumbile yameelezwa na kufafanuliwa hapo juu, sasa Zanzibar na Tanganyika ziingie katika mfumo wa “CONFEDERATION” kupitia Muungano wa Mkataba (Treaty based Union).

 

2.   Katika mfumo huo wa Muungano wa Mkataba, kutakuwa na Serikali mbili ambapo Jamhuri ya Tanganyika itakuwa na Serikali yake na Jamhuri ya Watu wa Zanzibar itakuwa na Serikali yake, zote mbili zikiwa na mamlaka kamili kitaifa na kimataifa, na kisha Serikali hizo mbili zitafunga mkataba wa mashirikiano baina yao ambao unaweza ukapewa jina la ‘Tanzanian Union Treaty’. Yale maeneo yatakayokubaliwa kuwa chini ya ushirikiano wa nchi mbili huru yatasimamiwa na Kamisheni ya Muungano (Tanzanian Commission) kama ilivyo kwa Kamisheni ya Ulaya (European Commission) au jina jengine lolote litakalokubaliwa na nchi mbili hizi.

 

3.   Kila nchi kati ya Zanzibar na Tanganyika zitakuwa na hadhi ya nchi kamili (sovereign states) na zitakuwa na uanachama wake katika Umoja wa Mataifa (UN) na pia katika jumuiya, mashirika na taasisi nyengine za kimataifa lakini kwa kuzingatia msingi wa mashirikiano zinaweza kukubaliana kuratibu sera zake za mambo ya nje kadiri zitakavyoona inafaa.

 

4.   Maeneo ya kuingia katika Mkataba au Mikataba ya Ushirikiano kati ya Zanzibar na Tanganyika yataamuliwa na serikali mbili zitakazokuwa na mamlaka kamili kila moja katika eneo lake. Mambo yanayoweza kufikiriwa ni pamoja na:

 

(i)        Ushirikiano katika Ulinzi na Usalama;

(ii)               Ushirikiano katika Uwekaji Viwango, Kuhakikisha Ubora wa Bidhaa, Utabiri wa Hali ya Hewa na Vipimo;

(iii)       Ushirikiano katika Mahusiano na Jumuiya nyengine za Kikanda na za Kimataifa pamoja na ushirikiano na nchi washirika wa maendeleo;

(iv)        Ushirkiano katika Kukuza Rasilimali Watu, Sayansi na Teknolojia;

 

5.    Kwa kufuata mfumo wa sheria za nchi za Jumuiya ya Madola (common law system) inapendekezwa kuwa Mkataba wa Ushirikiano kati ya Zanzibar na Tanganyika utiwe saini na Rais wa Jamhuri ya Zanzibar na Rais wa Jamhuri ya Tanganyika baada ya mazungumzo yatakayohusisha wawakilishi watakaoteuliwa kuunda timu za mashauriano na majadiliano za Serikali za nchi mbili hizi. Kabla ya kutiwa saini na Marais wa nchi mbili hizi, Rasimu ya Mkataba huu baada ya kukubaliwa ifikishwe mbele ya Bunge la Tanganyika na Baraza la Wawakilishi la Zanzibar kwa ajili ya kujadiliwa na kutolewa maoni na kisha Rasimu hiyo ipelekwe kwa wananchi wa Zanzibar na wa Tanganyika kupitia njia ya kura ya maoni kwa ajili ya kuidhinishwa kufuatana na Sheria ya Kura ya Maoni ya kila nchi.

 

NI ZIPI FAIDA ZA MUUNGANO WA MKATABA:

 

1.     Hakuna khofu ya nchi moja kuimeza au kuitawala nchi nyengine.

2.   Kila nchi inabaki na uhuru na  mamlaka yake kamili kitaifa na kimataifa kuamua mambo yake.

3.   Kila nchi mwanachama ina uhuru wa kujitoa katika jambo lolote ililoamua mwanzo kushirikiana pale inapoona hakuna maslahi au faida kuendelea nalo.

4.   Huvutia nchi nyingi kuingia katika Muungano wa aina hiyo kwa sababu hakuna khofu ya kupoteza mamlaka au kupunguziwa madaraka au mambo yake kuamuliwa na nchi nyengine.

5.    Mahusiano huwa ni ya kirafiki na ya ujirani mwema yanayopelekea kuaminiana na kuondoa kutiliana shaka kusikokwisha.

 

 

 

 

KAMA NI MKATABA, KWA NINI ISIWE KUPITIA EAC TU?

 

Wapo baadhi ya watu wakiwemo Makamishna wa Tume ya Mabadiliko ya Katiba waliohoji kwamba iwapo Zanzibar inaona hakuna haja tena ya kuendelea na mfumo uliopo wa Muungano na badala yake inataka kuwa na mashirikiano kupitia Muungano wa Mkataba kwa mambo yatakayokubaliwa, kwa nini mashirikiano hayo yasiwe kwa kupitia Jumuiya ya Afrika Mashariki (EAC) ambayo pia ni aina ya Muungano wa Mkataba? Wenye hoja hiyo wanasema basi wacha Zanzibar na Tanganyika zikutane Afrika Mashariki.

 

Hoja hii ni nzuri lakini haizingatii uhalisia wa mambo. Pamoja na kuundwa upya kwa Jumuiya ya Afrika Mashariki (EAC) kupitia Mkataba ambao unahusisha maeneo mengi kati ya yale niliyoyataja hapa kwamba yanaweza kufikiriwa kuwa ya ushirikiano kati ya Zanzibar na Tanganyika, ukweli unabaki kuwa utekelezaji wake katika eneo la Afrika Mashariki umekuwa ni mdogo mno.

 

Nchi tano zinazounda Jumuiya ya Afrika Mashariki – Tanzania, Kenya, Uganda, Rwanda na Burundi – hazionekani kuwa zimejenga kuaminiana kwa dhati licha ya matamshi ya hamasa za kisiasa yanayotolewa na viongozi wake. Ndiyo maana maeneo mengi yamebaki katika makaratasi lakini hakuna utekelezaji. Hata hatua zilizotangazwa kuwa zinapaswa kufikiwa kuelekea Shirikisho la Afrika Mashariki hazionekani kutekelezwa kwa dhati na badala yake kumekuwa na kutegana na hata kuogopana.

 

Baada ya miaka 49 ya kuwa pamoja katika Muungano (pamoja na matatizo yake yote), Zanzibar na Tanganyika angalau zimekuwa na uzoefu wa kufanya kazi pamoja. Kubadili aina ya mahusiano na mashirikiano yake kutoka kwenye Muungano wa Kikatiba kwenda kwenye Muungano wa Mkataba kunaweza kuwa jambo linalowezekana zaidi katika utekelezaji kuliko nchi hizi tano na pengine kunaweza kutoa mfano wa vipi utekelezaji wa maeneo hayo ya mashirikiano unavyopaswa kuendeshwa na kusimamiwa.

 

Isitoshe unaweza tukawa mwanachama wa EAC na bado kukawepo ushirikiano wa Zanzibar na Tanganyika kupitia mkataba baina yao peke yao. Duniani iko mifano ya nchi ambazo pamoja na kuwa ni wanachama wa pamoja wa miungano au jumuiya za ushirikiano zenye kushirikisha nchi nyingi zaidi, bado kunakuwa na nchi mbili ambazo kutokana na historia ya ushirikiano wake zinabaki kuwa na ushirikiano wao mwengine unaozihusisha nchi hizo tu. Mfano katika suala la ushirikiano wa ulinzi, pamoja na kwamba Marekani na Uingereza zote mbili ni wanachama wa NATO lakini bado nchi mbili hizo zina mikataba ya peke yao kuhusiana na ushirikiano wa ulinzi kati yao. Katika Ulaya, kuna mashirikiano kupitia mkataba baina ya nchi tatu – Belgium,  The Netherlands and Luxembourg (BENELUX) – lakini bado zote ni wanachama wa Umoja wa Ulaya (European Union).

 

KIPINDI CHA MPITO:

 

Hali ya kubadilisha msingi wa mahusiano ya Zanzibar na Tanganyika kutoka kwenye Muungano wa Katiba (Constitutional Union) kwenda kwenye Mfumo wa kisasa wa Muungano wa Mkataba (Treaty based Union) bila shaka utahusisha mabadiliko makubwa ambayo yanahitaji kipindi cha mpito (transitional period) na kuwepo kwa utaratibu wa mpito (transitional process) kutoka mfumo uliopo sasa kwenda kwenye mfumo mpya.

 

Katika kipindi hicho cha mpito, maoni ya watu wa Tanganyika kuhusu Katiba yaliyokusanywa na Tume ya Mabadiliko ya Katiba yanaweza kutumika kuandaa rasimu ya Katiba ya Tanganyika na baada ya kupitisha Katiba ya Tanganyika, Serikali za nchi mbili (Zanzibar na Tanganyika) zikae pamoja kuchagua maeneo ya kushirikiana na kisha kuandaa Mkataba wa Mashirikiano yao.

 

Kutahitajika kuundwe timu ya watalaamu wa masuala ya kisheria na kiutawala kutoka Zanzibar na Tanganyika na pia kuhusisha kuomba wataalamu waliobobea wa fani hizo na waliosimamia vipindi vya mpito kama hivi katika nchi nyengine kuja kusaidia kuweka utaratibu maridhawa utakaohakikisha kuendelea kuwepo kwa mahusiano ya kidugu ya nchi hizi katika mfumo mpya. Jumuiya za kimataifa kama Umoja wa Mataifa (UN), Jumuiya ya Madola (The Commonwealth), Umoja wa Afrika (AU), Umoja wa Ulaya (EU) na nchi jirani na nchi za nje zenye kufuata mfumo wa sheria za kiingereza kama Uingereza, Malaysia, Singapore, Kenya, Uganda na Afrika Kusini zinaweza kuombwa kusaidia kutoa wataalamu watakaokuwa kama washauri waelekezi (consultants) kwa nchi zetu wakati wa maandalizi ya utaratibu wa mpito (transitional process) kuelekea Muungano wa kisasa wa Mkataba wa Zanzibar na Tanganyika chini ya misingi ya uhuru, usawa, udugu na ukweli.

 

MUUNGANO WA MKATABA NI SAWA NA KUVUNJA MUUNGANO?

 

Wasioitakia mema Zanzibar au wang’ang’anizi wa mfumo uliopo wa Muungano waliouzoea (pengine kwa sababu unawanufaisha wao) wanaweza kudai kwamba hatua hizi zinazopendekezwa haziashirii nia njema ya kuendeleza na kuimarisha Muungano. Mimi binafsi na wenzangu tunaoamini katika Muungano wa Mkataba hatuamini hivyo. Tunaamini katika kuwa wakweli na wawazi, kwamba hivyo ndivyo mahitaji ya wakati huu na zama hizi yanavyodai.

 

Ulimwengu unabadilika kwa kasi. Zama za kuendesha mambo kwa ubabe na ukichwa ngumu zimepitwa na wakati. Tuache ile tabia ya kuyaona mapendekezo ya kubadili mfumo wa Muungano kuwa yana nia ya kuuvunja Muungano huo. Muungano ili udumu unahitaji ridhaa ya walioungana. Muasisi wa Muungano huu, Mwalimu Nyerere mwenyewe, aliwahi kueleza umuhimu wa ridhaa katika masuala haya na kuonyesha kwamba ridhaa ya mshirika mmojawapo ikiondoka, Muungano hauwezi kusimama. Alisema mwaka 1968:

 

“If the mass of the people of Zanzibar should, without external manipulation, and for some reason of their own, decide that the Union was prejudicial to their existence, I could not bomb them into submission … The Union would have ceased to exist when the consent of its constituent members was withdrawn.” [11]

 

“Iwapo wananchi walio wengi wa Zanzibar wataamua, bila ya msukumo wa kutoka nje, na kwa sababu zao wenyewe, kwamba Muungano unaathiri kuendelea kuwepo kwao, siwezi kuwalazimisha kwa kuwapiga mabomu … Muungano utasita kuendelea pale ridhaa ya washirika wake itakapoondolewa.”

 

Wazanzibari ni watu wenye historia ya maingiliano ya jamii za watu mbali mbali na hivyo hawawezi kukataa umoja, alimradi tu umoja huo uwe na maslahi na faida kwao. Mfumo uliopo sasa hauinufaishi Zanzibar na hivyo haukubaliki kwa Wazanzibari. Koti la Muungano kama lilivyo sasa linabana sana. Wakati umefika tushone koti jipya kwa mujibu wa mahitaji ya zama hizi.

 

Hakuna mabadiliko yasiyowezekana kufanyika na kusimamiwa vyema iwapo tutatumia njia ya mazungumzo. Mazungumzo makini, ya kina na yenye kuambatana na nia njema kwa wahusika wote ndiyo njia pekee ya matumaini katika kuyapatia ufumbuzi matatizo yanayolikabili Taifa letu. Hakuna mbadala wa mazungumzo. Nje ya mazungumzo ni fujo.



[1] Nnoli, O (1978) Self Reliance and Foreign Policy in Tanzania: The Dynamics of the Diplomacy of a New State, 1961 to 1971, NOK Publishers (New York), Uk. 91; Othman, Haroub (1979) State Succession with regard to International Treaties – Some Theoretical Observations on the Practice of Anglophonic Africa, Ph.D. Thesis, University of Dar es Salaam (Dar es Salaam), Uk. 413.
[2] Mazrui, Ali A. (1994) ‘Imperialism after the Empire: Lessons from Uganda and Tanzania The Sunday Nation (Nairobi), May 22, 1994
[3] Kwa maelezo zaidi kuhusiana na nadharia hizi, angalia kwa mfano, Nyerere, Julius K. (1965) ‘The Nature and Requirements of African Unity’ katika jarida la African Forum, Vol. 1, No. 1 (1965), Uk. 46.
[4] Angalia ‘A Declaration of Federation by the Governments of East Africa on June 5, 1963’ lenye Kumbukumbu Nam. 13/931/63/PDT/1/1 kama lilivyochapishwa katika Tanganyika Government (1964) Meetings and Discussions on the Proposed East African Federation, Ministry of Information (Dar es Salaam).
[5] William Edget Smith (1971) We Must Run While They Walk: A Portrait of Africa’s Julius Nyerere, Gollancz (London), Uk. 121.
[6] Nyerere, Julius K. (1966) Freedom and Unity, Oxford University Press (Dar es Salaam), Uk. 300.
[7] Shivji, Issa G. (1994) ‘The Union: Hopes and Fears’ The Family Mirror (Dar es Salaam), First Issue, January 1994, uk. 5
[8] Msekwa, Pius (1994) ‘The State of the Union’ - Paper presented to a Seminar on the State of the Union, Mkonge Hotel, Tanga 25 - 27 February, 1994.
[9] Mazrui, Ali A. (1994) ‘Imperialism after the Empire: Lessons from Uganda and Tanzania The Sunday Nation (Nairobi), May 22, 1994
[10] Shivji, Issa G. (2005) ‘Sovereignty and Statehood in Zanzibar in the Union: Critical Comments on S.M.Z. v. Machano Khamis Ali & 17 Others, kama ilivyochapishwa katika Peter, Chris Maina and Othman, Haroub (2006) Zanzibar and the Union Question, Zanzibar Legal Service Centre Publication Series (Zanzibar), Uk. 186.
[11] The Observer (London), April 20, 1968

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.