Habari za Punde

Tanzania Kunufaika na Dola Milioni 20 za Miradi

 

Mshauri wa Rais katika masuala ya Mazingira na Mwenyekiti wa Kundi la Majadiliano la Afrika kuhusu Mabadiliko ya Tabianchi (AGN) Dkt. Richard Muyungi akizungumza na Watanzania wanaoshiriki Mkutano wa 30 wa Umoja wa Mataifa wa kuhusu Mabadiliko ya Tabianchi (COP 30) unaoendelea katika Jiji la Belem nchini Brazil.

Tanzania ni miongoni mwa nchi zinazotarajia kunufaika na fedha kiasi cha hadi dola milioni 20 kwa ajili ya utekelezaji wa miradi ya kukabiliana na athari za mabadiliko ya tabianchi kupitia Mfuko wa Kukabiliana na Hasara na Uharibifu.

 

Hayo yamesemwa na Mshauri wa Rais katika masuala ya Mazingira na Mwenyekiti wa Kundi la Majadiliano la Afrika kuhusu Mabadiliko ya Tabianchi (AGN) Dkt. Richard Muyungi alipokutana na Watanzania wanaoshiriki Mkutano wa 30 wa Umoja wa Mataifa wa kuhusu Mabadiliko ya Tabianchi (COP 30) unaoendelea katika Jiji la Belem nchini Brazil.

 

Dkt. Muyungi amesema kuwa katika utekelezaji huo tayari zimetengwa fedha kiasi cha dola milioni 250 kwa mwaka ujao kwa kwa ajili ya kufadhili miradi hiyo ambayo Tanzania ni nchi mnufaika.

 

“Nasisitiza huu sio mkopo bali ni ufadhili na hadi sasa tuna mambo ya kufuatilia na sisi kama nchi tumepewa kipaumebele hivyo tunaweza kuwa na miradi hata miwili ambayo inaweza kuwa na manufaa makubwa, naomba Ofisi ya Makamu wa Rais tuteua mtu mmoja yaani focal person kwa ajili ya Mfuko wa Kukabiliana na Hasara na Uharibifu,” amesema.

 

Kubwa zaidi amebainisha kuwa mwaka 2025 Tanzania imeteuliwa kuwa Kituo cha Santiago ambacho kitakuwa kinaratibu msaada wa kiufundi kwa nchi zinazoathiriwa na hasara na uharibifu unaotokana na mabadiliko ya tabianchi. 

 

Aidha, Dkt. Muyungi ameomba Watanzania kutoka serikalini na sekta binafsi wanaoshiriki mkutano huo wenye takriban washriki 60,000 kusimama kama nchi na kujenga mitandao ya kuchangamkia fursa ili kuendelea kuinufaisha nchi. 

 

“Kama tunavyoona hapa COP 30 yapo mabanda mengi yenye wingi wa washiriki nawaomba tutumie fursa hii kutengeneza network, tuna timu ya negotiation tufuatilie fursa za benki , NGOs na Serikali ili tukitoka hapa tutoke na faida,” amesisitiza.

 

Vilevile, Dkt. Muyungi alitumia nafasi hiyo kuwaeleza washiriki hao kuwa wana jukumu la kuitangaza Dira ya Maendeleo 2025 na Serikali ya Tanzania imetekeleza mambo gani ya msingi kwa wananchi na hivyo kuchagiza upatikanaji wa fursa zaidi kwa maendeleo endelevu

 

Kwa upande wake Naibu Katibu Mkuu (Mazingira) Ofisi ya Makamu wa Rais Prof. Peter Msoffe amesema kuwa Ofisi hiyo imejipanga kuhakikisha kila fursa inayotokea inafanyiwa kazi.

Prof. Msoffe ametoa wito kwa Watanzania kuendelea kutafuta fursa na kuomba ushauri wa kitaalamu kutoka kwa wataalamu kulingana na aina ya fursa wanayokutana nayo.

 

“Ndugu zangu kama alivyozungumza Mwenyekiti (Dkt. Muyungi) tutafute fursa na kama itakuwa inahusu benki basi unaweza kuzishirikisha benki husika na kama utaona fursa kuhusu biashara ya kaboni usisite kuishirikisha Ofisi ya Makamu wa Rais,” amesema.

 

Naye Naibu Katibu Mkuu Wizara ya Fedha Bi. Amina Khamis Shaaban ameomba ushirikiano kwa wote wanaokutana na fursa lengo ni kusukuma mbele maendeleo ya nchi.

 

Bi. Amina amesema kuwa Wizara hiyo iko tayari kukutana na wadau wote wa miradi ambayo inakuwa tayari imetayarishwa na kupata idhini huku akisisitiza yote haya yanafanyika ili kuendelea kuifanya nchi iendelee kunufaika.

Naibu Katibu Mkuu Wizara ya Fedha Bi. Amina Khamis Shaaban akizungumza kwenye banda la maonesho la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania wakati Mkutano wa Mkutano wa 30 wa Umoja wa Mataifa wa kuhusu Mabadiliko ya Tabianchi (COP 30) unaoendelea katika Jiji la Belem nchini Brazil
Naibu Katibu Mkuu (Mazingira) Ofisi ya Makamu wa Rais Prof. Peter Msoffe akizungumza kwenye banda la maonesho la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania wakati Mkutano wa Mkutano wa 30 wa Umoja wa Mataifa wa kuhusu Mabadiliko ya Tabianchi (COP 30) unaoendelea katika Jiji la Belem nchini Brazil

Sehemu ya Washiriki na viongozi kutoka Tanzania wakiwa katika picha ya pamoja ya kwenye banda la maonesho la Tanzania kwenye Mkutano wa 30 wa Umoja wa Mataifa wa kuhusu Mabadiliko ya Tabianchi (COP 30) unaoendelea katika Jiji la Belem nchini Brazil Novemba 14, 2025.

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.