Habari za Punde

Wimbi uvamizi maduka ya dawa watisha


Na Mwandishi wetu
WIMBI la ujambazi limeanza kuibuka upya katika manispaa ya mji wa Zanzibar kwa kuvamiwa wafanyabiashara wa dawa katika maeneo mbali mbali.
Katika tukio la hivi karibuni, muuzaji wa duka la Izamir Pharmacy Limited liliopo Majestiki mjini Unguja, alinusurika kushambuliwa na majambazi hayo wakati akiwa njiani kuelekea nyumbani kwake.
Mfanyabiashara huyo, Nizar Machano aliiambia  gazeti hili kwamba watu wanne ambao anaamini kuwa ni majambazi walimvamia katika eneo la Maisara majira ya saa 3:45 usiku.
Alisema lengo la majambazi hayo ni kumshambulia na kumpora fedha lakini hata hivyo hawakufanikiwa.

Alisema wakati akiwa Maisara majambazi hao walimzingira kwa mbele kwa kutumia gari aina ya Scudo  na baada ya yeye kusimama majambazi manne yalishuka kwenye gari wakiwa na mapanga kwa lengo la kumshambulia.

“Kabla ya kushuka kwenye gari lao sikufahamu kuwa walikuwa majambazi, lakini baadae niligundua kuwa hawakuwa watu wema. Nilifanya maamuzi ya haraka ya kuliendesha gari langu kwa kasi kupitia kwenye mvinje na nikakimbia kituo cha polisi Madema,” alisema.
Alisema baada ya kuwakimbia majambazi hayo, alikimbilia polisi kuomba msaada wa polisi ambao walimuongoza hadi nyumbani kwake.
Hilo si tukio la kwanza kwa majambazi kuvamia maduka ya kuuzia dawa.
Katika tukio jengine la hivi karibuni majambazi hayo yalivamia duka la dawa la Mwembeladu.
Katika tukio  lilitokea mwezi wa Desemba mwaka 2012,  majambazi yaliyokuwa na silaha yalivamia duka la dawa liliopo karibu na hospitali kuu ya Mnazimmoja na kufanikiwa kuiba kopyuta na mamilioni ya fedha.
Aidha katika tukio jengine lililotokea mwaka 2012, majambazi yalivamia dula la dawa la Karibu  Pharmacy na kumuua mlinzi wa duka hilo na kupora mamilioni ya fedha.
Kamanda Polisi wa Mkoa wa Mjini Magharibi, ACP, Azizi Juma Mohamed alikiri kupokea taarifa za mfanyabiashara huyo kuvamiwa na majambazi.
Alisema mfanyabiashara huyo baada ya kufanikiwa kuwakwepa wahalifu hao alikimbilia kituo cha polisi ambapo alipatiwa ulinzi hadi nyumbani kwake.
Aliwataka wananchi na wafanyabiashara kuwa makini  na waangalifu wanaposafirisha fedha pamoja na kuomba msaada wa kusindikizwa na polisi wanapokuwa na kiwango kikubwa cha fedha.
Aidha aliwataka kutoa taarifa mapema iwapo wataona vitendo wanavyovitilia mashaka.
"Huduma ya kuwapa ulinzi wafanyabiashara inatolewa bure lakini sijui kwani wanakuwa wasiri kulitumia jeshi la polisi kuwapa ulinzi,” alisema.

2 comments:

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.