Habari za Punde

Dubai kuisadia Zanzibar utunzaji nyaraka



Na Hassan Hamad, OMKR
JUMUIYA ya Jumaa Al-Majid Foundation ya Dubai imesema iko tayari kushirikiana na Zanzibar katika utunzaji nyaraka na kumbukumbu ili kuzihifadhi katika mfumo wa kisasa.

Mkuu wa taaluma na mambo ya nje wa Jumuiya hiyo, Dk. Azzeddine Benzeghiba alieleza hayo alipokuwa na mazungumzo na Makamu wa Kwanza wa Rais wa Zanzibar, Maalim Seif Sharif Hamad ofisini kwake Migombani.

Dk. Azzeddine alisema nyaraka ni kitu muhimu cha kukienzi katika kutunza historia ya nchi, hivyo taasisi hiyo itashirikiana kwa karibu na Zanzibar katika kuhakikisha inasaidia kutunza nyaraka na historia yake.

Jumuiya hiyo pia imeonesha mwelekeo wa kushirikiana na taasisi za elimu nchini zikiwemo skuli za sekondari, vyuo vikuu, maktaba na taasisi binafsi za elimu.


Nae Maalim Seif Sharif Hamad alisema kuna haja kubwa ya kuzihifadhi nyaraka katika mfumo wa kisasa ili kutunza historia ya Zanzibar.

Alisema hali ya utunzanji na uhifadhi wa nyaraka kwa sasa sio ya kuridhisha, hivyo ipo haja ya kushirikiana na taasisi hiyo katika kutunza nyaraka na kumbukumbu za taifa.

Kuhusu elimu, Maalim Seif alisema Zanzibar imepata mafanikio makubwa katika miaka ya hivi karibuni kwa kufanikiwa kuwepo kwa vyuo vikuu vitatu kikiwemo Chuo Kikuu cha Taifa cha Zanzibar (SUZA), pamoja na kuwasajili watoto wote wenye sifa ya kuanza skuli.

Kwa upande mwengine Maalim Seif alisema Zanzibar inaendelea kuwakaribisha wawekezaji kutoka maeneo mbali mbali kuja kuwekeza hasa katika sekta ya utalii ambayo imekuwa ikiimarika kila mwaka.

Alisema miundombinu ya uwekezaji katika sekta hiyo imeimarika baada ya kuwepo kwa usafiri wa moja kwa moja kutoka Oman hadi Zanzibar, na kwamba serikali inaangalia uwezekano wa kuwepo usafiri zaidi wa moja kwa moja utakaoziunganisha nchi za kigeni na Zanzibar.
Alisema tayari serikali imefanya mazungumzo na makampuni mbali mbali ya ndege yakiwemo ya Uturuki, Emirates na Anatalia la Italia, ili kuweza kuleta ndege zao moja kwa moja, na kwamba yameonesha mwelekeo mzuri.

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.