Na
Mwandishi wetu, Dodoma
RAIS
Jakaya Kikwete ameliagiza jeshi la polisi kupambana na utovu wa maadili ili
lipunguze kunyooshewa vidole kuhusu
tuhuma za rushwa na kasi ndogo ya upelelezi wa makosa.
Rais
Kikwete aliyasema hayo jana wakati wa
akifungua mkutano mkuu wa maofisa waandamizi wa jeshi la polisi katika ukumbi
wa Bunge, Dodoma
“Suala la rushwa nimekuwa nikilikemea mara kwa
mara lakini lakini kutokana na umuhimu wake leo narudia tena kulisema,” alisema
Rais Kikwete.
Alisema
tuhuma za rushwa zinachafua sifa nzuri ya jeshi la polisi ingawa alisema sio
wote wanaojihusisha na vitendo vya
kuomba na kupokea rushwa.
“Jeshi
lina maofisa na askari wengi ambao ni waadilifu na wachapa kazi wenye uzalendo
wa kweli kwa nchi yetu. Lakini waswahili wana msemo usemao: “nazi mbovu harubu
ya nzima”.
Alisema
askari wachache wasiokuwa waadilifu wanaweza kuharibu sifa ya wengi walio
wazuri.
Aidha
amelitaka jeshi la polisi kuweka utaratibu mzuri wa kupokea na kushughulikia
maoni na malalamiko ya wananchi na kutaka wale watakaobainika kupokea rushwa
wasionewe aibu.
Aidha
alisema pamoja na vitendo vya kuomba na kupokea rushwa, jeshi la polisi
linalalamikiwa na wananchi kwa kuendesha upelelezi wa kesi za jinai kwa kasi
ndogo hali inayosababisha kesi zilizoko mahakamani kuchukua muda mrefu
kumalizika kuliko inavyostahili.
“Mimi
nilidhani tulipotenganisha shughuli za upelelezi na uendesha mashtaka
ingesaidia lakini inaelekea bado.
Nawasihi maafisa, wakaguzi na askari waliopangiwa kufanya kazi za
upelelezi kuifanya kazi hiyo kwa ufanisi na kasi inayokubalika kisheria. Mkifanya hivyo mtasaidia kupunguza moja ya
kero kubwa na ya muda mrefu ya msongamano wa mahabusu magerezani,” alisema.
Aliwataka
polisi kuendelea kuwashirikisha wananchi kwa karibu katika kupambana na
uhalifu, akisema hilo
ndio jawabu sahihi la uhaba wa polisi nchini.
Rais Kikwete alieleza jinsi alivyovutiwa na kauli mbiu ya
mkutano huo inayosema ‘Tujenge Uwezo wa Jamii na Polisi Kukabiliana na Vurugu,
kwa kuimarisha utii wa sheria bila shuruti.”
Alisema kauli mbiu hiyo imebeba ujumbe muafaka katika
mazingira yaliyopo sasa nchini.
Alisema hivi sasa matukio ya vurugu yanaanza kuwa taarifa
za kawaida na kuongeza kuwa kila kukicha au kila baada ya muda mfupi kuna tukio
la vurugu kutokana na sababu mbalimbali.
Alisema kauli mbiu hiyo, inakumbusha ukweli huo na umuhimu
wa jamii na polisi kushirikiana katika kukabiliana na vurugu nchini.
Aidha alisema inasisitiza nafasi ya utii wa sheria bila
shuruti katika kuzuia vurugu zisitokee au pale zinapotokea ziweze kumalizwa
haraka bila ya madhara makubwa kwa pande husika.
“Mimi naamini kama shabaha za kauli mbiu hii zitatimia,
vurugu hazitakuwepo nchini na Tanzania patakuwa mahali salama kuishi kwa kila
mtu,” alisema.
Alisema vurugu ni changamoto mpya ya usalama wa raia, mali
zao na nchi ambayo polisi hawana budi
kukabiliana nayo.
Alisema polisi hawanabudi kukaa kitako na kutafakari kwa
makini kiini cha vurugu na jinsi ya kukabiliana nazo kwa maana ya kuzuia
zisitokee na zinapotokea zinamalizwa haraka bila ya kuwa na athari kubwa au
kupunguza madhara kwa watakaoathirika.
Alisema kila mdau anatakiwa kuutambua wajibu huo na
kuhakikisha kuwa anatimiza ipasavyo yale yanayomhusu.
“Nyinyi katika jeshi la polisi mnajua vyema wajibu wenu
katika kudhibiti vurugu. Bahati nzuri
wajibu huo umetamkwa kisheria na una miongozo yake ambayo imeandikwa na
hufundishwa katika vyuo na hufanyiwa mazoezi vikosini.Nawaomba suala la kuzuia
na kudhibiti vurugu mlipe kipaumbele cha juu,” alisema.
Alisema siku za nyuma haikuwa lazima kufanya hivyo kwa
sababu halikuwa tatizo kubwa lakini siku hizi hali imebadilika.
Alisema vurugu zinakuwa nyingi na za aina nyingi hivyo
kugeuka kuwa shughuli kubwa kwa jeshi la polisi.
“Vurugu zinasababishwa
na mambo mengi, zipo zinazosababishwa na vyama vya siasa kwa kufanya mikutano
na maandamano yasiyoruhusiwa. Wakati
mwingine hata pale yaliporuhusiwa wahusika hufanya mambo yasiyohusika ama
wakati au baada ya mkutano,” alisema.
Lakini alisema zipo pia vurugu zinazosababishwa na kauli na
vitendo vya baadhi ya viongozi wa dini na waumini wao akitolea mfano wa vurugu
za hivi karibuni zilizotokea Buseresere, Geita.
“Hatukuwa
na hali tuliyonayo sasa ya watu kutumia
njia ya vurugu kuelezea hisia zao au kujaribu kutatua matatizo
yanayowakabili. Maadam sasa yameanza kujitokeza
kwa nguvu hatunabudi kukabiliana kisawasawa na aina hii ya uhalifu.
Hatunabudi kujifunza namna bora ya kukabiliana
na vurugu. Hatuwezi kusema yatapita, lazima tukubali ukweli kuwa matukio haya
yanaweza kuendelea kuwepo na hata kuongezeka siku za usoni,” alitahadharisha.
No comments:
Post a Comment