JK awaagiza polisi kuzishirikisha nchi rafiki kuchunguza
Na waandishi wetu Zanzibar, DSM
MKUU wa jeshi la Polisi nchini IGP, Said Mwema amesema
timu ya makachero waliobobea katika
masuala ya kukusanya taarifa na kiintelejesia wametumwa Zanzibar kuchunguza
tukio la mauaji ya Padrid, Evaristitus Mushi wa kanisa katoliki Parokia ya
Mtakatifu Joseph, Shangani yaliyofanywa na watu wasiojulikana jana asubuhi
katika eneo la Beit El Ras mjini Zanzibar.
Akizungumza na waandishi wa habari jijini Dar es
Salaam kufuatia mauaji hayo, IGP Mwema
alisema tayari watu watatu wanashikiliwa na polisi wakihusishwa na mauaji hayo.
Alisema polisi itawakamata na kuwachukulia hatua kali
watu wote waliohusika na mauaji hayo pamoja na wengine wanaochochea, kufadhili,
kushiriki na kushawishi vitendo vya kihalifu.
IGP Mwama alilaani mauaji ya Padri huyo na kusema jeshi
litawasaka na kuwakamata wauaji hao.
Aidha alisema polisi imeanza kuwatia mbaroni watu wote
wanaoonekana kutoa kauli za uchochochezi kwa mahojiano.
Kwa upande wake Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania,
Jakaya Mrisho Kikwete amelaani mauaji hayo na kusema serikali haiwezi kukubali
kuona kikundi cha watu kinavuruga amani na utulivu uliopo na kuingiza nchi katika mgogoro wa kidini.
Aidha ameliagiza jeshi la polisi kushirikiana na vyombo
vyengine vya ulinzi na usalama vya ndani na nchi jirani kufanya uchunguzi wa
kina kuhusu mauaji ya viongozi wa dini na matukio mengine yanayotishia uvunjifu
wa amani.
Akizungumza na waandishi wa habari makao makuu ya polisi
Kilimani, Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi Dk. Emmanuel Nchimbi aliyaita mauaji
ya Padri huyo kuwa ya kigaidi.
Alisisitiza kuwa jeshi la polisi litafanya kila
liwezekanalo kuwatia mbaroni wauaji na
kuwafikisha katika vyombo vya sheria.
Aidha alisema serikali imeshatoa ruhusa kwa jeshi la
polisi kushirikiana na vyombo vyengine vya usalama kutoka nje ya nchi
kuchunguza chanzo cha mauaji hayo pamoja na kuwatia nguvuni wahusika.
Alisema mauaji hayo yana nia ya kuwachonganisha
Watanzania kidini, lakini aliwataka Watanzania kuendelea kuwa wamoja na
kuimarisha misingi ya upendo, amani na utulivu uliopo.
Alisema mazingira ya muaji ya Padri Mushi yanalingana na
tukio la kujeruhiwa kwa risasi Padri
Ambros Mkenda, tukio ambalo lilitokea Disemba mwaka uliopita.
Aidha alisema silaha iliyotumika kumshambulia Padri Mushi
ndio ile ile iliyotumika kumjeruhi Padri Mkenda.
Kwa upande wake serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar
imepokea kwa masikitiko makubwa taarifa za mauaji ya Padri huyo.
Waziri wa Nchi, Ofisi ya Makamu wa Pili wa Rais wa
Zanzibar, Mohamed Aboud ameliagiza jeshi
la polisi kufanya uchunguzi wa kina ili kuwatambua wale wote waliohusika na
mauaji hayo.
Amewaomba wananchi kuendea kutulia na kuliacha jeshi la
polisi kutekeleza wajibu wake.
Pia alisema serikali inatoa mkono wa pole kwa familia wa
marehemu pamoja waumini na kuwataka kuwa
wastahamilivu katika kipindi hichi
kigumu.
Kwa upande wake, Kamishna wa Polisi Zanzibar, Mussa Ali
Mussa alisema Padri Mushi,alipigwa risasi akiwa ndani ya gari na kujeruhiwa
vibaya sehemu za kichwa na kifua.
Alisema baada ya
tukio hilo baadhi ya waumini wa kanisa hilo waliofika katika kanisa hilo kwa ajili ya ibada, walimpeleka Padri Mushi
katika hospitali kuu ya Mnazimmoja kwa matibabu
na alifariki muda mfupi baadae.
“Kutokana na uzito wa tukio hili jeshi la polisi Zanzibar
linaendelea na upelelezi wa kina kuhakikisha wahusika wote wanafikishwa katika
vyombo vya kisheria,“ alisema.
“Natoa wito kwa wananchi washirikiane na maafisa wetu juu
ya taarifa zozote zinazohusiana na tukio hili ili tuweze kutekeleza majukumu yetu
kwa wakati,” alisisitiza.
Kamanda wa polisi mkoa wa Mjini Magharibi,ACP Aziz
Mohamed alisema kwa sasa jeshi la polisi linaendelea na doria katika maeneo
mbalimbali ya mjini ili kuhakikisha wale wote waliohusika katika mauaji ya Padri
huyo wanakamatwa.
Naye Mkuu wa Mkoa Mjini Magharib, Abdallah Mwinyi alifika
katika hospitali ya Mnazimoja kuwafariji jamaa,ndugu na waumini wa dini hiyo
waliofika katika eneo hilo kwa ajili ya kufuatilia hatima ya kiongozi wao.
Akizungumzia tukio hilo,msemaji wa kanisa hilo ambaye pia
ni Katibu Mkuu wa Kanisa Katoliki,jimbo la Zanzibar, Padri Cosmas Shayo
aliwataka waumini wa kanisa hilo,kuwa wavumilivu katika kipindi hichi hadi
suala hilo litakapopatiwa ufumbuzi.
Alisema uongozi wa kanisa hilo,umepokea mauaji hayo kwa
masikitiko makubwa na pia kufariki kwa Padri huyo ni miongoni mwa pigo kubwa
kwa waumini na kanisa kwa ujumla.
Alisema kanisa linathamini mchango mkubwa uliotolewa na
marehemu wakati wa uhai wake,katika kuliendeleza kanisa kwenye huduma za
kiimani na kiroho kwa waumini wa kanisa.
Baadhi ya mashuhuda ,waliozungumza kwa nyakati tofauti
katika eneo la tukio, walisema kwamba wakati waumini wa kanisa hilo wakijiandaa
kwa ibada,pembeni mwa kanisa hilo kulikuwa na watu watatu ambao hawajulikani na
mara baada ya kufika Padri huyo walisikia milio ya risasi na baadae watu wawili
wakaondoka kwa kutumia vespa mwengine akakimbilia vichochoroni.
Kufuatia mauaji hayo hali ya mji wa Zanzibar umekuwa
kimya kwa muda mrefu huku askari polisi wenye silaha wakionekana kuranda randa
kila kona ya barabara za mji huo kuimarisha doria huku wananchi wakiwa
wamejikusanya makundi kuzungumzia mauaji ya Padri huyo.
Hilo ni tukio la tatu kwa viongozi wa dini kushambuliwa
visiwani Zanzibar, ambapo katika tukio la kwanza Katibu wa Mufti wa Zanzibar,
Sheikh Suleiman Soraga alishambuliwa kwa kumwagiwa tindi kali mwezi Septemba
wakati akifanya mazoezi.
Habari hii imeandaliwa na
Khamis Amani, Husna Shehe na mwandishi wetu, DSM
No comments:
Post a Comment