Habari za Punde

Papa aagwa



VATICAN, Italia
 MAELFU  ya watu walikusanyika katika uwanja wa kanisa la mtakatifu Petro jana kuhudhuria tukio la mwisho la Papa Benedict wa XVI la kuwaombea waumini hadharani.

Hiyo ilikuwa ibada ya mwisho ya Papa kabla ya kuachia kabisa nafasi hiyo ya kuliongoza kanisa katoliki duniani.

Kimsingi misa hiyo ya mchana ya Jumapili huwavutia watu wachache ikiwa ni pamoja na watalii lakini mara hii wamejitokeza maelfu kwa maelfu ya waumini katika uwanja huo kumshuhudia kwa mara yao ya mwisho Papa Benedict.

Inasaidikiwa kwamba watu 150,000 walihudhuria misa hiyo ya wazi katika uwanja wa mtakatifu Petro.

Baadhi ya watalii walisikika wakisema kwamba wamefika katika uwanja huo kumuaga na kumtakia mema na zaidi ya yote, mtalii kama Amy Champion aliyetokea Uingereza alisema inahitaji ujasiri kufanya kazi ya Papa na vile vile wakati unapoamua kuachia ngazi.


Kuanzia Jumapili jioni Papa  hatoweza kuonekana tena mbele ya hadhara katika kipindi cha wiki nzima, ambacho kanisa mjini Vatican linaanza kipindi maalum cha maombi na tafakari.

Jumapili ya jana uongozi wa mji wa Roma uliongeza usafiri wa mabasi na treni za chini kwa chini ili kusaidia kukabiliana na msongamano wa watu waliokuwa wanamiminika kuelekea Vatican pamoja na kutoa usafiri bure wa mabasi madogo kwa ajili ya watu wakongwe na walemavu.

Papa  Benedict aliushtua ulimwengu wiki iliyopita kwa kutangaza anajiuzulu kuanzia Februari 28, kitendo ambacho hakijawahi kushuhudiwa na kanisa hilo kwa kipindi cha miaka 600.

Wakati Makadinali wakitazamiwa kumchagua mrithi wake mpya katika kikao maalum cha siri,  Papa Benedict mwenye umri wa miaka 85 atakuwa katika mapumziko na kufanya ibada katika makazi ya kanisa huko Kusini mashariki mwa mji wa Roma.

Baada ya wiki kadhaa anatazamiwa kuhamia kwenye makaazi mengine yaliyoko kwenye eneo la Vatican ambako ataishi maisha ya kitawa.

Makao makuu ya kanisa  Katoliki mjini Vatican hayajatangaza tarehe ya kuanza kwa kiao cha siri cha kumchagua kiongozi mpya lakini yametangaza kwamba kikao hicho huenda kikafanyika mapema kabla ya Machi 15 na tarehe hiyo mpya inaweza kutangazwa chini sheria za sasa za kanisa.


Papa atahitajika kutia saini juu ya tarehe hiyo kitendo ambacho kitakamilisha kabisa kipindi chake cha takriban miaka 8 ya uongozi wa kanisa.

Wakati huohuo tayari Makadinali wameshaanza kuwasili Roma kuanza kipindi cha kujadiliana kwa mujibu wa sheria za kanisa kuamua ni kina nani walio wagombea wenye nafasi nzuri ya kuchukua wadhifa huo wa Papa.

Askofu Mkuu Robert Sarah mzaliwa wa Guinea, ambaye ni Kadinali anayeongoza ofisi ya misaada ya Vatican amewaambia waandishi wa habari kwamba viongozi wa kanisa watapaswa kumchagua Papa mpya kwa utulivu na kuaminiana.

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.