Habari za Punde

Wiki ya lala salama Kenya



Na Mwandishi maalum, Kenya
WAGOMBEA wa urais nchini Kenya wameingia katika wiki ya lala salama ya kampeni, huku kila mmoja akitangaza kuleta mageuzi makubwa katika sekta ya uchumi, ajira na viwanda nchini humo.
Ushindani mkubwa upo kati ya mgombea wa muungano wa CORD, Waziri Mkuu, Raila Odinga na mpinzani wake mkubwa, mgombea wa muungano wa Jublee, Naibu Waziri Mkuu, Uhuru Kenyatta.
Akiwa mjini Mombasa, Odinga aliwambia wafuasi wake kwamba ana kila sababu ya kushinda katika duru ya kwanza ya uchaguzi huo na kusema serikali yake itaimarisha huduma za elimu kwa kuhakikisha wanafunzi wote wanasoma bure hadi sekondari ya upili.

Aidha ameahidi kuimarisha sekta ya ajira, kuboresha uchumi wa Kenya, kuimarisha sekta ya kilimo na viwanda.
Odinga ambae anaungwa mkono na idadi kubwa ya vijana, alisema uchumi wa Kenya utajengwa upya katika kipindi cha miaka mitano cha serikali yake.
Kenyatta kwa upande wake, akiwa mjini Nyeri aliwahakikishia Wakenya maendeleo bora ya kiuchumi, kupunguza pengo la umaskini na kuboresha maisha ya wananchi.
Alisema serikali yake itatoa kipaumbele kwa vijana kujiajiri na kuajiriwa katika sekta za umma na binafsi pamoja na kupanua wigo wa uimarishaji viwanda.


Aliahidi kusimamia amani na umoja wa Wakenya na kusisitiza kuwa uchaguzi huo utafanyika kwa misingi amani na utulivu.

Kura ya hivi karibuni ya maoni inaonesha kuwa wapiga kura wenye umri wa zaidi ya miaka 51 wanampendelea zaidi Kenyatta kuliongoza taifa hilo lenye uchumi mkubwa Afrika Mashariki ilhali mwenzake wa Cord Raila Odinga anaungwa mkono zaidi na vijana.

Odinga na mgombea wake mwenza Kalonzo Musyoka wanaungwa mkono na asilimia 58 ya vijana wa umri wa kati ya miaka 18 na 20 akilinganishwa na Kenyatta na mgombea mwenza William Ruto wanaoungwa mkono na asilimia 32 ya vijana.

Kijinsia, kura tofauti ya maoni iliyofanywa na kampuni ya Strategic Africa, ambayo pia utafiti wake ulidhaminiwa na kampuni ya Nation Media Group inaonyesha vyama vya Restore and Build Kenya (RBK) na Narc Kenya vinaungwa mkono zaidi na wanawake kwa asilimia 62 na 60.

Nao wanaume wengi zaidi wanaunga mkono muungano wa Eagle, asilimia 61.4 ukifuatwa na Cord (60.5), Amani (57.9) na hatimaye Jubilee (57.2).

Pia inaonekana Profesa James Ole Kiyiapi wa RBK anaungwa mkono na wanawake wengi zaidi kwa asilimia 85.7 dhidi ya asilimia 14.3 ya wanaume.

Wakati huo huo mgombea urais wa muungano wa Cord, Raila Odinga, amelalamika kwamba baadhi ya familia katika Kaunti ya Nakuru zimetishiwa kuondoka eneo hilo kabla ya uchaguzi mkuu wa Machi 4.

Aliwaonya wanaotoa vitisho na kuziambia familia hizo kutohama.

 “Usiache nyumba yako ukipokea vitisho vya aina hiyo. Serikali itakulinda,” alisema Odinga akihutubia mkutano wa kampeni katika uwanja wa Afraha, mjini Nakuru.

Lakini Mkuu wa Mkoa wa  Rift Valley, Osman Warfa, alisema hakuna aliyetishwa kuhama, huku akisema baadhi ya wafanyakazi wa mashamba ya maua katika eneo la Naivasha walikuwa wakielekea walikojiandikisha kupiga kura ili kushiriki uchaguzi huo.

 “Wanaenda walikojisajili kupiga kura na ndio maana wanaondoka,” alisema Warfa.

Mwenyekiti wa Ford Kenya  Moses Wetang’ula alikuwa wa kwanza kudai baadhi ya watu walitishwa kuhama Nakuru.

“Kuna watu wanaotisha wengine kwamba watafurushwa makwao wakisema maisha yao yamo hatarini. Wanawaambia wahame Nakuru,” alisema.

Warfa aliwaonya wanasiasa dhidi ya kujadili jambo hilo wakati huu kwa sababu mkoa huo wakati wa uchaguzi mkuu hukumbwa na ghasia.

Mkuu wa mkoa aliongeza kwamba kamati za usalama za wilaya zinajadili jambo hilo.

Katika mkutano huo wa kampeni Odinga aliahidi kutatua matatizo ya ardhi akichaguliwa kuwa rais.

Alisema inasikitisha kuona watu waliofurushwa makwao kwenye ghasia za baada ya uchaguzi wa 2007 wanahangaika katika kambi za wakimbizi ilhali  baadhi ya viongozi wa Muungano wa Jubilee wana zaidi ekari 500,000 za ardhi.

Mgombea mwenza wa Odinga, Kalonzo Musyoka alisema serikali ya Cord itahakikisha masomo bila malipoi kuanzia shule ya chekechea hadi upili.

Wakati huo huo jana wagombea hao walishiriki katika mjadala wa mwisho ambao uligusia masuala matatu muhimu ya uchumi, rasilimali na usimamizi wa rasilimali,sera za ushirikiano na mataifa ya kigeni.

Kuna hofu kwamba huenda upigaji kura ukachelewa kukamilika kwa wakati kwa sababu wapiga kura wengi hawajaelewa utaratibu utakaotumika uchaguzini na watahitaji dakika tano kila mmoja kufanya hivyo.

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.