Habari za Punde

Ponda afungwa kifungo cha nje

 Na Kunze Mswanyama, DSM
MAHAKAMA ya Hakimu Mkazi Kisutu, imemwachia huru kwa masharti Katibu wa Taasisi na Jumuiya za Kiislam, Sheikh Issa Ponda Issa na wenzake 49, baada ya kumtia hatiani kwa kosa la kuingia kijinai katika eneo la ardhi linalodaiwa kumilikiwa na Kampuni ya Agritanza Limited.
Ponda na wenzake 49 walikuwa wanakabiliwa na mashtaka ya kula njama, wizi wa mali yenye thamani ya shilingi milioni 59.6 , uchochezi na kuingia kwa jinai katika ardhi inayomilikiwa na kampuni ya Agritanza Ltd na kujimilikisha isivyo halali.
Wakati Ponda akitiwa hatiani na kuachiwa kwa masharti ya kutokutenda kosa lolote katika kipindi cha mwaka mmoja, washatakiwa wenzake, wote 49 waliachiwa huru bila masharti baada ya mahakama  hiyo uwaona  hawana hatia kwa mashtaka hayo yaliyokuwa yakiwakabili.


Mahakama iliwaachia huru  baada ya kuridhika kuwa upande wa mashtaka umeshindwa kuthibitisha mashtaka yaliyokuwa yakiwakabili.
 
Hakimu Mkazi wa mahakama hiyo, Viktoria Nongwa aliyekuwa akisikiliza kesi hiyo, pia alimtaka Ponda awe ni kiongozi wa kutunza amani katika jamii  na asijichukulie sheria mkononi.
Hakimu Nongwa alisema kwa kuwa mshtakiwa amekaa rumande kwa muda mrefu baada ya Mkurugenzi wa Mashtaka (DPP) kuzuia dhamana yake ni haki kuangalia muda huo.
“Hivyo mahakama chini ya kifungu cha kifungu cha 25(g) cha kanuni za adhabu, mshtakiwa unaachiwa kwa masharti ya kutokutenda kosa kwa miezi 12, unatakiwa ulinde amani na kuwa na tabia njema katika jamii. Ukishindwa hiyo utarudi hapa kwa adhabu nyingine inayokufaa,” alisema.
Awali Hakimu Nongwa alichambua ushahidi wa mashahidi wote 16 wa upande wa mashtaka na ushahidi wa mashahidi 53 wa utetezi akasema upande wa mashtaka umeshindwa kuthibitisha mashtaka dhidi ya washtakiwa hao.
Alifafanua kuwa upande wa mashtaka umeshindwa kuthibitisha  katika kosa la kwanza, la tatu na nne, yaliyokuwa yanawakabili washtakiwa wote na katika shtaka la tano lilolikuwa likimkabili Ponda na mshtakiwa wa tano, Mukadamu Swalehe, ambaye ni kiongozi wa taasisi na jumuiya za kiislam.
Katika shtaka la pili, Hakimu Nongwa alisema upande wa mashtaka umeweza kuthibitisha shtaka dhidi ya mshtakiwa wa kwanza tu, Ponda na kwamba kwa upande wa washtakiwa wengine umeshindwa kuthibitisha mashtaka dhidi yao.
Alisema hakuna ushahidi unaoonesha ni jinsi gani washtakiwa hao walivyohusika katika  kosa hilo na kwamba hata kwa upande wa mshtakiwa wa tano japo kuna maelezo ya onyo yanayoonesha kuwa alikiri, lakini akasema maelezo ya onyo tu ya mshtakiwa hayatoshi kumtia hatiani ni lazima upande wa mashtaka utoe ushahidi zaidi.
Alisema upelelezi hakukufanyika kwa umakini kiasi kwamba kuna mambo ambayo hayakuwa wazi yaliyoibuliwa na upande wa utetezi, ambayo kama upelelezi ungefanyika kwa umakini basi washtakiwa wote wangetiwa hatiani.
“Katika kesi hii ni dhahiri upelelezi haukuwa mzuri kwani kuna mambo mengi yaliyoibuliwa na upande wa utetezi ambayo kama upelelezi ungefanyika vizuri, washtakiwa wote wangetiwa hatiani,” alisema Hakimu.
Pia aliionya Jamhuri kujiepusha na mashtaka ya kula njama ambayo hata yenyewe inajua kuwa ni vigumu kuyathibitisha na kuishauri iwe inajikita katika mashtaka yanayoweza kuthibitika kwa urahisi.
Ponda na wenzake walipandishwa kizimbani kwa mara ya kwanza Oktoba 18, 2012 na kusomewa mashtaka manne wote kwa pamoja, huku yeye akikabiliwa na kosa lingine zaidi pekee yake.
Mashtaka hayo ya pamoja ni kula njama, kuingia kwa jinai katika eneo la ardhi, kulikalia kwa nguvu eneo hilo, na wizi wa vifaa vya ujenzi mali ya kampuni ya Agritanza.
Shtaka la ziada kwa Ponda lilikuwa ni kushawishi  kutenda kosa.

 

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.