Habari za Punde

Pinda akiri urasimu sekta ya uwekezaji.

Na Kija Elias,Tanga
WAZIRI Mkuu, Mizengo Pinda amekiri kuwepo urasimu katika uwekezaji nchini tatizo ambalo linahitaji juhudi za pamoja kuliondoa.

Hayo aliyasema wakati akichangia mada katika kongamano la kwanza la uwekezaji kanda ya kaskazini linalofanyika jijini Tanga.

Alisema wapo baadhi ya viongozi wa serikali wamekuwa na urasimu pale mwekezaji anapotaka kuwekeza hali ambayo inawakatisha tamaa wawekezaji wengi.

Pinda alisema suala la urasimu katika uwekezaji bado ni changamoto kubwa inayoikabili sekta hiyo, ambpo aliwatka viongozi wanaohusika na sekta hiyo kuacha tabia ya kupokea rushwa ili kuwasaidia wawekezaji.

Alisema viongozi watakaobainika kupokea rushwa watachukuliwa hatua kali za kisheria ili kukomesha tatizo.

Hata hivyo, alisema kumekuwepo na majukumu makubwa katika vituo vya uwekezaji, hivyo wanahitaji kugawa madaraka kuanzia ngazi za wilaya na mkoa ili kupunguza urasimu.

Mbunge wa jimbo la Kilindi, Beatrice Shelukindo, alisema suala la urasimu katika kupata maeneo ya uwekezaji bado ni tatizo kubwa kwa wawekezaji.

Aidha alisema kutokana na tatizo hilo atapeleka hoja binafsi bungeni ili ijadiliwe na hatimaye kupelekwa kwa wananchi.

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.