Habari za Punde

Dk Shein aongoza viongozi na wananchi katika mazishi ya Kanal Abuu Amour Juma

Na Said Ameir, Ikulu
Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Ali Mohamed Shein leo amejumuika na viongozi wengine wa kitaifa pamoja na wananchi katika mazishi ya Kanali Mstaafu Abuu Amour Juma aliyefariki jana huko katika hospitali ya jeshi Lugalo jijini Dar es Salaam.

Mazishi ya Kanali Abuu ambaye ni kaka wa Rais Mstaafu wa Awamu ya Tano Dk. Salmin Amour yalifanyika huko kijijini kwake Kidombo, wilaya ya Kaskazini ‘A’, Mkoa wa Kaskazini Unguja ambako ndiko alikozaliwa mnamo mwaka 1940.

Miongoni mwa Viongozi waliohudhuria mazishi hayo ni pamoja na Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dk. Mohamed Gharib Bilal, Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Balozi Seif Ali Iddi, Rais Mstaafu Ali Hassan Mwinyi, Kaka wa marehemu Rais Mstaafu wa Zanzibar Awamu ya Tano Dk. Salmin Amour, Spika wa Baraza la Wawakilishi Pandu Ameir Kificho, Mufti Mkuu Sheikh Saleh Omar Kabi na viongiozi wengine wa Serikali.  

Kwa mujibu wa wasifu wa marehemu uliosomwa na Mkuu wa Mafunzo na Utendaji Kivita Brigedi ya Zanzibar Kanali Shaaban Lissu marehemu alijiunga na Jeshi tarehe 28 Januari 1966 na ilipofika mwezi Juni mwaka huo alipata cheo cha Luteni Ussu na mwezi Oktoba mwaka huo huo alipandishwa cheo kuwa Luteni.

Mwaka 1970 marehemu alipandishwa cheo kuwa Kepteni na mwaka 1974 alipanda cheo hadi kuwa Meja, mwaka 1979 alipandishwa cheo cha Luteni Kanali na mwaka 1984 alipanda cheo hadi kuwa Kanali.  

Katika utumishi wake jeshini marehemu alishika nyadhifa mbalimbali na vilevile alitunukiwa medali mbalimbali kama medali ya Vita vya Kagera, medali ya miaka 20 ya Jeshi la Wananchi wa Tanzania (JWTZ), medali ya utumushi mrefu ,medali ya Uhuru na medali ya Muungano.


Marehemu Kanali Abuu Amour Juma ameacha mke na watoto 9. Mungu ailaze roho ya marehemu peponi- Amin.

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.