Habari za Punde

Balozi Seif azindua vyoo vya Skuli za kijitoupele

 Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Balozi Seif Ali Iddi akivizindua rasmi vyoo vya Skuli ya Kijitoupele A, B na Sekondari pamoja na Mifereji na Tangi la Maji vilivyojengwa na ufadhili ya Shirika la Umoja wa Mtaifa la Kuhudumia Watoto { UNECEF }.
 Mifereji Maalum iliyozunguukwa na wanafunzi kwenye sherehe ya kuzinduliwa rasmi ambayo imejengwa kwa ajili ya kuhudumia wanafunzi wa Skuli ya Kijitoupele A,B na Sekondari
 Moja kati ya madarasa ya skuli ya msingi ya Kijitoupele yanaonekana kuwa na msongamano mkubwa wa wanafunzi wasiopunguwa idadi ya 240.


Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Balozi Seif akibadilishana mawazo na Mwenyekiti wa Kamati ya Skuli ya Kijitoupele Nd. Manafi Said Mwinyi mara baada ya hafla ya kuzinduliwa kwa vyoo vya skuli hiyo.
Kushoto ya Nd. Manafi ni Waziri wa Elimu na Mafunzo ya Amali Mh. Ali Juma Shamhuna nanyuma yao ni Katibu Mkuu wa Wizara hiyo Bibi Mwanaid Saleh

Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Balozi Seif akimpongeza mwakilishi wa UNICEF hapa Zanzibar Bibi Francesca Morandini kwa uamuzi wa shirika lake kusaidia ufadhili wa ujenzi wa vyoo vya skuli ya Kijitoupele iliyopo Wilaya ya Magharibi.


Nyuma ya Bibi Francesca ni Naibu Katibu Mkuu Wizara ya Elimu na Mafunzo ya Amali Nd. Abdulla Mzee Abdulla.


Picha na Hassan Issa wa – OMPR – ZNZ.
 
Na Othman Khamis Ame OMPR
 
Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Balozi Seif Ali Iddi alisema kwamba misingi ya ufundishaji wanafunzi Maskulini itaendelea kukosekana iwapo idadi kubwa ya Wanafunzi  itapindukia kiwango kilichowekwa Kitaifa au Kimataifa.
 
Alisema idadi ya kawaida ya wanafunzi ndani ya darasa moja
inahitajika kuwa    watoto wasiozidi arubaini wakiwa na vikalio pamoja na vifaa vyote wanavyohitajika kuwa navyo wanafunzi hao darasani.
 
Balozi Seif alisema hayo mara baada ya kukabidhiwa na kuvizindua rasmi vyoo 18 vya Skuli za Kijitoupele  za Msingi A na B  pamoja na ile ya Sekondari hafla iliyofanyika katika Skuli  hiyo na kuhudhuriwa na Wanafunzi, Walimu pamoja na Wazazi wa Wanafunzi wa Skuli hizo.
 
Balozi seif alisema msongamano wa watoto wengi Darasani mbali ya kwenda kinyume na mfumo, taratibu na maadili ya ufundishaji ndani ya darasa lakini pia unabebesha mzigo mkubwa walimu  kuweza kuhudumia wanafunzi hao kwa wakati mmoja.
 
Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Balozi Seif aliupongeza Uongozi wa Kamati ya Skuli ya Kijitoupele kwa uamuzi wao wa kukubali Wanafunzi wao kuhamishwa kwenda kupata taaluma skuli nyengine  ili kupunguza msongamano mkubwa wa wanafunzi ndani ya Skuli hizo.

 
“ Walimu wetu wamekuwa wakiendelea kupata mzigo mkubwa  kuwasomesha watoto wetu kutokana na wingi wa idadi yao darasani. Inasikitisha sana kuona Darasa moja la Skuli hii lina wastani wa wanafunzi 240 jambo ambalo pia ni hatari kwa afya ya wanafunzi wenyewe “. Alifafanua Balozi Seif.
 
Alisema katika kukabiliana na tatizo hilo Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar itajitahidi kuangalia maeneo mengine ya wazi ndani ya Wilaya ya Magharibi ili kutoa fursa ya ujenzi wa Skuli nyengine Mpya  zitakazosaidia kukidhi mahitaji ya wanafunzi  wa maeneo hayo.
 
Balozi Seif aliwasihi Wanafunzi hao kuendelea kuvitunza vyema vyoo hivyo ili vidumu kwa muda mrefu pamoja na kuwakumbusha kupenda masomo yao  kwa lengo la kushika nafasi za Uongozi na Taaluma kwa Taifa hili hapo baadaye.
 
“ Nawajibu wa kuwapongeza Walimu na Kamati ya Wazazi wa Skuli hii kwa juhudi zao za usimamizi mzuri wa wanafunzi wao na kupelekea kutoa wanafunzi wengi wanaofaulu vizuri kuingia katika skuli mbali mbali za Michepuo hapa Nchini “.
 
Akisoma Risala kwa niaba ya Wanafunzi, Walimu na Wazazi wa Skuli hizo Mwalimu Hidaya Haji Mkema alilipongeza Shirika la Kuhudumia Watoto la Umoja wa Mataifa { UNICEF } kwa msaada wa vyoo hivyo ambavyo lilikuwa na uwezo wa kuvijenga Skuli nyengine.
 
Mwalimu Hidaya alisema Skuli za Kijitoupele bado zinakabiliwa na msongamano mkubwa wa wanafunzi changamoto ambayo iko katika hatua ya kutafutiwa ufumbuzi wake  ifikapo mwaka 2015.
 
Alisema uandikishaji wa wanafunzi wapya katika skuli hizo za Kijitoupele A na B umefikia idadi ya watoto 800 kwa mwaka kiasi ambacho ni kikubwa kupindukia mfumo na utaratibu uliowekwa wa sera ya Elimu.
 
Akitoa salamu za Shirika la Umoja wa Mataifa la kuhudumia Watoto { UNICEF } Mwakilishi wa Shirika hilo hapa Zanzibar Bibi Francesca Morandini alisema watoto wana haki ya msingi ya kupata elimu inayoambatana na usafi wa mazingira.
 
Bibi Francesca alisema utafiti uliofanywa miaka mitatu iliyopita na Serikali ya Jamuhuri ya Muungano wa Tanzania kwa kushirikiana na Benki ya Dunia katika suala la huduma za usafi wa mazingira  maskulini umethibitisha hasara ya zaidi ya shilingi Bilioni 300 kwa mwaka.
 
Mwakilishi huyo wa Shirika la kuhudumia Watoto la Umoja wa Mataifa hapa  Zanzibar alieleza kwamba Taasisi yake kwa kushirikiana na Wizara ya Elimu na Mafunzo ya Amali Zanzibar  tayari wameshatengeneza muongozo  wa ujenzi wa vyoo katika maskuli mbali mbali unguja na Pemba.
 
Alisema muongozo huo una lengo la kuwajengea mazingira rafiki wanafunzi na  tayari umeshazinufaisha skuli nane za Pemba naTano kwa Unguja wakati awamu ijayo itahusisha skuli nyengine Sita hapa Zanzibar.
 
Naye kwa upande wake Katibu Mkuu Wizara ya Elimu na Mafunzo ya Amali Zanzibar { WEMA } Bibi Mwanaid Saleh alisema mradi huo uliohusisha Skuli 13 Unguja na Pemba kwa  ufadhili wa Unicef  umegharimu Shilingi za Kitanzania Milioni Mia Tatu na Ishirini na Tano { 325,000,000/- }.
 
Katibu Mkuu  Mwanaidi alizitaja Skuli zilizofaidika na mradi huo kuwa ni pamoja na Makombeni, Vitongoji, Wingwi,Kwale,Pujini, Mabatini na Konde kwa Pemba na Kijitoupele, Nyerere Msingi,Tunguu, Bububu na  Mtopepo kwa Unguja.
 
Akimkaribisha Balozi Seif katika hafla hiyo Waziri wa Elimu na Mafunzo ya Amali Zanzibar Mh. Ali Juma Shamhuna  alisema Madarasa 40 yanahitajika kujengwa ndani ya Wilaya ya Magharibi ili  kukidhi mahitaji yaliyopo ndani ya Wilaya hiyo.
 
Waziri Shamhuna alifafanua kwamba upo mradi maalum wa ujenzi wa Skuli kumi za Sekondari  katika Wilaya zote za  Zanzibar  mradi ambao utatoa upendeleo wa kwanza kwa wilaya ya Magharibi ili kukabiliana na tatizo la msongamano wa wanafunzi katika Skuli za Wilaya hiyo.
 

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.