HALI YA KISIASA YA MUUNGANO WA TANZANIA: TULIKOTOKA, TULIPO
NA TUENDAKO
MHADHIRI IDARA YA
SIASA NA UTAWALA, CHUO KIKUU DAR ES SALAAM
19 APRILI, 2014
ZANZIBAR
- UTANGULIZI
Miaka hamsini ya Muungano ni safari ndefu iliyopitia na
kushuhudia maendeleo, mageuzi, misukosuko na changamoto kadhaa za kisiasa,
kiuchumi, kijamii, kiteknolojia nakadhalika. Tathmini iliyokamilika kuhusu
Muungano ulipotoka, ulipo na unapokwenda ni ile inayotazama maeneo yote hayo
kwa undani, yaani kisiasa, kiuchumi, kijamii na kiteknolojia. Mada hii lakini
imejikita katika eneo moja tu la kisiasa. Bado neno kisiasa linabeba dhana pana ambayo inaweza kujumuisha masuala yenye
sura za mifumo ya kiuchumi, kijamii na kiteknolojia. Hivyo ipo haja ya kutoa
ufafanuzi kuhusu dhana ya ‘Hali ya Kisiasa ya Muungano’ tunayomaanisha. Hali ya
Kisiasa hapa itamaanisha masuala yafuatayo- muktadha wa kisiasa kabla na baada
ya muungano kufikiwa; harakati za kisiasa zilizopelekea kuundwa kwa muungano;
maendeleo, mafanikio, mageuzi, misukosuko na changamoto za mfumo wa kisiasa
tangu kuzaliwa kwa muungano mpaka leo hii unapotimiza miaka hamsini.
Mfululizo wa mada hii upo katika sehemu kuu sita. Kufuatia
utangulizi huu sehemu ya pili inatazama kipindi cha harakati za kuondokana na
ukoloni mpaka uwepo wa nchi ya Tanzania. Sehemu ya tatu inaangalia safari ya
muungano toka 1964 mpaka 1984 iliposemekana hali ya kisiasa ilichafuka visiwani
Zanzibar. Matukio ya kipindi kigumu kisiasa kwa uongozi wa juu wa nchi yalijitokeza
tena mwanzoni mwa miaka ya tisini kulipojitokeza kundi la G55. Sehemu ya nne
inamulika matukio hayo na mengine muhimu ya kisiasa. Sehemu ya tano inaangaza
matukio baada ya vuguvugu la G55 mpaka mjadala wa sasa wa katiba mpya.
Hitimisho la mada linahusu mustakabali wa muungano wenyewe kwa kizazi hiki na
kijacho.
- KABLA
YA 1964: Harakati za Kujikomboa na Kuondokana na Ukoloni mpaka Kuwepo
Tanzania
Jambo lingine muhimu kulizungumza japo kwa muhtasari ni kwamba vuguvugu la
harakati za kujikomboa na kuondokana na minyororo ya ukoloni kwa pande zote
mbili ilishika kasi miaka ya 1950. Kipindi hiki kilishuhudia wanaharakati
mashuhuri wa pande hizi mbili wakikutana visiwani Zanzibar na kwingineko Afrika
kwa lengo kuu moja la wakati huo-ukombozi wa jamii zao. Itakumbukwa kwamba hata
kabla ya mahusiano ya vyama vya Afro Shirazi Party (ASP) na Tanganyika African National
Union (TANU) hayajafanywa rasmi baadae miaka ya 1960, viongozi wanaharakati
walipata fursa ya kukutana katika mikusanyiko kama ya PAFMECA (Pan-African
Movement for East and Central Africa) iliyofanyika sehemu tofauti za Afrika
mashariki na kati. Kwa mfano mkutano wa PAFMECA uliofanyika Mwanza mwaka
1958 ulihudhuriwa wanasiasa mashuhuri
wakiwemo kutoka visiwani Zanzibar[2]. Mkutano wa
pili wa PAFMECA ulifanyika Zanzibar
April 1959 na msisitizo uliendelea kushawishi vyama vya ASP na ZNP
kuunganisha nguvu na juhudi hizi zilichangia kuanzishwa Kamati ya Ukombozi
(Freedom Committee) japo haikudumu kwa muda mrefu[3].
Pilika zilizopelekea kujipatikana
uhuru wa Tanganyika mnamo Disemba ya 1961; harakati, mbinu za kujiongezea
ufuasi katika chaguzi; giliba za kisiasa wakati wa Zama za Siasa Zanzibar, na hatimaye Mapinduzi ya 1964 visiwani
yameelezwa kwa mitazamo tofuati katika makala kadhaa. Si nia ya mada hii
kurudia kwa ukamilifu masimulizi ya matukio yaliyotufikisha kwenye uhuru wa
Tanganyika wa 1961 na mapinduzi ya Zanzibar ya 1964. Ifahamike kwa ufupi tu
kwamba yale mawasiliano ya viongozi wa vyama ya TANU na ASP yaliendelea pia
baada ya mapinduzi na kupelekea kuungana 1964. Sehemu inayofuata inatazama
lengo la kuungana na mengine yaliyojitokeza katika miongo miwili ya kwanza ya
Muungano (yaani 1964-1984).
- 1964-1984:
Sherehe za Kuchanganya Udongo wa Nchi Mbili mpaka ‘Kuchafuka kwa Hali ya
Kisiasa Visiwani’
Kama ilivyobainishwa hapo awali mara tu baada ya Mapinduzi ya Zanzibar ya
tarehe 12 Januari 1964, viongozi wa
Tanganyika na Zanzibar, Mwalimu Julius K. Nyerere na Sheikh Abeid A.
Karume walianza mazungumzo yaliyolenga kuziunganisha nchi hizo mbili. Mbali na
kutetea au kukosoa namna mazungumzo ya viongozi hawa yalivyoendeshwa,
kumbukumbu za kihistoria zinatuonyesha mazungumzo yao yaliendeshwa kwa faragha
kutokana na unyeti wa suala lenyewe na mazingira ya wakati huo ya vita baridi.
Hatimaye Mwalimu Nyerere na Sheikh Karume walifikia makubaliano ya
kuziunganisha nchi zao na kuamua kusaini Mkataba wa Muungano kati ya Jamhuri
ya Tanganyika na Jamhuri ya Watu wa Zanzibar (The Articles of the Union between the
Republic of Tanganyika and the People’s Republic of Zanzibar) (utaitwa “Mkataba wa Muungano”).
Mkataba wa Muungano ulitiwa saini huko Zanzibar tarehe 22 Aprili 1964. Sherehe
rasmi za Muungano zilifanyika mnamo tarehe 26 Aprili 1964, moja ya matukio
ikiwa ni kuchanganywa kwa udongo ikiashiria kuungana kwa nchi mbili.
Makala nyingine za wachambuzi na wasomi, zimejaribu kuchambua malengo
halisi ya vinara hawa wawili wa muungano. Kama kweli walifanya maamuzi kwa
msukumo ama wa kiusalama wa ndani au wa nje, ama miskumo wa kiumajumui wa
Afrika ama vyote kwa nafasi na viwango tofauti, bado ni mjadala unaoendelea. Tunaweza
kuafiki kwamba kumekuwa na uthubutu wa wasomi zama hizi kubainisha katika
maandiko yao kauli zilizoonyesha hisia za wakati huo, hususan baada ya waasisi
hawa kuondoka duniani. Kauli kama “Koti likikubana livue”[4]
inayodaiwa kutolewa na Mzee Karume; “If I could tow that island out into the
middle of the Indian Ocean, I’d do it”[5]
iliyodaiwa kutolewa na Mwalimu Nyerere, zimekuwa zikirudiwa haswa katika miongo
miwili iliyopita. Lakini madhumuni ya kuungana yaliwekwa wazi kwenye utangulizi
wa Mkataba wa Muungano kama ifuatavyo:
Whereas the
Governments of the Republic of Tanganyika and of the People's Republic of
Zanzibar, being mindful of the long association of the peoples of these lands
and of their tics of kinship and amity, and being desirous of furthering that
association and strengthening these tics and of furthering the unity of African
peoples, have met and considered the union of the Republic of Tanganyika with
the People's Republic of Zanzibar[6].
Kwa ufupi, sababu
kubwa mbili za kuungana kwa mujibu na utangulizi huo ni ushirikiano wa muda
mrefu wa kirafiki na udugu miongoni mwa watu wa nchi hizo mbili, na pia nia ya
kutaka kuuendeleza uhusiano huo na kuzidisha umoja wa Kiafrika.
Katika kipindi cha miongo miwili ya kwanza tangu
mkataba wa muungano kusainiwa mambo
mengi yaliyogusa uendeshaji wa muungano wa Tanzania yalitokea. Kisiasa nchi
ilipitia mabadiliko ya kikatiba kutoka katiba ya muda ya 1965 iliyodumu mpaka
1977, kuuwawa kwa Sheikh Abeid Amani Karume (April 7 1972), pamoja na kuungana
kwa vyama vya ASP na TANU na kuunda chama kimoja, Chama cha Mapinduzi
(CCM). Kipindi hichi cha chama kushika
hatamu kilishuhudia kuanza kwa zoezi la kuongeza mambo ya Muungano baada ya
jumuiya ya Afrika Mashariki kuvunjwa. Rais wa Zanzibar wakati huo Aboud Jumbe
alianzisha mchakato wa katiba ya Zanzibar (Katiba ya Zanzibar ya 1979).
Hiki pia ni kipindi ambapo muungano ulipata mtihani
wake mkubwa: ni dhahiri kulijitokeza dalili
za kutoridhika na muundo wa muungano hasusan kwa upande wa visiwani. Hii
ilitafsiriwa na uongozi wa juu wa chama tawala wakati huo kama ‘kuchafuka kwa
hali ya kisiasa visiwani’[7]. Kwa
sasa tunafaida ya kuangalia matukio ya wakati ule kwa utambuzi baada ya jambo
kutokea (with hindsight). Kwa wakati ule dai la tafsiri ya mkataba wa muungano
kama je lilidhamiria serikali mbili au tatu lilichukuliwa kama tukio la
‘kiuhaini’[8]. Mwanazuoni
maarufu nchini, Issa Shivji anasema uongozi wa chama tawala chini ya Mwalimu
Nyerere, ulipoteza fursa adimu ya kushughulikia kidemokrasia ujumbe wa utaifa uliojitokeza
wakati ule na badala yake ‘mjumbe alifukuzwa’[9]. Matukio
yalihitimishwa na mkutano maalum wa halmashauri kuu ya CCM liyojadili kuchafuka
kwa hali ya kisiasa na mwishowe Aboud Jumbe alijiuzulu nyadhifa zote. Kilikuwa
ni kipindi cha taharuki. Kusema ukweli, siasa zimebadilika leo hii wanasiasa
wanalizungumza suala la muundo wa muungano hadharani kwenye mikutano ya
hadhara, na kwenye bunge wakirekodiwa na vyombo vya habari. Bado lakini suala la
muundo linazungumzwa zaidi kwa mtindo wa ushabiki wa kivyama. Tutalirejea suala
hili sehemu ya tano ya mada hii.
- 1985-1993:
Baada ya ‘Kuchafuka Hali ya Kisiasa’ mpaka Kundi la 55
Baada ya hali tete ya 1983-84 kudhibitiwa chama tawala kiliona umuhimu wa
kuweka jitihada rasmi za kushughulikia matatizo na madai mbalimbali, kwa mfano
kwamba Zanzibar inaburuzwa katika kufikia maamuzi yanayohusu Muungano na kwamba
haipati haki sawa kiuchumi[10]. Miongoni mwa
jitihada hizo ni Tume ya Chama cha Mapinduzi ikiongozwa na Dk. Salmin Amour
iliundwa 1984. Pia Tume ya Rais ya Mapato na Matumizi ya Serikali ya Jamhuri ya
Muungano wa Tanzania ya mwaka 1991 iliyoongozwa na Edwin Mtei iliundwa. Kamati
zingine zilizoundwa ni Kamati ya Baraza la Mapinduzi (Kamati ya Amina Salim
Ali- 1992) na Kamati ya Shelukindo (1994).
Kujiuzulu kwa Mzee Jumbe na kurejea kwa hali ya utulivu visiwani
hakukumaanisha hoja ya kubadili muundo wa muungano ilipotea kabisa. Hoja hii
iliibuka tena pale Tume ya Nyalali ilipopendekeza muundo wa shirikisho la
serikali tatu. Si nia ya makala hii kurejea namna pendekezo hilo lilivyofikiwa
na maoni na hoja yaliyokusanywa tume hiyo. Malalamiko ya upande wa Tanzania
bara, kama yalikuwa sio dhahiri basi yaliwekwa bayana na kundi la wabunge 55
lililojulikana kama ‘G55’ ambalo mwaka 1993 lilitoa hoja bungeni ya kuundwa
serikali ya Tanganyika. Hii ilikuwa baada ya taarifa za Zanzibar kujiunga na umoja wa OIC
(Organization of Islamic Conference). Mwalimu kama mmoja wa waasisi wa muungano
alitafuta wasaa wakuzungumza na wabunge hao akivaa kofia ya ‘Mkulima toka
Butiama’[11].
Pamoja na kufanikiwa kuwasilishwa bungeni baada ya marekebisho kadhaa bado hoja
ya kundi hili ilizimwa. Je kuzimwa kwa hoja ya G55 kulileta athari gani katika
jitihada za kushughulikia malalamiko kuhusu muungano? Swali hili linajibiwa sehemu
inayofuata.
- 1994-2014:
Baada ya Vuguvugu la G55 mpaka Mjadala wa Katiba Mpya
Wakati vuguvugu la G55 linaibuka na kufifia, Jamhuri ya Muungano ilikwishwa
ingia rasmi katika mfumo wa siasa za vyama vingi hapo mwaka 1992. Pamoja na
kufungua uwanja kwa ushiriki wa siasa za ushindani na kuongeza uhuru wa kutoa
maoni, kurejea kwa mfumo huu kuliambatana na mabadiliko, mafanikio na
changamoto kadhaa kwa utawala wa nchi na hivyo muungano, vyama vya siasa,
wanasiasa, wananchi na wadau wengine wa mfumo wa kisiasa nchini. Tunaweza
kuyaorodhesha baadhi kama ifuatavyo:
- Kushuka kwa kasi kwa uvumilivu wa kisiasa na matokeo ya
uvunjivu wa amani;
- Kushamiri kwa siasa za migawanyiko na viashiria vya
kuyumba kwa utengamano ndani ya mipaka ya Jamhuri ya Muungano;
- Kuongezeka jitahada
za kitaasisi kushughulikia ‘Kero za Muungano’;
- Ushiriki wa Zanzibar katika Jumuiya ya Afrika Mashariki;
- Mazungumzo yaliyopekea kufikiwa Miafaka Mitatu ya
Zanzibar.
Sasa tuangalia japo kwa ufupi baadhi ya masuala yaliorodheshwa hapo juu.
Moja ya misingi muhimu sana katika mfumo wowote wa kisiasa unaruhusu siasa za
ushindani ni uvumilivu wa kisiasa. Katika hotuba yake ya ufunguzi wa Mkutano wa
Hali ya Siasa Zanzibar uliofanyika tarehe 22 na 23 Desemba, 2009 mjini Zanzibar
uliokuwa na mada kuu ya “Ujenzi wa Uvumilivu wa Kisiasa Zanzibar: Zanzibar
Tuitakayo”, Rais wa Zanzibar, Amani Abeid Karume alitoa ufafanuzi kuhusu dhana
ya uvumilivu wa kisiasa kama ifuatavyo:
Kwa mtazamo wangu, uvumilivu wa kisiasa ndio msingi mkuu wa amani na
maendeleo ya taifa. Uvumilivu wa kisiasa unatokana na ukweli kwamba palipo na
wengi pia kuna mawazo tofauti. Tofauti ndio sifa kubwa inayowatambulisha
binadamu. Kila mmoja wetu huumbwa akiwa na haiba na hulka inayomfanya
atofautiane na mwenzake. Tofauti hizi za haiba na hulka huendena na tofauti za
mawazo na mitazamo. Tofauti za kila mmoja wetu ni muhimu katika kujenga
demokrasia. Tofauti hizi wengine huziita migogoro[12].
Karume anaendelea kufafanua kwamba “Yaliyotokea baada ya uchaguzi kwa
majirani zetu Kenya, au hata Zimbabwe, ilikuwa ni dalili za kufifia kwa
uvumilivu wa kisiasa”[13]. Ufafanuzi huu
uliojitosheleza unahusisha dhana ya uvumilivu wa kisiasa na mambo mawili muhimu
sana kwa mustakabali wa taifa: amani
na maendeleo. Ieleweke kwamba dalili
za kufifia kwa uvumilivu wa kisiasa kulikoendana na upanuzi wa ulingo wa
kisiasa kumejitokeza si tu nchi za jirani. Hata hapa kwetu siasa za vyama
vingi, mbali ya kuwa jukwaa murua la kuwakilisha na kushughulikia matakwa na
kero za wananchi, zimetumika vibaya pia na kupelekea matukio kadhaa ya uvunjivu
wa amani. Baadhi ya changuzi, bara na visiwani, zimeshudia matukio ya vurugu
kubwa kabisa. Matukio ya vurugu katika
siasa pia yameathiri maendeleo ya sehemu
husika kwa kuwa nguvu na akili zinaelekezwa katika kusuluhisha na kuondoa
vurugu badala ya kuelekezwa katika shughuli za maendeleo. Vurugu za kisiasa
zilizopelekea baadhi ya wananchi kukimbilia nchi jirani mwaka 2001 zilitia doa
taswira ya muungano wetu kama ‘kisiwa cha amani’ kwa jumuiya ya kimataifa.
Sambamba na kufifia uvumilivu wa kisiasa, siasa za migawanyiko zimeendelea
kushamiri. Tunapendelea kutumia dhana ya siasa
za migawanyiko kuliko dhana iliyotawala kauli za viongozi wa kiserekali na
kisiasa haswa katika mwongo uliopita,
yaani mpasuko wa kisiasa. Nimewahi
kuandika katika makala mengine kwamba si sahihi kutumia misimamo ya wapigaji
kura katika sanduku la kura kila uchaguzi unapofanyika kama kielelezo cha
mpasuko wa kisiasa. Nikitumia mfano wa Pemba nilieleza kwamba, “Kwa ujumla,
kuna mwelekeo wa kueleza uamuzi wa wapiga kura wa Pemba kupigia kura chama cha
upinzani kama kielelezo cha mpasuko wa kisiasa Zanzibar. Wakati mwelekeo huo
unatoa picha fulani ya hali ya sasa, lakini unaonekana kupuuza hoja kuwa wapiga
kura wa Pemba wameonyesha mtazamo wao dhidi ya mfumo wa siasa, wakionyesha
kutaka mabadiliko ya kisiasa. Pia, imeonekana kuwa jamii zimekuwa
zikishirikiana kwa amani, ikimaanisha kuwa uhasama wa kisiasa haujajikiita sana
kwenye masuala ya jamii kama ilivyo kwenye siasa”[14].
Kwa hivyo, dhana ya siasa za migawanyo inatufaa zaidi kwa kuwa ni pana
kiasi cha kujumuisha sio tu mizozo inayotokana na mitazamo tofauti ya wanasiasa
na wafuasi wao, bali pia migawanyiko inayotokana na usimamizi mbovu na/au wa
kiupendeleo wa sheria zilizopo hata kupelekea kuibua hisia za ubaguzi wa uraia.
Hili ni moja ya nyufa zilizojitokeza katika miaka ya hivi karibuni ya muungano
wetu. Kumeendelea kujitokeza mwenendo unaobidi ufuatiliwe kwa taadhari wa
kusisitiza utofauti wa utanzania na uzanzibari. Kisa alichowahi simulia
aliyekuwa Jaji Mkuu wa Tanzania, Augustino Ramadhani, kitatusaidia kufafanua
hili. Bila kumumunya maneno Jaji Ramadhani anaeleza:
Mimi ni Mzanzibari nimezaliwa Zanzibar, baba na mama wamezaliwa Zanzibar,
babu zangu na bibi zangu wa pande zote mbili wamezaliwa na kuzikwa Zanzibar.
Ninaambiwa kuwa kwa asili, baadhi ya hao waliotangulia walitoka Masasi. Lakini
simjui yeyote Masasi.
Niliteuliwa kuwa Makamu wa Mwenyekiti wa Tume ya Taifa ya Uchaguzi kwa
kuwa ni Mzanzibari. Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, 1977 imeweka
kuwa kama Mwenyekiti wa Tume anatoka upande mmoja wa Muungano basi Makamu atoke
upande mwingine. Mwenyekiti, Jaji Makame, anatoka Bara hivyo niliteuliwa kuwa
Makamu kwa kuwa mimi ni Mzanzibari.
Labda nielezee utata ambao unatusonga bila kujifahamu. Katika Uchaguzi
Mkuu wa mwaka 2005, mimi sikujiandikisha kupiga kura Zanzibar kwa kuogopa
hitajio la ukaazi wa miezi 36 kabla ya uchaguzi. Hivyo mimi nilijiandikisha Dar
es Salaam. Kwa bahati chaguzi za Bara na Zanzibar hazikufanyika siku moja, na
kwa kuwa nilikuwa Makamu Mwenyekiti wa Tume ya Zanzibar nilisimamia upigaji
kura Zanzibar. Baadaye niliweza kupiga kura Dar es Salaam. Vinginevyo,
ningekosa haki yangu ya msingi ya kupiga kura. Lakini si hivyo tu, Makamu
Mwenyekiti wa Tume ya Uchaguzi ya Zanzibar alihimiza wengine kujitokeza kupiga
kura, na alishiriki kuandaa mipango murua ya uchaguzi, lakini yeye mwenyewe
hakupiga kura Zanzibar!
Sasa kama kwetu Zanzibar ninabaguliwa na kuambiwa kuwa mimi ni Mzanzibara, niende wapi? Sisi sote wenye
asili ya bara na wale wenye asili ya Arabuni, tuliojikuta tumezaliwa Zanzibar,
na wale ambao ndio wenyeji asilia wa Visiwa hivi, sote tu Wazanzibari na tuna
haki sawa katika undeshaji wa Serikali[15].
Pamoja na ufafanuzi uliowahi kutolewa na Mwanasheria Mkuu wa Zanzibar, Idi
Pandu Hassan, kuhusu utofauti uliopo kati ya Mtanzania na Mzanzibari[16],
masimulizi ya Jaji Ramadhani yanatoa picha kwamba tunaweza kuwa na sheria kwa
nia nzuri lakini matatizo yakawa kwenye utekelezaji wake. Kwa mtazamo wake,
Makame Mahamud Khamis anaona sheria zinazokidhi haja zipo lakini watendaji
wengi huzitafsiri na kuzitekeleza kwa kuweka mbele utashi wao wa kisiasa zaidi[17].
Ni vyema kufahamu pia kwamba ni katika kipindi hiki (miongo miwili hii ya
mwisho) ‘kero’ nyingi za muungano zimerekodiwa lakini pia jitihada kadhaa
zimefanywa na Serikali ya Muungano kushughulikia kero hizo. Ni kwa kiasi gani kero
za muungano zimepatiwa ufumbuzi thabiti ni suala jingine lenye mjadala mzito.
Mwaka 1998 Serikali ilianzisha Sekretarieti ya Muungano kwa lengo la kuratibu
na kufuatilia utekelezaji wa masuala ya muungano na yasiyo ya muungano[18]. Katika
kipindi cha mwaka 2000-2010 pekee vikao vipatavyo 1000 vya ushirikiano
vimefanyika kujadili masuala ya kisekta ya kubadilishana uzoefu, ujuzi,
utaalamu, sera, mafunzo na ushiriki katika masuala ya kimataifa[19]. Ni kipindi
ambacho pia tume na kamati nyingi ziliundwa kwa minajili ya kushughulikia kero
za muungano kama baadhi ya tume na kamati hizo zilivyorodheswa kwenye jedwali
la kiambatisho A. Kipindi hiki pia Serikali ya Muungano imetoa mwongozo wa
namna ya kuishirikisha Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar katika masuala yote ya
kimataifa.
Tathmini ya jumla ni kwamba, kwanza, kamati na tume nyingi zimeundwa. Hii
ni ishara kwamba nia ya kushughulikia imekuwepo ingawa ni dhahiri vikao vya
tume na kamati hizi vimewagharimu walipa kodi wa Tanzania. Ni wakati muafaka wa
kuzimaliza kero zilizopo kabla ya matatizo mengine hayajajitokeza siku za
usoni. Pili, inaonekana bado watanzania wanaamini katika njia ya mazungumzo
katika kusuluhisha mizozo na migogoro ya kisiasa. Duru kadhaa za mazungumzo
zilizopelekea muafaka wa kwanza mpaka wa tatu visiwani Zanzibar ni thibitisho
kwamba meza ya mazungumzo imeendelea kuwa nyenzo muhimu ya kutuliza jazba na
mihemko ya kisiasa. Lakini lazima tuzingatie angalizo kwamba si vyema kuendelea
na mtindo wa kusubiri misuguano itokee ndio tutafute suluhu. Utaratibu mzuri na
wa gharama ndogo ni kuzuia hali na mazingira ya misuguano kutokea.
- Hitimisho:
Mustakabali wa Muungano
Tunapohitimisha mada hii baada ya kupitia safari ndefu ya kihistoria ya
miaka hamsini, ni vyema kutafakari mustakabali wa muungano mwenyewe. Je kuna
nuru kwenye njia iliyombele kwa muungano wetu kuelekea (sio miaka mitano ijayo)
bali kuelekea miaka hamsini ijayo? Katika nukta hii sina budi kunuku maneno
ya Waziri wa Ushirikiano wa Afrika
Mashariki, Samuel John Sitta, katika dibaji ya kitabu kiitwacho “Miaka Hamsini
ya Uhuru wa Tanzania Bara: Tulikotoka, Tulipo na Tunakokwenda,” anasema “Sisi
raia wa Tanzania tunatamani tuendelee kuwa taifa linaloongozwa na utu, umoja,
heshima, uzalendo na maendeleo ya wote bila ubaguzi wa kukusudia au
kutokukusudia. Safari ya miaka hamsini (50) imeanza kutupa tahadhari kuhusu
tabia mbovu za ubinafsi, uzembe na kupungua kwa utu unaoheshimu kila mmoja
wetu”[20]. Angalizo la
tahadhari ni suala la kuzingatia kwa kuwa viashiria vya kupungua kwa moyo wa
utu, umoja na uzalendo vimejidhihirisha.
Katika tathmini yake ya hali ya muungano baada ya miaka kadha ya utekelezaji
wa makubaliano ya muungano, Gaudens Mpangala, anabainisha kwamba wakati siasa
na harakati za miaka ya 1950 na 1960 zililenga kumng’oa mkoloni na kuondoa
matabaka kati ya wafanyakazi na wakulima wadogowadogo kwa upande mmoja, na
matajiri na wamiliki wa ardhi kwa upande mwingine, kipindi hiki cha mfumo wa
vyama vingi harakati zimekuwa na sura ya kisiasa zaidi, kugombea madaraka au kulinda madaraka[21].
Mtazamo huo unaungwa mkono na msomi wa sheria, Harrison Mwakyembe ambaye anaona
mafanikio ya muungano yanapimwa kwa vigezo finyu vya vyeo badala ya kiwango cha
utatuzi wa kero wananchi[22].
Muungano wa Tanzania umepitia mitihani na misukosuko kadhaa kufikia wakati
huu ambapo mchakato wa kutengeneza katiba mpya
umeamsha hisia nzito hususan kuhusu muundo gani utumike kwa siku zijazo.
Kama ilivyoonyeshwa katika mada hii, hoja kuhusu muundo wa muungano ilijitokeza
kwa dhahiri miaka ya 1980 na kupelekea viongozi waandamizi wa Serikali ya
Mapinduzi Zanzibar kujiuzulu. Hoja ilijitokeza tena kwenye mapendekezo ya Tume
ya Nyalali ya 1991 na kufuatiwa na vuguvugu la G55 mnamo mwaka 1993, na
hatimaye kwenye ripoti ya Tume Ya Jaji Kissanga ya 1999. Ni matumaini yetu sisi
kama wachambuzi na pia wadau wa muungano wetu masuala yote ya muungano yatapewa kipaumbele sawa na
ufumbuzi wa kudumu wa matatizo na changamoto za muungano.
Tuungane na wale wasiopenda kuangalia uwepo au ustawi wa muungano kwa
darubini finyu ya idadi ya serikali tuzitakazo. Suala la kujirudi hapa ni kwa
kiasi gani tunapunguza au kuondosha siasa katika kuundesha muungano na badala
yake kuuimarisha na kuutumia muungano wenyewe kutimiza matarajio na matakwa ya
wadau wakuu wa muungano, yaani wananchi? Hili la pili likifanyika, litasaidia
sana kuondoa dhana iliyojengeja miongoni mwa watanzania wa pande zote mbili za
muungano, kwamba muungano ni wa viongozi wa kuchaguliwa na kuteuliwa badala ya
wananchi wanaoona fahari kuitwa watanzania kujisikia kuumiliki muungano.
Mwisho kabisa, misukosuko kwa muungano wa aina yoyote ile ni jambo la
kutarajia. Muhimu ni kutojisahau na kuipuuzia misukosuko hiyo mpaka iyumbishe
misingi madhubuti ya muungano husika. Mmoja wa wapigania haki maarufu duniani,
Mahatma Ghandi, aliwahi kusema hivi: Unity
to be real must stand the severest strain without breaking. Tafsiri isiyo
rasmi ya maneno haya ni kwamba umoja ili uwe wa kweli au halisi ni lazima
ustahimili majaribu au misukosuko mikali bila kuvunjika. Je umoja wetu
uliolelewa ndani ya muungano kwa kipindi cha miongo mitano (miaka hamsini)
unaweza kuhimili mawimbi makali siku zijazo pasipo kupagaranyika? Jibu la swali
hili laweza kuwa rahisi au gumu kutokana na mtazamo wa anayelitafutia majibu
swali lenyewe.
Kiambatisho A: Tume na Kamati Zilizoundwa Kipindi cha
1994-2014
Na
|
Tume/Kamati
|
Mwaka
|
1
|
Kamati ya
Shellukindo
|
1994
|
2
|
Kamati ya Jaji Mark
Bomani
|
1995
|
3
|
Kamati ya Baraza
la Mapinduzi kuhusu Ushirikiano wa Jumuiya ya Afrika Mashariki
|
1999
|
4
|
Kamati ya Rais ya
Kupambana na Kasoro za Muungano ya Shamhuna
|
1997
|
5
|
Kamati ya Rais ya
Kuchambua Ripoti ya Kisanga-Kamati ya Salum Juma
|
-
|
6
|
Kamati ya Rais ya
Kuandaa Mapendekezo ya Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar Juu ya Kero za
Muungano-Kamati ya Ramia
|
2000
|
7
|
Kamati ya Jaji
Kisanga
|
1998
|
8
|
Kamati Kuhusu
Masuala ya Simu- Kamati ya Kusila
|
-
|
9
|
Kamati ya Baraza
la Mapinduzi Juu ya Sera ya Mambo ya Nje
|
-
|
|
|
|
Chanzo: kutoka vyanzo mbalimbali.
[1] Soma Othman, Haroub“Tanzania: The Withering Away oft he Union“, uk. 35);
Bakari, Mohammed na Makulilo, Alexander, 2014, “Between Confusion and Clarity:
Rethinking the Union of Tanganyika na Zanzibar after 50 Years“, African Review
Vol. 40, No. 41, uk. 2-3.
[3] Shivji, Issa G., 2008 “Pan-Africanism or Pragmatism? Lessons of
Tanganyika-Zanzibar Union“, OSSREA: Addis Ababa, pp. 28-31.
[4] Abdul Sheriff, 2014,“The Proposed New Constitution and the Union Question“,
African Review, Vol. 41, No. 1, p.84.
[5] Shivji, Issa G., 2008, Pan-Africanism or Pragmatism? Lessons of
Tanganyika-Zanzibar Union, OSSREA: Addis Ababa, pp. 28-31.
[7] Minja, Rasul A.,
2014,”Revisiting the Plight of the Union:Why Still Embracing Pragmatism and
Political Expediency?”, African Review, Vol. 41, No. 1, uk. 185.
[10] Kamati ya Kuratibu
Maoni Kuhusu Katiba (Kamati ya Jaji Kisanga), Ripoti ya Kamati, Kitabu cha
Kwanza: Maoni ya Wananchi na Ushauri wa Kamati, 1999, uk. 46-47.
[11] Tazama Shivji, Issa G., 2006, Let the
People Speak: Tanzania Down the Road to Neo-Liberalism, CODESRIA Book
Series: Dakar, uk. 98.
[12] Amani Abeid Karume, 2011, “Hotuba ya Ufunguzi“, katika kitabu kiitwacho
Zanzibar Tuitakayo: Ujenzi wa Uvumilivu wa Kisiasa, Vitabu vya Mpango wa REDET
Na. 19, Dar es Salaam, uk. 1-2.
[14] Soma Rasul Ahmed, 2007, “Pemba Kama Ngome ya Upinzani: Tafakuri Kuhusu
Ustahimilivu wa Kisiasa na Kuimarika kwa Demokrasia“, Uchaguzi na Ukomavu wa
Demokrasia Tanzania, Vitabu cha Programu ya REDET Na. 14, Dar es Salaam, uk.
242.
[15] Augustino S. L. Ramadhani, 2011,“Zanzibar Tuitakayo: Utamaduni, Historia na
Uvumilivu wa Kisiasa,“ Ujenzi wa Uvumilivu wa Kisiasa, Vitabu vya Mpango wa
REDET Na. 19, Dar es Salaam, uk. 13-14.
[16] Idi Pandu Hassan anafafanua: “Inaposemwa Mtanzania, inakusudiwa kueleza
raia wa Tanzania amabaye anaweza kuwa ama anatoka Tanzania Bara au Zanzibar. Lakini anapotajwa Mzanzibari, ina maana ni
lazima awe ni raia wa Tanzania mkaazi wa Zanzibar. Hapa ieleweke wazi kuwa
kumtaja Mtanzania ni kutaja uraia au kwa maana nyingine utaifa; na kumtaja
Mzanzibari inakusudiwa Mtanzania anayeishi Zanzibar au kwa maana ya mbali,
mwenye asili na makaazi Zanzibar. Tofauti hii imeelezwa katika Sheria ya
Mzanzibari Na. 5/1985... Hivyo kwa mujibu wa Sheria ya Jamhuri ya Muungano na
Sheria ya Zanzibar, kila Mzanzibari kwanza lazima awe Mtanzania ndipo baadaye
aweze kuwa Mzanzibari. Kwa maana nyingine hakuna Mzanzibari asiyekuwa raia wa
Tanzania, lakini wapo raia wa Tanzania ambao si Wanzanzibari. Hiyo ndiyo
tofauti kubwa ya Mtanzania na Mzanzibari. Soma Idi Pandu Hassan, “Uzanzibari na
Ukaazi, Msingi wake Kikatiba na Kisheria: Mtazamo wa Ndani“, Zanzibar Tuitakayo: Ujenzi wa Uvumilivu wa Kisiasa, Vitabu vya Mpango wa REDET Na. 19,
Dar es Salaam, uk. 26.
[17] Makame Mahamud Khamis, 2011, “Uzanzibari na Ukaazi, Msingi wake Kikatiba na
Kisheria: Mtazamo wa Nje“, Zanzibar
Tuitakayo: Ujenzi wa Uvumilivu wa
Kisiasa, Vitabu vya Mpango wa REDET Na. 19, Dar es Salaam, uk. 47-48.
[18] Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Ofisi ya Makamu wa Rais, Taarifa ya Miaka
Hamsini (50) ya Uhuru wa Tanzania Bara katika Kudumisha Muungano na Hifadhi ya
Mazingira, 1961-2011, Novemba 2011, uk. 30.
[20] John M. Kasembo, chapisho
la 2013, Miaka
Hamsini ya Uhuru wa Tanzania Bara: Tulikotoka, Tulipo na Tunakokwenda, Limuru: Francisca Kolbe Press, uk. 16.
[21] Soma Gaudens P. Mpangala, 2011, “Tathmini ya Chaguzi katika Kipindi cha
Mfumo wa Vyama Vingi Zanzibar“, Zanzibar
Tuitakayo: Ujenzi wa Uvumilivu wa
Kisiasa, Vitabu vya Mpango wa REDET Na. 19, Dar es Salaam, uk. 60-61
(Msisitizo wetu).
[22]
Kwenye mada yake ingawa Mwakyembe
alikuwa akifanya tathmini ya mapinduzi na muungano lakini maono yake ni somo tosha kwa
viongozi na wadau wote wa Serikali ya Muungano. Tazama Harrison G. Mwakyembe,
2007, “Mapinduzi na Muungano,“ Muungano
wa Tanzania: Mafanikio, Matatizo Yake na Jinsi ya Kuuimarisha, Vitabu vya
Programu ya REDET Na. 15, Dar es Salaam, uk. 29.
bwana rasuli sema unachopenda wewe ni mamluki tu wa tanganyika na nakusikitia sana kama ulikuwa katika tume ya uchaguzi , kwa kuwa utakuwa umehusika kughushi kura na kumfanya sheni ashinde , nahuku bado unajiita rasuli unafikiri mungu atakuachia kwa jina lako? tambueni wenye akili kwa mungu kinachotambulika ni vitendo tu basi , hakuna cha jina wala nasaba wala rangi wala utaifa wala chochote kile , ndugu yangu rasuli jitatayarishe na kigongo cha mungu kwa kuwa ni mwongo na mnafiki na mzushi
ReplyDeletenakubaliana na mdau hapo juu , huyu anatafuta mafao ya kidunia ambayo atayapata kwa mada yake nzuri ya kujipendekeza kwa serikali ya muungano , wala sitoshangaa akapewa uwaziri ila atambue kwa mtukufu mungu atakuwa fukara wa kutupwa , mwache astarehe kidogo duniani
ReplyDelete