Habari za Punde

Polisi Yatangaza Donge Nono Atakaewafichua Wahusika na Mripuko Arusha.

Na Joseph Ngilisho,Arusha
JESHI la Polisi nchini limetangaza bingo ya shilingi milioni 10, kwa mtu atakayesaidia kufichua magaidi  waliohusika kuripua bomu katika baa ya Arusha Night Park, iliyopo Mianzini jijini hapa,ambapo watu 15 walijeruhiwa vibaya.

Aidha limekana taarifa iliyotolewa na Mkuu wa Mkoa wa Arusha, Magesa Mulongo ambae amekuwa akitoa taarifa juu ya kujulikana kwa watuhumiwa wa mabomu walioripua katika kanisa katoliki la mtakatifu Joseph Mfanyakazi, Olasiti na katika mkutano wa Chadema,eneo la Soweto.

Mkurugenzi wa upelelezi wa makosa ya jinai,Isaya Mngulu, ametoa kauli hiyo mbele ya wanahabari jijini hapa na kusisitiza kuwa polisi imeshindwa kuwatia mbaroni watuhumiwa wa mabomu na upelelezi bado unaendelea.

Alisema licha ya kuripua baa hiyo,watu hao walitega bomu jingine katika baa ya Washington iliyopo jijini hapa, ambalo halikuweza kuripuka baada ya kugundulika majira ya saa 6 usiku na kwamba polisi wanalifanyia uchunguzi zaidi.

Akijibu swali la mwandishi wa habari aliyetaka kujua kauli ya mkuu wa mkoa wa Arusha aliyoutangazia umma kwamba mtandao wa waripuaji wa mabomu umejulikana, alisema taarifa hiyo anaijua yeye kama msemaji wa serikali ila jeshi la polisi haliwezi kutoa taarifa ya upotoshaji.

“Nimesema muulizeni yeye, huyo ni msemaji wa serikali, hayo aliyowaambia mrudieni mkamuulize yeye, sisi kama polisi hatuna taarifa kama hiyo,’’ alisema.


Akizungumzia hali ya ulinzi na usalama katika jiji la Arusha, alisema polisi hawawezi kutoa ulinzi wa kila eneo lenye mkusanyiko wa watu ila aliwasihi wananchi kujilinda wenyewe kwani jeshi hilo halina uwezo wa kutoa huduma kila eneo kutokana na uchache wao.

Aliwataka wafanyabishara katika maeneo yenye mikusanyiko ya watu wengi kuhakikisha wanafunga kamera za usalama  (CCTV) yenye uwezo wa kurekodi matukio muda wote na kuimarisha ulinzi katika maeneo yao muda wote.

Aidha, alisema ni vyema wananchi wakachukua tahadhari na kutoa taarifa polisi pindi wanapoona kitu kisichoeleweka ama kumshuku mtu mwenye kubeba mfuko ambao utakuwa na mashaka.

Akielezea hali ya majeruhi, alisema watu 15 waliojeruhiwa na kulazwa kati yao saba wameruhusiwa na wengine nane wanaendelea kupatiwa matibabu katika hospitali ya mkoa Mount Meru.

Aliwataja wanaoendelea kupatiwa matibabu katika hospitali hiyo ni Evance Maleko, Evarist Richard, Petro James, Christine Zakaria, Pius Shayo, Antelus Zakaria,Sudi Ramadhani  na Mariam Juvenary Hans.


Aliongeza kuwa jeshi la polisi limeunda kikosi maalumu cha wataalamu wa kuchunguza mripuko wa bomu,kwa kushirikiana na jeshi la wananchi JWTZ na Ofisi ya Mkemia Mkuu wa serikali ili kubaini bomu hilo ni la aina gani.

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.