HOTUBA MAALUM YA WAZIRI WA NCHI OFISI YA MAKAMU WA KWANZA
WA RAIS MHE. FATMA ABDULHABIB FEREJ YA MAADHIMISHO YA SIKU YA KIMATAIFA YA UPIGAJI
VITA MATUMIZI NA USAFIRISHAJI WA DAWA HARAMU ZA KULEVYA DUNIANI- JUNE 26, 2014
--------------------------------------------------------------------------------------
Ndugu Wananchi
Assalamu Aleykum,
Hatuna budi
kutanguliza shukurani zetu Kwake Yeye Mwenyezi Mungu Subhaallah Wataala Aliyetukuka Mwingi wa Rehma kwa kutupatia
rasilimali adhimu ya kuwa katika hali ya afya, uzima, amani na
utulivu katika jamii yetu. Aidha napenda nichukue fursa hii kumuomba Mwenyezi
Mungu aendelee kutujaalie Rehema na Baraka zake katika maisha yetu yote na nchi yetu kuendelea kuwa na amani, utulivu na
masikilizano – AMIN.
Nichukue nafasi
hii pia kuvipongeza vyombo vya habari nchini kwa mchango mkubwa
vinavyotoa katika kuelimisha jamii katika masuala mbali mbali ambayo naamini yanachangia katika kuleta
ustawi na maendeleo kwa taifa letu kwa ujumla.
Ndugu Wananchi,
Ni wakati mwengine
tena Ofisi ya Makamu wa Kwanza wa Rais kupitia Tume ya Kuratibu na Udhibiti wa
Dawa Kulevya inaungana na jamii ya kimataifa katika maadhimisho ya Siku ya
Kimataifa ya Upigaji Vita Matumizi na Usafirishaji wa Dawa Haramu za Kulevya
(International Day Against Drug Abuse and Illicit Trafficking) ambayo huadhimishwa kila ifikapo tarehe
26 ya mwezi wa Juni ya kila mwaka duniani
kote.
Siku hii adhimu ilipitishwa rasmi katika azimio nambari 42/112 la Umoja
wa Mataifa mnamo mwezi wa Disemba 1987 likiwa na lengo
kuu la kutanabahisha juu ya athari mbali mbali zinazoambatana na tatizo la dawa za
kulevya, kusisitiza mshikamano duniani
kote na kuongeza nguvu na ushirikiano kwa jumuiya za kitaifa na kimataifa ili
kushinda vita dhidi ya dawa za kulevya na kuiweka jamii kuwa huru na matumizi
ya dawa hizo. Siku hii huratibiwa na Shirika la Umoja wa Mataifa linalopambana na
Dawa za Kulevya na Uhalifu Duniani.
(United Nations Office on Drugs and Crimes – UNODC).
Ndugu
Wananchi,
Kwa mnasaba wa maadhimisho haya,
Shirika la Umoja wa Mataifa la Dawa za Kulevya na Uhalifu huja na ujumbe au
kauli mbiu ya maadhimsho haya ambayo kwa mwaka huu inasema “ Ujumbe wa Matumaini: Matumizi ya Dawa za Kulevya Yanakingika na
Yanaweza Kutibika ’’ ( A message of Hope : Drug Use Disorders is Preventable
and Treatable).
Ujumbe au kauli mbiu hii ya kimataifa inalenga katika kuwepo mwitiko maalum na wa
makusudi katika kuongeza juhudi na mikakati juu ya utoaji wa taaluma za awali
za kinga zinazolenga kuinusuru jamii kutojiingiza katika matumizi ya dawa za
kulevya na kwamba matokeo ya matumizi ya dawa hizo yanaweza kupatiwa huduma
muafaka za tiba.
Ndugu Wananchi
Kwa mujibu wa taarifa ya Shirika la Umoja wa
Mataifa la Dawa za Kulevya na Uhalifu ya mwaka 2013 (World Drug Report 2013)
inayotolewa kila mwaka imeeleza kwamba tatizo la dawa za kulevya limeendelea kuwa tishio kubwa kwa afya za
watu, usalama na ustawi wa maendeleo ya
jamii kwa ujumla , kurejesha
nyuma uchumi na hali ya utulivu wa kisiasa duniani kote, taarifa hiyo inasisitiza
kwamba ni lazima juhudi za makusudi kuchukuliwa katika kukabiliana na hali
hiyo.
Aidha, taarifa hiyo ya UNODC
imeongeza kwamba matumizi ya dawa za kulevya na maambukizi ya virusi vya
UKIMWI bado ni changamoto na tishio katika masuala ya kiafya kwa mataifa mengi
duniani hususan kwa yale maeneo ambayo maambukizi yamekuwa yakichangiwa na
makundi maalum ikiwemo watumiaji wa dawa za kulevya kwa njia ya kujidunga
sindano.
Aidha kumekuwa na matokeo ya kupungua kwa maambukizi mapya
kwa makundi hayo kwa yale mataifa yanayozingatia Mkakati wa Upatikanaji wa Huduma kwa Wote
(The Universal Access) na programmu za mpango wa huduma kwa watumiaji wa dawa
za kulevya wanaojidunga sindano (Comprehensive Package for Injecting Drug
Users) ambao ulipitishwa na Jamii ya kimataifa kupitia Mkutano wa Ngazi ya Juu wa UKIMWI wa Mwaka
2006 . Shirika la Umoja wa Mataifa la Dawa za Kulevya na Uhalifu ( UNODC) kwa kushirikina na Shirika la Afya Duniani (
WHO) zimefanya tafiti mbali mbali zinazoenyesha upunguaji wa maambukizi ya
virusi vya UKIMWI kupitia mpango wa programu hizo.
Ndugu Wananchi,
Taarifa za hivi karibuni zilizotolewa kufuatia utafiti
uliofanywa hapo Zanzibar
zinaonyesha kuwepo kwa jumla ya watumiaji elfu tatu (3,000) wa dawa za kulevya,
ikijumuisha wale wanaotumia dawa hizo kwa njia ya kujidunga sindano. Aidha maambukizi ya virusi vya UKIMWI kwa
watumiaji wa dawa za kulevya kwa njia ya kujidunga sindano yamepungua kutoka
asilimia kumi na sita (16%) kwa
mwaka 2007 na kufikia asilimia kum na
tatu (13%) kwa mwaka 2012. Aidha huduma kwa vijana
wanaoacha matumizi ya dawa za kulevya kupitia nyumba za Marekebisho zilizoanza
karibu miaka minne iliyopita maarufu Sober House Unguja na Pemba
zimekuwa chachu ya mafanikio kwa vijana katika kujivua na matumizi ya dawa
hizo. Kwa kipindi cha 2009-2013 jumla ya vijana elfu moja mia tano na arobaini
(1,540) waliweza kupatiwa huduma katika makaazi hayo na asilimia thethalini (
30%) waliweza kujivua na matumizi ya dawa hizo na kuendelea na harakati zao za
kimaisha. Huduma na juhudi hizo ambazo
zimekuwa mfano wa kuigwa katika baadhi ya nchi za jirani zinapaswa kupongezwa
na kupewa kila aina ya msukumo.
Ofisi ya Makamo wa Kwanza wa Rais kupitia Tume ya Kuratibu na Udhibiti
wa Dawa za Kulevya itaendelea kutoa kila
aina ya msukumo katika kuendeleza mbele
huduma za makaazi kwa vijana wanaoacha matumizi ya dawa za kulevya maarufu
Sober Houses zinazoendeshwa na taasisi
zisizo za kiserikali Unguja na Pemba.
Ndugu Wananchi,
Wengi wetu ni mashahidi wa athari mbalimbali zinazotokana na matumizi ya
dawa za kulevya ikiwemo ongezeko la vitendo vya uhalifu, kutokuwepo kwa amani,
magonjwa ya akili, kupotea kwa rasilimali watu ya vijana na hata vifo na hivyo
hatupaswi kufumbiwa macho harakati na vitendo vya uuzaji wa dawa za kulevya
katika maeneo yetu hasa ikizingatiwa kwamba waathirika wakubwa ni vijana ambao ni
rasilimali na nguvu kazi kuu ya taifa
lolote duniani, na wanahitaji kuenziwa kwa kila hali. Maendeleo ya taifa lolote
hutegemea zaidi nguvu ya vijana wenye mwelekeo makini na hivyo hatma ya nchi
yetu ya kufikia Dira ya Maendeleo ya Zanzibar ya 2020 na Malengo ya Dunia ya Melenia (Millennium Development Goal) kamwe
hayataweza kufikiwa iwapo vijana wataendelea kujitumbukiza katika janga la
utumiaji wa mihadharati.
Ndugu Wananchi
Kwa mnasaba wa kauli mbiu ya Maadhimisho ya Siku hii naomba nichukue
nafasi hii adhimu ya kuviomba vyombo vya habari nchini kuchukua juhudi za makusudi
kwa kushirikina na taasisi husika katika kuelimisha jamii kwa kutoa makala na taarifa
mbali mbali sahihi zenye lengo la kuikinga jamii na hususan vijana katika
kujiepusha na matumizi ya dawa za kulevya. Aidha familia na jamii kwa ujumla
kuwa karibu na vijana wao na kufuatilia
nyendo na harakati zao na
kuwapatia maadili memo kwa lengo la kuwanusuru na kuwakinga katika kujiingiza
kwenye vitendo viovu ikiwemo matumizi ya dawa za kulevya.
Ndugu Wananchi,
Pia Napenda kutoa shukurani zangu za dhati kwa mashirika mbalimbali ya
nje na ndani kwa misaada yao ya hali na mali katika mapambano dhidi ya dawa za
kulevya hapa Zanzibar,baadhi ya mashirika hayo ni UNODC ,AIHA,ICAP,FHI na CDC. Aidha, shukurani za dhati ningependa
kuziwasilisha kwa Jumuiya zisizo za kiserikali hapa Zanzibar (NGO’s) kwa juhudi
zao katika kuunga mkono mwitiko wa Serikali katika vita Dhidi ya Dawa za
Kulevya nchini.
Ndugu Wananchi,
Mwisho ningependa tufahamu kwamba
kila mmoja wetu kwa nafasi yake
ikijumuisha, taasisi zisizo za kiserikali, elimu, Jumuiya za kidini,
wafanyabiashara kwa ujumla kuunganisha nguvu zetu ikiwa ni sehemu ya Maadhimsho
haya adhimu na pia katika kuongeza kasi ya Mapambano Dhidi ya Dawa za Kulevya nchini na
kuwanusuru vijana wetu ambao ni tegemeo la taifa letu.
“ZANZIBAR
BILA YA DAWA YA KULEVYA INAWEZEKANA”
Ahsanteni kwa kunisikiliza na Inshaallh Mwenyezi Mungu Awabariki
No comments:
Post a Comment