Na Haji Nassor, Pemba
Waliobakwa na kisha kuozwa
waume katika wilaya ya Wete mkoa wa kaskazini Pemba, wamesema ndoa za mkeka
zinazofungwa kama sulhu, zinachangia kwa kiasi kikubwa kasi ubakaji katika
jamii.
Uchunguzi uliofanywa na
mwandishi wa habari hizi, umeonesha jamii imekuwa na uharaka wa kuwafungisha
ndoa mara wanapobaini kuwepo vitendo hivyo,wakidhani ndio sulhu ya kuvitokomeza
badala yake vimekuwa vikichangia kuongezeka.
Uchunguzi umebaini imekuwa na
kawaida kuharakia sulhu ya ndoa, hata kama shauri hilo limeshafikishwa katika
vyombo vya sheria, jambo ambalo huwapa jeuri na kiburi wabakaji.
Mmoja kati ya waathirika wa
ubakaji na kisha kuolewa mwenye miaka 17, mkaazi wa shehia ya Mchangamdogo
wilayani humo, alisema binafsi baada ya kujihisi ameshapewa ujauzito,
alikimbilia kituo cha polisi na kisha muhusika kukamatwa.
Awali, alimueleza mpenzi wake
huyo kwamba, ameshampa ujauzito na alipokataa, ndipo alichukua uamuzi wa
kukimbilia kituo cha polisi Wete,inagwa kesi hiyo haikufikishwa mahakamani.
Nae muathirika mwengine wa vitendo
hivyo, mkaazi wa shehia ya Mchangamdogo (18) ambae alikatisha masomo alisema,
mara baada ya kubainika na wazazi wake kwamba ameshapata ujauzito, harakati za
kuolewa zilianza.
Aliwekewa mkazo na wazazi wake
na hata baadhi ya marafiki, kwamba ni vyema akakubali kuolewa na baada ya
kujkifungua aliachwa.
Wazazi wa vijana hao wa kike
walikiri kufanya hivyo, kutokana na kuogopa usumbufu katika vyombo vya sheria.
Kwa upande wake Mratibu wa
wanawake na watoto wa shehia ya Mchangamdogo, Mbeu Makame Bakari, alisema
chanzo cha vitendo hivyo ni kwa wakosaji kukosa kutiwa adabu inayofaa.
Sheha wa shehia ya Kinyikani wilaya
ya Wete, Mussa Rashid Said, alieleza kuwa, chanzo cha vitendo hivyo ni kuondoka
kwa malezi ya pamoja ambayo yalikuwa katika miaka ya iliopita.
Nae Mratibu wa wanawake na
watoto wa shehia ya Mjini Ole, Khadija Henop Maziku, alisema, bado jamii
haijaona ubakaji kuwa tatizo kutokana na kupuza pale linapotokezea katika
shehia zao.
No comments:
Post a Comment