Habari za Punde

Rais Azungumza na Balozi wa Canada.

STATE HOUSE ZANZIBAR
OFFICE OF THE PRESS SECRETARY
PRESS RELEASE
  Zanzibar                                                                                                                         27.11.2014
---
RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Ali Mohamed Shein amesema kuwa katika Mpango wa Kukuza Uchumi na Kuondoa Umasikini Zanzibar (MKUZA), sekta ya utalii ndio sekta mama na nyegine zimekuwa zikiongeza nguvu hivyo inahitaji kuendelea kuungwa mkono ndani na nje ya nchi.

Dk. Shein aliyasema hayo wakati alipofanya mazungumzo na  Balozi mpya wa Tanzania nchini Canada Mhe. Jack Mugendi Zoka,  Ikulu mjini Zanzibar aliyefika kwa ajili ya kuaga kwenda katika kituo chake kipya cha kazi nchini humo  kufuatia uteuzi wa Rais wa Jamhuri ya Muuungano wa Tanzania Dk. Jakaya Mrisho Kikwete hivi karibuni.

Katika maelezo yake Dk. Shein alimueleza Balozi huyo mpya wa Tanzania nchini Cadana kuwa Serikali ya Mapinduzi Zanzibar imekuwa ikifanyaa juhudi za makusudi katika kuhakikisha sekta ya utalii inaimarika na inaendelea kuwa sekta mama na muhimu hapa nchini.

Dk. Shein alisisitiza kuwa katika hatua ya uekezaji kwenye sekta ya utalii, serikali imejikita zaidi na uekezaji kwenye ujenzi wa mahoteli ya kitalii kwa kuzingatia kuwa ni miongoni mwa vivutio vikuu katika sekta hiyo ambayo imekuwa aikichangia asilimia 80 ya fedha za kigeni hapa Zanzibar.

Alisema kuwa kutokana na umuhimu huo hivi sasa hapa Zanzibar tayari kuna hoteli kadhaa za daraja la kwanza huku bado serikali ikiendelea kuwakaribisha na kuwahamasisha wawekezaji kutoka katika nchi mbali mbali duniani kuja kuekeza katika ujenzi wa hoteli za kitalii hapa Zanzibar.


Aidha, Dk. Shein alitumiaa fursa hiyo kumpongeza Balozi Zoka kwa kuteuliwa kuwa Balozi nchini humo na kueleza kuwa Zanzibar na Canada  zimekuwa na mashirikiano makubwa hivyo, ipo haja ya kuyakuza na kuyaimarisha zaidi ili kukuza uhusiano uliopo.

Akieleza juu ya sekta ya uwekezaji Dk. Shein alimueleza Balozi Zoka kuwa mbali ya kutilia mkazo uwekezaji katika ujenzi wa mahoteli pia, Serikali imekuwa ikitilia mkazo uwekezaji katika Hospitali za kisasa za binafsi ambazo zinatibu maradhi maalum.

Akiyataja maradi hayo, Dk. Shein alisema kuwa ni pamoja na maradi ya moyo, sukari, figo na mengineyo ambayo bado huduma zake za tiba zinahitajika kwa kiasi kikubwa hapa nchini, hivyo ipo haja kwa wawekezaji kutoka nchini Canada kuangalia fursa hiyo.

Dk. Shein alisema kuwa kupitia Shirika lake la Maendeleo la Kimataifa la Canada (CIDA) , nchi hiyo imeweza kuiunga mkono Zanzibar kwa kiasi kikubwa.

Akizungumzia kuhusu nchi ya Cuba ambapo Balozi Zoka pia, ataiwakilisha Tanzania, Dk. Shein alimueleza Balozi huyo kuwa nchi hiyo imekuwa na mahusiano ya kihistoria kati yake na Zanzibar na kueleza kuwa ni miongoni mwa nchi za mwanzo kuyatambua Mapinduzi ya  Zanzibar ya Januari 12, 1964.

Dk. Shein alimueleza Balozi Zoka haja ya kukuza uhusiano na ushirikiano na Cuba ambayo Balozi Zoka pia, ataifanyia kazi kwani  ni nchi rafiki wa Zanzibar ambayo imeweza kuunga mkono juhudi za Serikali katika kuimarisha sekta ya afya kwa kusaidia kuleta madaktari wakufunzi pamoja na uanzishwaji wa Chuo cha Udaktari cha Zanzibar  kwa kushirikiana na Chuo Kikuu cha Matanzas cha Cuba.

Nae Balozi mpya wa Tanzania nchini Canada Mhe. Jack Mugendi Zoka alitoa pongezi kwa mafanikio yaiopatikana hapa Zanzibar chini ya uongozi wa Dk. Shein katika kuimarisha sekta za maendeleo ikiwemo sekta ya utalii.

Balozi Zoka aliahidi kuwa atatumia fursa aliyoipata ya kuwawakilisha Watanzania wakiwemo Wazanzibari nchini Canada sambamba na kuitangaza Zanzibar kiutalii kutokana na vivutio vyake vilivyopo.

Aidha, Balozi huyo alimueleza Dk. Shein kuwa ameweza kukutana na wadau wa sekta ya utalii paamoja na uwekezaji wa hapa Zanzibar na kuweza kufanya nao mazungumzo pamoja na kubadilishaja nae mawazo juu ya kuzifanyia kazi sekta hizo atakapokuwa nchini humo ambao wameahidi kushirikiana nae kwa maslahi ya nchi.

Rajab Mkasaba, Ikulu Zanzibar

Postal Address: 2422 Tel.:0777427449. Fax: 024 2231822 
 E-mail: rajabmkasaba@yahoo.co.uk

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.