STATE HOUSE ZANZIBAR
OFFICE OF THE PRESS SECRETARY
PRESS RELEASE
Zanzibar
26.12.2014
RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la
Mapinduzi Dk. Ali Mohamed Shein amepokea gwaride la wanariadha kutoka Wilaya
kumi za Zanzibar na kuwataka washiriki vizuri pamoja na waamuzi kutenda haki
katika mashindano hayo kwani nia ya Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar ni kufufua vuguvugu
la michezo kama ilivyokuwa hapo siku za nyuma.
Mapokezi hayo ya
gwaride la wanariadha wa Zanzibar pamoja na waamuzi wa mashindano hayo ambapo
pia liliwashirikisha wanamichezo wenye ulemavu, yaliyofanywa na Dk. Shein yalifanyika
katika uwanja wa Amaan mjini Unguja na kuhudhuriwa na viongozi mbali mbali wa
Serikali, michezo pamoja na wanamichezo na wananchi.
Akiwasalimia
wanaridha hao mara baada ya kupokea gwaride lao lililopita mbele yake
likiongozwa na Brassband kutoka Chuo cha Mafunzo Zanzibar, Dk. Shein aliwataka
wanariadha hao washiriki vizuri na washindane kwa amani kama lilivyo jina la
uwanja huo wanaoshindania mashindano hayo wa Amaan, ambao uliasisiwa na Rais wa
mwanzo wa Zanzibar Marehemu Mzee Abeid Amani Karume.
Dk. Shein alisema
kuwa kufanikiwa kwa mashindano hayo na kufanyika kwa vizuri huku waamuzi
wakitenda haki kutaendelea kumpa hamasa ili apate kuendelea kuyaunga mkono
mashindano hayo ili kufikia malengo ya serikali ya kufufua vuguvugu la michezo
nchini.
Aidha, Dk. Shein
aliungana na wanamichezo hao pamoja na waamuzi wa mashindano hayo kufuata viapo
walivyokula mbele yake kuwa watashindana na kucheza kwa amani bila ya ugomvi na
kucheza kwa amani huku waamuzi wakiahidi kutenda haki.
Pamoja na hayo,
Dk. Shein alitumia fursa hiyo kutoa shukurani kwa Wizara ya Habari, Utamaduni
na Michezo, Baraza la Michezo la Taifa
la Zanzibar (BMTZ) pamoja na Wizara zote zilizosaidia kuendesha mashindano
hayo.
Mapema wanariadha
hao walikula kiapo kuwa watashiriki na kushindana kwa kufuata Sheria za
Shirikisho la riadha la Afrika na dunia sambamba na kufuata kanuni zote
zinazotawala michezo hiyo ambapo waamuzi nao waliapa kufuata sheria za
Kimataifa na kanuni zote bila ya woga wala upendelea wowote huku wakiadidi
zaidi kutenda haki.
Pamoja na hayo,
Dk. Shein mara baada ya kumaliza kutoa salamu zake hizo kwa wanamichezo hao
aliyazindua rasmi mashindano hayo ambayo yanatarajiwa kufanyika kwa muda wa
siku mbili terehe (26-27) Disemba mwaka
huu.
Mashindano hayo
yameandaliwa na Baraza la Michezo la Taifa Zanzibar (BMTZ) kwa kushirikiana na
Chama cha Riadha Zanzibar (ZAAA) chini
ya ufadhili wa Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Ali
Mohamed Shein.
Lengo la
mashindano hayo ni kuinua mcezho wa riadha Zanzibar kuanzia vijijini, maskulini
na maeneo mengine pamoja na kufufua vipaji vya wanariadha kutoka katika sehemu
husika kwa lengo la kuviendeleza sambamba na kutekeleza sera ya Michezo
Zanzibar.
Aidha, lengo jengine ni pamoja na kuonesha juhudi
binafsi za Dk. Shein katika kutekeleza dhamira yake ya kuona kuwa Zanzibar
inarejesha hadhi yake ya asili ya ubingwa katika michezo tofauti.
Mashindano hayo
yanawashirikisha wanariadha vijana 250 wa kike na kiume kutoka Wilaya zote kumi
za Zanzibar na yatahusisha michezo yote ya riadha ikiwemo kukimbia masafa ya
mita 100,200,400,800 na 1500. Pia, kurusha mkuki, kurusha tufe na kurusha
kisahani.
Fainali za
mashindano hayo zinatarajiwa kufanyika kesho jioni ambapo pia, Dk. Shein
anatarajiwa kuwa mgeni rasmi.
Rajab
Mkasaba, Ikulu Zanzibar
Postal Address: 2422 Tel.:0777427449. Fax: 024
2231822
E-mail:
rajabmkasaba@yahoo.co.uk
No comments:
Post a Comment