Habari za Punde

Dk. Bilal:Wanaotumia wanyonge kusaka uongozi wakemewe

Na Augusta Njoji, Dodoma
MAKAMU wa Rais wa Jamhuri wa Muungano, Mhe. Dk. Mohammed Gharib Bilal, amewataka viongozi wa dini kuwakemea wanasiasa na watu wanaotaka kuingia madarakani kwa manufaa ya binafsi kupitia migongo ya wanyonge.

Dk. Bilal alitoa kauli hiyo jana katika sherehe za kumuapisha Askofu Mkuu wa Kanisa Katoliki jimbo kuu  la Dodoma, Mhashamu Askofu Beatus Kinyaiya.

"Ni vyema tukakumbuka kigezo kikubwa cha kiongozi bora ni yule mwenye hofu ya Mungu na anaewajali watu anaowaongoza bila ubaguzi wowote,"alisema.

Alisema mwaka huu ni wa uchaguzi na chaguzi zimekuwa zikiibua hisia tofauti miongoni mwa wananchi, hivyo  aliwaomba viongozi wa dini zote nchini kuliombea taifa   katika kipindi hiki ili wananchi waweze kufanya uamuzi sahihi.

"Uamuzi huu utawafanya kuchagua watu ambao wataliongoza taifa kwa kuendeleza misingi ya amani, umoja, upendo na mshikamano,"alisema.

Aliwahakikishia wananchi kuwa serikali imejipanga vilivyo kuhakikisha  inasimamia zoezi lote la uchaguzi kwa misingi ya haki, amani na utulivu.


"Tunaamini zoezi hilo litafanyika kwa amani na utulivu mkubwa na mwisho wa  siku Watanzania watapata viongozi wazuri, wanaowataka ili washirikiane nao kusukuma mbele gurudumu la maendeleo yetu,”alisema.

Aliwataka Watanzania  kudumisha amani,umoja, upendo na mshikamano.
“Mungu ameibariki sana nchi yetu, tumeishi kwa muda mrefu kama taifa moja  lenye amani na mshikamano mkubwa bila kujali tofauti za rangi, kabila, dini  wala hali za watu, amani ni sharti la kwanza katika maendeleo ya binadamu.Kuna baadhi ya watu wanadhani wanapozungumzia kulinda amani  ya nchi ni hila za siasa tu, hao wamepotoka wapuuzwe na kuwaombea kama  alivyosema Yesu Kristu pale msalabani,"alisema.


Kwa upande wake Askofu Mkuu wa kwanza wa jimbo hilo,Kinyaiya, aliwataka  wazazi kutimiza wajibu wao katika kusimamia maadili ya watoto hao ili  kupunguza mmonyoko wa maadili.

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.