Habari za Punde

Kinana ahimiza viongozi kuwaletea maendeleo wananchi

Na Mwantanga Ame
Katibu Mkuu wa Chama cha Mapinduzi,Abdulrahman Kinana, amewataka viongozi wa upinzani waliomo ndani ya serikali kuiendesha serikali kwa kuwapatia maendeleo wananchi na sio kuonesha ubabe, vurugu za kusukumiana maneno.

Kinana, aliyasema hayo katika uwanja wa Gereji, wakati akiwahutubia wananchi walioshiriki mkutano wa hadhara, wilaya ya magharibi Unguja.

Alisema wanaCCM, wana kila sababu ya kujiandaa kuyarejesha majimbo yalio mikononi mwa wapinzani, kwa kile kinachoonekana baadhi ya viongozi wameshindwa kuwajibika vyema, na kutumia nafasi zao kuwajengea hasama wananchi.

Alisema hivi sasa, baadhi ya shughuli za serikali katika wizara zimedorora, kiasi ambacho hakuna sababu ya kuogopa kuyarudisha majimbo hayo ndani ya mikono ya CCM.

Alisema CCM kina ilani yake, ambayo inalazimika kutekelezwa na viongozi walio madarakani, lakini kinachoonekana bado kuna waliopewa dhamana hawataki kutimiza hilo kwa kudai kuwa wanasubiri serikali yao iingie madarakani.


Alisema huo sio uwajibikaji uliokuwa unatakiwa utekelezwe katika serikali ya umoja wa kitaifa, kwa vile utaratibu unawataka walio madarakani kushirikiana kuwaletea maendeleo wanachi.

Alisema maendeleo ya Zanzibar hayapaswi kuletwa kwa maneno, wakati kuna watu walieleza kuwa wana uwezo wa kuwapatia maendeleo na kuwaahidi vijana kuwapa ajira, lakini kwa kutangaza masharti hadi washike serikali, jambo ambalo haliwatendei haki.

“Sisi tukiamka tunafikiria nini tuwafanyie wananchi, wao wanafikiria kuwaambia maneno ya kudai wananyanyaswa,wakiondoka wanasindikizwa na ving’ora nataka kuwaambia waliopewa dhamana ndani ya serikali ya umoja wa kitaifa onyesheni mfano,” alisema.

Aidha, Kinana, aliwataka wanaCCM kujiandaa kushiriki katika kura ya maoni pamoja na kujiandaa na uchaguzi mkuu ujao.
Hata hivyo,aliwaonya viongozi wa chama hicho kutochangia kuuharibu uchaguzi mkuu ujao, kwani chama hakitawavumilia.

Naibu Katibu Mkuu wa UVCCM Zanzibar, Shaka Hamdu, , alisema ipo haja ya Msajili wa Vyama vya Siasa Tanzania, kuvionya vyama vinavyokiuka taratibu kwa kutumia bendera na nyimbo ambazo vyama vyake vilishafutwa.

Naye Balozi Ali Karume, ambaye ni Mjumbe wa Halmashauri Kuu ya Taifa, alisema ipo haja ya kuangaliwa upya mfumo wa Serikali ya Umoja wa Kitaifa baada ya kumalizika kwa uchaguzi mkuu.

Nae Mjumbe wa Kamati Kuu, Shamsi Vuai Nahodha, alisema CCM hakina sababu ya kutounga mkono kura ya maoni kwa vile kutofanya hivyo ni kuvunja Muungano.


Mapema Kinana alifanya ziara katika miradi mbali mbali ya chama kwa kufungua na kuweka mawe ya msingi katika maskani za chama na kuahidi kuzisaidia mabati pamoja na mifuko ya saraju.

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.