Habari za Punde

Askari waliojeruhiwa Tanga watoka hospitali

Na Amina Omari,Tanga
ASKARI polisi watano waliojeruhiwa kwenye tukio la kurushiana risasi katika ya polisi na kikundi cha wahalifu kwenye mapango ya Mleni jijini Tanga, wameruhusiwa kutoka hospitali baada ya hali zao kuimarika.

Akizungumza na Zanzibar Leo kwa njia ya simu, Kamanda wa Polisi Mkoa wa Tanga, Freisser Kashai, alisema majeruhi hao waliruhusiwa mapema jana baada ya madktari kuridhishwa na hali zao.

Akizungumzia hali ya usalama katika eneo la tukio, alisema eneo hilo kwa sasa hali ni ya usalama huku vikosi vya polisi vikiendelea na doria za kawaida za kuimarisha amani.

"Kwa sasa hali ni ya amani tunaendelea na upelelezi wetu wa kuwahoji watuhumiwa tulio wakamata huku vikosi vya jeshi vikendelea kufanya doria ili kuwabaini watuhumiwa wengine,” alisema.

Alisema kinachoendelea kwa sasa ni upelelezi na misako ili kuwakamata watuhumiwa wengine na kuendelea kuitafuta silaha moja ambayo bado haijapatikana.


Alisema kwa sasa vikundi vya jeshi ambavyo vilikuwa wanashirikiana navyo kwenye oparesheni vimepungua kwenye eneo la mapango hayo.

Katika hatua nyingine Kamanda Kashai alisema ameridhishwa na mafanikio ya oparesheni hiyo yalivyofanyika na kufanikiwa kuwakamata baadhi ya watuhumiwa pamoja na silaha moja katika ya mbili zilizoporwa.

"Niwaombe wananchi wa Tanga waendelee kuwa na imani ya jeshi lao kwani tunafanya kazi usiku na mchana ili kuhakikisha mkoa huu unakuwa na amani na utulivu,"alibainisha.

Pia aliwataka wananchi kuwa na subra katika kipindi hiki kwani baada ya upelelezi kukamilika taarifa kamamili kuhusiana na watuhumiwa wataitoa na kueleza kama ni watu wa namna gani.


Kwa upande wa wakazi wa Mleni wamekiri kuwa kwa siku ya jana doria za magari makubwa ya jeshi hazikuwepo kabisa ila walikuwepo askari wachache kwa ajili ya kuendelea na upelelezi.

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.