Habari za Punde

Tume yalaani mauaji ya albino

Na Mwandishi wetu
TUME ya Haki za Binadamu na Utawala Bora (THBUB) imesikitishwa na mauaji ya kikatili ya mtoto Yohana Bahati, aliyetekwa nyara hivi karibuni katika kijiji cha Ilelema, Chato mkoani Geita.

Pia tume hiyo imelaani kuumizwa kwa mama yake, Ester Jonas, wakati anatetea uhai wa mwanae wakati wa tukio lililotokea Februari 15 mwaka huu.

Taarifa iliyosainiwa na Mwenyekiti wa tume hiyo,Bahame Tom Nyanduga,imesema kwa ujumla vitendo vya ukatili wanaofanyiwa watu wenye ulemavu wa ngozi, ni matukio ya ukiukwaji wa sheria na haki za kibinadamu.

Alisema matukio hayo yanaonesha yamekuwa yakichagiwa na imani za kishirikina hivyo tume inakemea matendo haya na kutaka yapigwe vita.

Mwenyekiti huyo alisema chini ya katiba na mikataba ya kimataifa ya haki za binadamu serikali inao wajibu wa kulinda raia wake hivyo aliiomba serikali kuwatafuta wale wote wanaohusika na vitendo hivyo na kuwafikisha mbele ya vyombo vya sheria.


Aidha alisema tume inaungana na wananchi, wadau mbalimbali na serikali kulaani vikali mauaji ya mtoto Yohana na kujeruhiwa vibaya mama yake wakati akitetea haki ya mwanae kuishi katika jamii huru.

Aliikumbusha serikali kuwa wakati umefika wa kufanyia marekebisho makubwa sheria ya uchawi (sura ya 18 ya 1928) au kutunga sheria mpya ili kupiga marufuku vitendo vyote vinavyoendeleza imani za uchawi na ushirikina.

Alisema tume inatoa wito kwa wananchi na jamii yote kwa ujumla kuachana na imani potofu zenye mtizamo hasi kwamba mafanikio yoyote yanaweza kupatikana kwa njia za kishirikina.

“Tume inakumbusha wananchi kuwa mafanikio yoyote yatapatikana kwa kufanya kazi zote halali kwa bidii, na siyo kwa njia za kishirikina ikiwemo kutumia viungo vya watu wenye ulemavu wa ngozi,” alisema.


Wakati huo huo, Kamishna wa Haki za Binadamu wa Umoja wa Mataifa, Zeid Ra'ad Al Hussein, amekemea mauaji ya walemavu wa ngozi nchini Tanzania.  

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.