Habari za Punde

Dk. Shein Afungua Kiwanja cha Kisasa cha Gofu Zanzibar.

STATE HOUSE ZANZIBAR
OFFICE OF THE PRESS SECRETARY
PRESS RELEASE
  Zanzibar                                                                                                                              9.2.2015
---
RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Mhe. Dk. Ali Mohamed Shein amefungua kiwanja kipya na cha kisasa cha mchezo wa Gofu na kusema kuwa ufunguzi   huo  unakwenda sambamba na jitihada zinazochukuliwa na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar, Awamu ya Saba ya kufufua michezo nchini.

Dk. Shein aliyasema hayo, katika hotuba yake iliyosomwa kwa niaba yake na Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais na Utawala Bora, Mhe. Dk. Mwinyihaji Makame  katika sherehe za ufunguzi wa kiwanja cha mchezo wa Gofu katika Hoteli ya Sea Cliff, iliyopo Kiombamvua, Wilaya ya Kaskazini B, Mkoa wa Kaskazini Unguja.

Katika hotuba hiyo, Dk. Shein alisema kuwa lengo na jitihada hizo ni kuona kuwa vuguvugu la michezo linarejea Zanzibar na kuweza kutoa wanamichezo wenye vipaji mbali mbali wenye uwezo wa kushinda katika mashindano ya Kimataifa.

Alisema kuwa imani yake ni kuwa uwanja huo wa gofu utapelekea Zanzibar kuwa na wanamichezo wenye vipaji vya kucheza mcheo huo na kushinda katika michuano ya Kimataifa.

“Bado ni mapema kufikia kuwa na Tiger Woods kutoka Zanzibar, lakini hakuna sababu ya kuondoa matumaini kwamba hatuwezi kuwa na mchezaji mahiri katika mchezo huo”, alisema Dk. Shein.

Aidha, Dk. Shein alisema kuwa ufunguzi wa kiwanja hicho cha Gofu chenye hadi ya Kimataifa utachangia sana katika kurejesha sifa na umaarufu wa Zanzibar katika michezo ukiwemo mchezo wa gofu.

“Nafahamu kwamba hivi sasa si watu wengi wanaofahamu kuwa Zanzibar ilikuwa ni miongoni mwa nchi za mwanzo kabisa barani Afrika kuwa na Kiwanja cha Mchezo wa Gofu ambacho kilikuwa katika eneo la MnaziMmoja, Mivinjeni hadi upande wa uwanja wa Maisara, Mjini Unguja”,alisema Dk. Shein.

Pamoja na hayo, Dk. Shein alisema kuwa amefurahi kupata taarifa kuwa wamiliki wa hoteli hiyo hawaoni kama kiwanja hicho ni mali yao pekee yao bali wanaona kama ni mali ya Zanzibar na watu wake wote kutokana na kupata hisia kuwa kuzingatia kuwa uzuri wa kiwanja hicho utatumika katika kuitangaza Zanzibar kiutalii na kimichezo duniani kote.


Dk. Shein alitoa nasaha kwa wananchi kuendelea kuwaunga mkono na kuwapa mashirikiano yanayohitajika wawekezaji wote walioekeza hapa nchini ili nao waendelee kufanya mambo makubwa yenye manufaa kwa maendeleo ya kila mmoja.

Alisisitiza kuwa ni dhahiri kuwa ufunguzi wa kiwanja hicho unakwenda sambamba na juhudi zinazochukuliwa na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar Awamu ya Saba za kuimarisha Sekta ya Utalii, ambayo ndio sekta kiongozi kwa uchumi wa Zanzibar.

Alisema kuwa utalii hivi sasa unachangia asilimia 80 ya fedha za kigeni na una mchango wa asilimia 27 katika pato la Taifa.

Sambamba na hayo, Dk. Shein aliwasihi wamiliki wa hoteli hiyo waongeze kasi katika kukitangaza kiwanja hicho na vivutio mbali mbali vya utalii viliopo Zanzibar katika sehemu mbali mbali za dunia kupitia mitandao, televisheni na vyombo mbali mbali vya habari.

Kwa mara nyengine Dk. Shein aliuhimiza uongozi wa Wizara ya Habari, Utamaduni na Utalii na Michezo pamoja na uongozi wa Kamisheni ya Utalii Zanzibar kuendelea kushirikiana na wawekezaji wa ndani na nje ya anchi katika kuitangaza Zanzibar.

Dk. Shein alitumia fursa hiyo kuwahakikishia wawekezaji walioekeza hapa nchini kuwa Serikali itaendelea kulinda na kuendeleza hali ya amani na utulivu, jambo ambalo limeipatia sifa kubwa Zanzibar na kuendelea kuwavutia wageni kutoka pande zote za dunia.

Aidha, alisema kuwa Serikali ityaendelea kwualinda watalii, wawekezaji pamoja na mali na rasilimali zao zilizopo nchini.

Katika hotuba yake hiyo, Dk. Shein alitumia fursa hiyo kutoa pongezi kwa mtengenezaji maarufu wa viwanja vya Gofu duniani, Bwana Peter Matkvich kutoka Afrika ya Kusini ambaye ndie aliekitengeza kiwanja hicho.

Mapema Bwana Peter Matkovich alitoa shukurani na pongezi kwa kupata fursa hiyo na kueleza kuwaujenzi wa kiwanja hicho utasaidia kwa kiasi kikubwa kuimarisha mchezo huo unaopendwa duniani na ni miongoni mwa viwanja bora katika ukanda huu wa bara la Afrika.

Alisema kuwa uwanja huo una vishimo 18 ambayo ni idadi ya vishimo vinavyokuwemo kwenye viwanja vinavyotumika kwa mashindano makubwa ya Kimataifa.

Nae Mwenyekiti wa Kampuni ya ‘Sea Cliff  Resort and Spa Zamzibar’, Bwana Subhash Patel alitoa pongezi kwa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar pamoja na uongozi wake kwa mashirikiano yao mazuri katika kuhakikisha mafanikio hayo yanapatikana.


Aidha, Bwana Patel alisema kuwa hatua hiyo itasaidia kuongeza kasi ya michezo nchini sambamba na kuinua sekta ya utalii bila ya kusahau soko la ajira na kujenga urafiki.

Viongozi mbali mbali walihudhuria katyika hafla hiyo akiwemo Waziri wa Ardhi, Makaazi, Maji na Nishati, Mhe. Ramadhan Abdalla Shaaban, Mkuu wa Mkoa wa Kaskazini Unguja Mhe. Meja Mstaafu Juma Kassim Tindwa, viongozi wa serikali, wageni mbali mbali wa mchezo huo kutoka ndani na nje ya Zanzibar.

Rajab Mkasaba, Ikulu Zanzibar

Postal Address: 2422 Tel.:0777427449. Fax: 024 2231822 
 E-mail: rajabmkasaba@yahoo.co.uk

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.