Habari za Punde

CCM Wilaya ya Arusha Kimesema Kitachukua Hatua Kali kwa Wanachama wake.

Na Joseph Ngilisho,Arusha
CHAMA cha Mapinduzi wilaya ya Arusha, kimesema hakitasita kuchukua hatua kali kwa wanachama wake watakaofanya kampeni mapema kwa kugawa msaada wowote utakaoashiria kampeni.

Aidha chama hicho kimepiga marufuku wagombea ‘njaa’ wasio na kipato na kuwataka wajitathimini kabla ya kuonyesha nia ya kuwania nafasi yoyote.

“CCM haihitaji wagombea wachovu,kama mgombea hana uwezo hata wa kugharamia kipaza sauti asishiriki, tunataka mgombea mwenye uwezo na  hata kama hana uwezo basi awe na watu wanaomuunga mkono,” alisema Katibu wa CCM wilaya hiyo,Feruz Banno.

Alizungumza kwenye maadhimisho ya siku ya Jumuia ya Wazazi,ambapo pamoja na mambo mengine aliwataka makada walioonesha nia ya kugombea kiti cha ubunge jimbo la Arusha mjini,kutoshiriki kampeni zozote kwa sasa.

Alikiri chama kutafunwa na makundi ya wagombea uchaguzi uliopita ambayo hadi sasa hayajavunjika na usaliti ndani ya chama,huku akieleza kuwa mabalozi wake wengi wamekuwa wasaliti na wamepandikizi ndani ya chama hatua ambayo imesababisha CCM  kuangushwa.


Alisema hadi sasa jumla ya makada wake wanane wameonesha nia ya kugombea ubunge katika jimbo la Arusha mjini,akiwemo kamanda wa UVCCM mkoa, Philemon Mollel.

Katibu wa jumuiya ya wazazi mkoa wa Arusha, Mayasa Kimbau, alionyesha mashaka ya kuendelea kupoteza jimbo la Arusha,iwapo wananchama hawatobadilika kwa kuvunja makundi.

Alisema japo makundi ni muhimu kwa mgombea yoyote lakini ni vyema yakavunjwa baada ya uchaguzi kumalizika.


“Tangu nihamishiwe Arusha wiki mbili zilizopita kwa kweli nimegundua Arusha kuna makundi makubwa ya tangu uchaguzi wa mwaka 2010 na msipo yavunja hatutaweza kulichukua jimbo hili na tutaendelea kupoteza maeneo mengi kwa sababu ya chuki zetu na usaliti,” alisema.

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.