WASIFU WA MAREHEMU MHESHIMIWA SALMIN AWADH SALMIN,
MWAKILISHI WA JIMBO LA MAGOMENI
Baraza la
Wawakilishi Zanzibar, limepokea kwa mshtuko na masikitiko makubwa, kifo cha Mwakilishi
wa Jimbo la Magomeni Zanzibar, Mheshimiwa Salmin Awadh Salmin kilichotokea
baada ya kuugua ghafla hapo jana Alkamis
tarehe 19. 02. 2015 wakati akiwa katika kikao cha kikazi cha kichama.
Mheshimiwa Salmin Awadh ambaye alikuwa Mwakilishi tangu Octoba 2005, alizaliwa
tarehe 06. 06. 1958 huko Makunduchi, Wilaya ya Kusini, Mkoa wa Kusini Unguja.
Marehemu
Salmin Awadh alipata elimu yake ya msingi katika Skuli ya Kiongoni kuanzia
mwaka 1963 na baadaye kuendelea na masomo ya sekondari katika Skuli ya
Sekondari ya Makunduchi. Vile vile Marehemu alijiunga na Chuo cha Uchumi Zanzibar mwaka 1971 hadi mwaka 1974.
Marehemu
Mheshimiwa Salmin Awadh aliwahi kujiunga na kazi ya Ulinzi kupitia Jeshi la
Wananchi JWTZ kuanzia 1976 hadi 1986 na kufikia cheo cha Sergent. Mbali ya kazi ya
hiyo ya Ulinzi, Marehemu aliwahi kuwa Meneja katika Hoteli ya Narrow Street,
Zanzibar baina ya mwaka 2000 na mwaka 2005.
Katika
shughuli za kisiasa, marehemu amewahi kushika nyadhifa mbali mbali katika Chama
cha Mapinduzi ikiwemo Ujumbe wa Halmashauri Kuu ya tawi la Magomeni kuanzia
mwaka 1982 hadi 1992, Mjumbe wa Kamati ya Siasa ya Jimbo la Magomeni tangu
mwaka 1992. Mnamo mwaka 1995 hadi mwaka 2000 marehemu Salmin Awadh alikua
Diwani wa Magomeni.
Mheshimiwa
Salmin alikuwa Mjumbe wa Baraza la Wawakilishi wa Jimbo la Magomeni, kupitia
Chama cha Mapinduzi tangu Uchaguzi Mkuu wa mwaka 2005 na kuendelea na wadhifa huo hadi
kufariki kwake. Aidha Marehemu alichaguliwa Kuongoza Kamati mbali mbali ikiwemo Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya
Fedha na Uchumi ya Baraza la Wawakilishi pamoja na Kamati ya Fedha, Biashara na
Kilimo ya Baraza la Wawakilishi, Kamati ambayo alikuwa anaiongoza hadi kufariki
kwake.
Vile vile kutokana na umakini wake na nidhamu ya utendaji kichama mnamo
mwezi Juni, 2011 Marehemu alichaguliwa kuwa Mnadhimu wa Chama cha Mapinduzi
ndani ya Baraza la Wawakilishi ambapo kwa nafasi hiyo alikuwa pia Mjumbe wa
Halmashauri Kuu na Kamati Kuu ya Chama cha Mapinduzi wadhifa ambao ameendelea
nao hadi kufarika kwake.
Marehemu
Salmin Awadh pia alikuwa miongoni mwa Mjumbe wa Bunge Maalum la Katiba na alitowa
mchango mkubwa katika Bunge la Katiba ambapo alikuwa Makamo Mwenyekiti wa Kamati namba 10 ya Bunge hilo. Aidha kutokana
na uelewa wake wa masuala mbali mbali
Marehemu alichaguliwa kuwa Makamo Mwenyekiti wa Bodi ya Gazeti la Zanzibar
leo tokea mwaka 2009 hadi kufariki
kwake.
Katika
kipindi chote cha kuwawakilisha wananchi
wa Jimbo la Magomeni, Marehemu alikuwa mtetezi mkubwa wa maslahi ya wananchi wa
jimbo hilo pamoja na wananchi wote wa Zanzibar na aliifanya kazi yake hiyo kwa
moyo wake wote, uadilifu na mashirikiano makubwa na Wajumbe wenzake wa Baraza
la Wawakilishi.
Ni
dhahiri kuwa Baraza la Wawakilishi, Chama cha Mapinduzi, Wananchi wa Jimbo la Magomeni na wananchi
wote kwa jumla, wameondokewa na mtu muhimu na mahiri mwenye kujiamini katika
kusimamia anachokiamini katika kuleta maendeleo ya Taifa.
Marehemu
ameacha kizuka na watoto saba.
Tunamuomba
Mwenyezimungu aijaalie familia ya Marehemu pamoja na wananchi wa Jimbo la
Magomeni, subira na utulivu katika kipindi hiki kigumu cha msiba. Tukielewa kwamba sote ni waja wa Mwenyezi
Mungu na hapana shaka marejeo yetu ni kwake.
Mwenyezi
Mungu aiweke roho ya Marehemu mahali pema peponi. Amin.
Amour M. Amour
MKUU WA UTAWALA
BARAZA LA WAWAKILISHI
ZANZIBAR.
20 Februari, 2015.
No comments:
Post a Comment