Habari za Punde

Nini Muislam anatakiwa kufanya jua likipatwa?

Tukijaaliwa siku ya Ijumaa tarehe 20/03/2015 katika nchi ya Uingereza, na sehemu nyengine za Ulaya jua litapatwa majira ya asubuhi kuanzia saa 3.30 kwa mujibu wa wakati wa Uingereza.

Kupatwa kwa jua ni jambo nadra sana kutokea kwani mara ya mwisho hapa Uingereza jua lilipatwa mwaka 1999. Na kwa mujibu wa wataalamu jua litapatwa tena mwaka 2026 bi ithni Llaah.

Nini anapaswa Muislamu kufanya jua likipatwa?

Kwa mujibu ya hadithi aliyoisimulia Al Mughiyrah , Allaah amuwie radhi, amesema: Mtume swalla Allaahu ‘alayhi wasallam amesema:

‘Hakika jua na mwezi ni alama mbili miongoni mwa alama za Allaah, Hayapatwi kwa sababu ya mauti ya mtu au uhai wake na mkiona (kupatwa huku), ombeni du’aa kwa Allaah na msali mpaka litakapoachiwa’ Bukhaari na Muslim.

Sala hii, kwa mujibu wa Maulamaa, ni Sunnah iliyotiliwa mkazo na ni miongoni mwa Sala za sunnah za nadra kutokea katika uhai wa binadamu kwani imesimuliwa kwamba Mtume swalla Allaahu ‘alayhi aliisali sala hii mara moja tu katika uhai wake siku alipofariki mwanawe Ibraahim, na watu wakaunganisha tukio la kufa mwanawe na kupatwa kwa jua mpaka ikambidi atoe ufafanuzi kwamba vitu hivi viwili havihusiani.

Vipi Sala ya Kusuuf husaliwa:

Husaliwa Jamaa msikitini na ndio vizuri zaidi (wanawake wanaweza kutoka na kwenda kusali msikitini ikiwa hakutokuwa na fitna pia wanaweza kusali majumbani)

Haina adhana wala Iqaamah.

Baada ya sala hufuatiwa na Khutbah na kuomba du’aa.

Ina Rakaa mbili kila rakaa huwa na rukuu mbili, visimamo viwili na visomo viwili (tofauti na sala za kawaida zenye rukuu moja, kisimamo kimoja na kisomo kimoja)

Utaratibu wake kwa ufupi

  • Unaleta takbiiratul Ihraam
  • Unasoma Suuratul Faatihah
  • Unasoma sura nyengine ( vizuri iwe ndefu mfano wa baqarah)
  • Unarukuu rukuu iliyokuwa ndefu
  • Unasimama baada ya kurukuu na kusema Samia Llaahu liman hamidah Rabbanaa walakal hamd
  • Unasoma Suuratul Faatihah tena
  • Unasoma Sura nyengine vizuri iwe ndefu chini ya sura ya mwanzo
  • Unarukuu rukuu iliyokuwa ndefu chini ya urefu wa rukuu ya kwanza
  • Unasimama baada ya kurukuu na kusema Samia Llaahu liman hamidah Rabbanaa walakal hamd
  • Unasujudu sijda ya kwanza
  • Unakaa kitako baina ya sijda mbili na kuomba dua kama kawaida
  • Unasujudu sijda ya pili na kuomba du’aa
  • Unainuka na kuanza rakaa ya pili na kufanya kama ulivyofanya rakaa ya kwanza hadi mwisho wa Sala kwa kuleta tashahhud na kisha kutoa salam.

Tujitahidi kuhakikisha tunaisali sala hii tukijaaliwa kesho kwani tutakuwa tunahuisha Sunna za Mtume wetu Swalla Allaahu ‘alayhi wasallam na pia kuonesha umuhimu wa dini yetu yanapotokea matukio yasiokuwa ya kawaida kwamba tunarudi kwa Mola wetu na kuomba.

Allaahumma Aamiyn


2 comments:

  1. SHEKH Allah akujaze kheri kwa kutufunza mimi nilikuwa hata sijui, lakini nikijaaliwa kesho nami nitashiriki kuitekeleza sunna hii inshaalah

    ReplyDelete
  2. Shukran Maalim kwa ukumbusho uliobeba ujumbe mzito ndani yake, Allah akulipe kheri akhera na duniani, kwa wasiojaaliwa kuswali kuna nyiradi zozote ambazo wanaweza wakasoma?

    ReplyDelete

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.