Habari za Punde

Vijana wa chipukizi wapongezwa kwa kushiriki kikamilifu kwenye sherehe za Mapinduzi


  
STATE HOUSE ZANZIBAR
OFFICE OF THE PRESS SECRETARY
PRESS RELEASE
  Zanzibar                                                                                                           29.3.2015
---
RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Ali Mohamed Shein leo aliungana pamoja na Vijana wa Chipukizi walioshiriki katika Sherehe za miaka 51 ya Mapinduzi ya Zanzibar ya Januari 12, 2015  katika chakula  maalum cha mchana alichowaandalia vijana hao na kuwapongeza kwa ushiriki wao huo.

Katika hafla hiyo ya chakula cha mchana iliyofanyika katika ukumbi wa Hoteli ya Bwawani, viongozi mbali mbali walihudhuria akiwemo Makamo wa Pili wa Rais Balozi Seif Ali Idd, Mawaziri, viongozi wa Chama cha Mapinduzi (CCM) pamoja na viongozi wengine wa Serikali.

Akitoa neno la shukurani kwa niaba ya Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Shein Ali Mohamed Shein, Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais, Ikulu na Utawala Bora Dk. Mwinyihaji Makame Mwadini alitoa pongezi kwa Vijana hao wa Chipukizi kwa kushiriki kikamilifu katika Sherehe hiyo adhimu hapo Januari 12, mwaka huu huko katika uwanja wa Amaan mjini Zanzibar.

Alisema kuwa Sherehe ya miaka 51 ya Mapinduzi matukufu ilifanyika kwa ustadi mzuri na ushiriki wa vijana hao ulikuwa mzuri katika gwaride, maandamano pamoja na halaiki maalum iliyowashikirisha, na kuweza kuipamba sherehe hiyo adhimu ya miaka 51 ya Mapinduzi Matukufu ya Januari 12, 1964 huku akiwasisitiza vijana hao kuwa na uchungu na kuzidi kuipenda nchi yao.


Dk. Mwinyihaji alisema kuwa kuna kila sababu ya kuyaenzi, kuyatunza na kuyasherehekea Mapinduzi ya Januari 12, 1964 kwani ndio yaliyowakomboa wanyonge wa Zanzibar.

Aidha, Dk. Mwinyihaji Makame aliwataka vijana hao pamoja na wananchi wote wa Zanzibar kuendelea kuyapenda Mapinduzi ya Zanzibar sambamba na kuendelea kusherehekea maadhimisho yake kila wakati unapofika kutokana na umuhimu wake mkubwa.

Pamoja na hayo, Dk. Makame aliwasihi na kuwasisitiza vijana hao kuendelea kusoma kwa bidii kubwa na huku akiwaeleza kuwa hatua za makusudi zilizochukuliwa na Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Ali Mohamed Shein kutangaza rasmi kuondoa michango maskulini kuanzia mwaka huu ni jambo la busara ambalo litawasaidia wao vijana pamoja na wazazi wao kwa jumla.

Alisema kuwa hiyo ndio azma ya Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar ya kuondoa michango yote iliyokuwa ikitolewa hapo kabla hatua ambayo imeweza kuungwa mkono na Waziri husika wa Wizara ya Elimu na Mafunzo ya Amali Mhe. Ali Juma Shamuhuna kwa kusisitiza kuwa hakuna mtoto hata mmoja atakae fika umri wa kuanza masomo na kukosa elimu kwa sababu ya kutotoa mchango wa skuli.

Akiendelea kutoa salamu kwa niaba ya Dk. Shein, Dk. Mwinyihaji alitumia fursa hiyo kwa kutoa pongezi kwa Kamati ya Sherehe na Mapambo chini ya uongozi wa Makamu wa Pili wa Rais, Balozi Seif Idd pamoja na viongozi wengine wa Wizara hiyo na nyenginezo ambao wameshiriki kikamilifu katika maandalizi ya shehere hizo.

Pia, Alitoa shukurani kwa waandaanji wa hafla hiyo pamoja na ile iliyofanyika hapo jana kwa ajili ya vikosi vya Ulinzi vilivyoshiriki katika gwaride la kutimiziza miaka 51 ya Mapinduzi ya Januari 12, 2015, hafla ya chakula ambayo ilifanyika katika Kambi ya Bavuai, Migombanai mjini Zanzibar.

Hafla hiyo ilipambwa na taarab maalum ya kikundi cha ‘Diamond Taarab’ ambacho kiliweza kutumbuiza kwa nyimbo zao mbali mbali za midundo ya kileo na ile midundo ya asili na kuweza kutoa burudani safi kwa vijana na waalikwa wote waliofika katika hafla hiyo.

Mapema Mkuu wa Halaiki ya vijana hao, Bwana Ali Mohammed  Baraka alitoa shukurani kwa Dk. Shein kwa niaba ya vijana hao na kueleza kuwa kuwaandalia chakula hicho cha mchana vijana hao ni kuonesha mapenzi makubwa aliyonayo Dk. Shein kwa vijana na kutumia fursa hiyo kuwashukuru vijana hao kwa kuendelea kulitendea wema Taifa lao.

Hafla hiyo ni muendelezo wa utamaduni aliouweka Dk. Shein wa kuwapongeza na kuwaandalia chakula cha mchana vikosi vya ulinzi pamoja na Chipukizi ambao hushiriki katika maadhimisho ya Sherehe za Mapinduzi matukufu ya Zanzibar zinazofanyika kila ifikapo Januari 12 ya kila mwaka.

Rajab Mkasaba, Ikulu Zanzibar

Postal Address: 2422 Tel.:0777427449. Fax: 024 2231822 
 E-mail: rajabmkasaba@yahoo.co.uk

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.