Habari za Punde

Dk Shein atembelea uwanja wa ndege wa Kimataifa wa Abeid Amani Karume kuangalia maendeleo ya ujenzi


  
STATE HOUSE ZANZIBAR
OFFICE OF THE PRESS SECRETARY
PRESS RELEASE
  Zanzibar                                                                             9.4.2015
---
RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Ali Mohamed Shein leo amefanya ziara ya kutembelea na kuangalia maendeleo ya ujenzi wa uwanja wa ndege wa Kimataifa wa Abeid Amani Karume.

Dk. Shein alifanya ziara hiyo mapema leo asubuhi akiwa ameongozana na viongozi wa Wizara ya  Miundombinu na Mawasiliano, Wizara ya Nchi Ofisi ya Rais Tawala za Mikoa na Idara Maalum, uongozi wa Wizara ya Fedha na viongozi wengineo wa Mamlaka ya Uwanja huo.

Mapema Dk. Shein alipata maelezo kutoka kwa Katibu Mkuu wa Wizara ya Miundombinu na Mawasiliano Dk. Malick Akili ambaye alimueleza hatua zinazoendelea katika ujenzi wa jengo jipya la abiria pamoja na mradi wa ujenzi wa uzio  katika uwanja huo.

Katika maelezo yake, Dk. Malick alisema kuwa ujenzi wa jengo la abiria unaendelea vizuri hivi sasa chini ya Kampuni ya Kichina ya Beijing Construction Engineering Group Co. Ltd (BCEG).

Katibu Mkuu huyo alitoa maelezo juu marekebisho ya ujenzi wa jengo jipya la uwanja wa ndege wa Abeid Amani Karume pamoja na hatua za ujenzi wa uzio unaozunguka uwanja huo.

Akieleza kuhusu mradi wa ujenzi wa uzio, Katibu Mkuu huyo alisema kuwa hadi kufikia hivi sasa sehemu iliyowazi ambayo mkandarasi anaendelea na kazi ni takriban mita 500 iliopo sehemu ya Kaskazini Magharibi ya kiwanja na kusisitiza kuwa ili kukamilisha eneo hilo la uzio kwa kipande cha mita hizo jumla ya TZS milioni 560 zinahitajika.


Aidha, Dk. Shein kabla ya kuanza ziara hiyo alitembelea kituo cha Zimamoto na Uokozi kiliopo uwanjani hapo na kupata maelezo  juu ya uimarishaji wa Kikosi cha Zimamoto kiwanjani hapo kutoka kwa uongozi wa Kikosi hicho.

Katika ziara yake kwenye ujenzi wa jengo jipya la abiria la uwanja wa ndege wa Abeid Amani Karume, Dk. Shein alipata maelezo kutoka kwa viongozi wa Wizara ya Miundombinu na Mawasiliano pamoja na kutoka kwa Mshauri Elekezi mpya wa Kampuni ya ADPI ya Ufaransa bwana  Verna Guillaume.

Kwa mujibu wa maelezo ya Mshauri Elekezi wa Kampuni ya ADPI bwana Guillaume kutoka Ufaransa, alimueleza Dk. Shein hatua za ujenzi zinazoendelea vizuri huku akitoa maelezo juu ya marekebisho kadhaa ya ujenzi huo unaoendelea ambayo yatasaidia katika kufikia lengo lililokusudiwa.

Nae,  Msimamizi Mkuu wa Mradi wa Ujenzi wa jengo jipya la abiria Bwana  Yasser De Costa alitoa maelezo kadhaa kwa Mhe. Rais juu ya ujenzi huo unaoendelea ambao utasaidia kwa kiasi kikubwa kutoa huduma kwa wageni na wenyeji wanaosafiri kupitia jengo hilo jipya na la kisasa.

Ongezeko la eneo la jengo baada ya masawazisho hayo ya kiufundi yatapelekea kuongezeka kwa uwezo wa jengo hilo kuhudumia jumla ya abiria milioni 1.6 badala ya abiria milioni 1.1 iliyopangwa kupitia mkataba wa awali.

Sambamba na hayo, takwimu zinaonesha kuwa Kiwanja cha Ndege cha Kimataifa cha Abeid Amani Karume kinakadiriwa kuchukua abiria wapatao milioni 2 ifikapo mwaka 2025, hatua ambayo pia,  itachangia kukuza uchumi na kuimarisha sekta ya utalii hapa Zanzibar.

Rajab Mkasaba, Ikulu Zanzibar

Postal Address: 2422 Tel.:0777427449. Fax: 024 2231822 
 E-mail: rajabmkasaba@yahoo.co.uk

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.