Habari za Punde

Wawakilishi kuanza Kuchambua Bajeti.

Na, Himid  Choko, BLW.                                                              
WAJUMBE wa Baraza la Wawakilishi Zanzibar, wanatarajiwa kuaza kuchambua Bajeti ya Serikali na  ile ya kila wizara kwa mwaka wa Fedha 2015/2016 kuanzia Alkhamis ijayo.
Akizungumza na mwandishi wa habari hizi huko Afisini kwake Chukwani nnje Kidogo ya Mji wa Zanzibar, Katibu wa Baraza la Wawakilishi  Zanzibar, Yahya Khamis Hamad amesema maandalizi yote kwa ajili ya shughuli hiyo tayari yamekamilika.

Amesema shughuli  zote  za kupitia Bajeti  hizo zitafanyika katika Afisi ya Baraza la Wawakilishi Chukwani, na zitaanza kwa Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Ikulu na Utawala Bora kuwasilisha Mpango wa Maendeleo wa Mwaka 2015/2016 na baadae Waziri wa  Fedha kuwasilisha Bajeti ya Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar 2015/2016 mbele ya  Kamati ya Wenyeviti ya Baraza la Wawakilishi, siku ya Alkhamis ya Tarehe 30/5/2015.

Katibu Yahya amefafanua kwamba Kamati hiyo ya Wenyeviti inaundwa na Wenyeviti wa Kamati zote  saba za Kudumu za Baraza la Wawakilishi  na  itajadili Bajeti hiyo   siku ya Jumamosi  ya tarehe  02/05/2015 na Jumapili ya tarehe 03/05/2015  na hatimae bajeti hiyo itawasilishwa katika Baraza zima la Wawakilishi Jumatano ya tarehe 13/05/2015.

Aidha amesema  kwa upande wa Bajeti za Kisekta, Kamati za kudumu zitaanza kujadili Bajeti za Wizara zinazozisimamia kuanzia Jumatatu ya tarehe 04/05/2015 hadi Alkhamis ya tarehe 07/05/2015  na baadae zitawasilishwa katika Baraza zima wakati wa Mkutano wa Bajeti.

Katibu huyo wa Baraza la Wawakilishi  amezidi kufafanua kwamba, Utaratibu wa kuwasilisha, kujadili, na kupitisha bajeti  ya serikali kwenye Baraza la Wawakilishi la Zanzibar umewekwa kwenye Katiba ya Zanzibar ya 1984 na umefafanuliwa kwa upana zaidi kwenye Kanuni za Baraza la Wawakilishi, Toleo la 2012.

“Makadirio ya jumla ya Bajeti ya Serikali kwanza hupelekwa kwenye Kamati ya Wenyeviti wa Kamati za Kudumu za Baraza la Wawakilishi kwa mujibu wa Kanuni ya 95 (1) (Kanuni za Baraza la Wawakilishi, Toleo la 2012) na baadae ndipo huwasilishwa kwenye Baraza’’ Alisema Katibu Yahya.

Yahya aliendelea kusema kwamba “Mapendekezo ya bajeti ya kila Wizara kwanza hupelekwa kwenye Kamati husika  ya kisekta kwa mujibu wa Kanuni ya 96 (1)  na baada ya Kamati husika kumaliza kazi ya kushughulikia mapendekezo hayo ndipo huwasilishwa kwenye Baraza na Waziri mwenye dhamana ya Wizara husika au Kaimu wake.”

Amesema bajeti ni nyenzo muhimu na muhimili wa maendeleo  na ustawi wa jamii  hivyo amewaomba wananchi kufuatilia mchakato wa Bajeti  kwenye Baraza na kushirikiana ipasavyo na Wawakilishi wao  na wahakikishe kwamba bajeti inaakisi  maisha yao ya kila siku  kulingana na wakati  uliopo.

Aidha  amesema hivi sasa ni wakati muwafaka  wa wananchi  kuwatosheleza  wawakilishi wao  pamoja na Wajumbe wenyewe  kufanya utafiti ili hatimae kuhakikisha kwamba maudhui ya mijadala ya shughuli za kila Wizara yanalenge  juu ya Sera na Sheria za  Fedha, Utawala na Utendaji bora wa shughuli za Umma.

“Pamoja na kuzingatia hizo sera na masuala ya Malengo ya Milenium Mijadala yao pia inatakiwa ijikite katika kuwasilisha  maoni na  mitizamo ya wananchi  pamoja na  kero zinazowakabili katika kutathmini vipaumbele vya Bajeti hiyo ”  alisema Katibu Yahya.

Mkutano ujao wa Baraza la Wawakilishi ambao utajadili Bajeti, unategemewa kuanza  Jumatano ya tarehe 13/05/2015  na kuchukua takriban mwezi mmoja na nusu.  
MWISHO.
Imetolewa na.
Himid CHOKO,
O777436016
BLW, zanzibar,

28/04/2015.

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.