STATE HOUSE ZANZIBAR
OFFICE OF THE PRESS SECRETARY
PRESS RELEASE
Zanzibar 01 Mei, 2015
TAARIFA KWA VYOMBO VYA HABARI
Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Ali Mohamed Shein amewahakikishia watumishi wa umma kuwa Serikali itawalipa, mapema kwenye mwaka wa fedha unaoanza Julai 2015/2016, malimbikizo yao yote ya madai yanayotokana na kasoro zilizojitokeza wakati wa marekebisho ya mishahara na posho.
Akizungumza na wafanyakzi wakati wa Maadhimisho ya Siku ya Wafanyakazi Duniani leo yaliyofanyika katika viwanja vya Kiwanda cha Mkonyo kilichoko Wawi wilaya ya Chakechake Pemba, Dk. Shein amewahakikishia watumishi hao kuwa Serikali inazifanyia kazi kasoro hizo na kuwahakikisha kuwa hakuna mtumishi atakayepoteza haki yake.
“Serikali inaendelea kuyahakiki malimbikizo hayo na tayari tumeshafanya uamuzi wa kuyalipa katika bajeti ya mwaka wa fedha 2015/2016”alisisitiza Mheshimiwa Rais.
Sambamba na kuwahakikishia malipo hayo, Dk. Shein alibainisha kuwa hatua zote zinazochukuliwa na Serikali kuimarisha hali ya wafanyakazi lengo lake ni kulifanya suala la kuwapatia maslahi bora watumishi wa umma liwe ni suala endelevu kadri uchumi unavyoimarika.
Miongoni mwa hatua hizo ambazo amezitaka kuwa ni miongoni mwa mafanikio ya Serikali ya Awamu ya Saba katika kuimarisha utumishi wa umma ni kupitisha sheria mbalimbali zikiwemo Sheria Na. 2 ya Utumishi wa Umma ya mwaka 2011.
Aidha alieleza kuwa kanuni 12 za Sheria za Kazi zimetungwa katika kipindi hiki na kuanza kutumika miongoni mwao ni za Sheria ya Ajira Namba 11, Sheria ya Mahusiano Kazini Namba. 1, zote za mwaka 2015 na Kanuni za mwaka 2014 za Sheria ya Utumishi wa Umma Namba 2 ya mwaka 2011.
Katika mnasaba huo ametoa wito kwa watumishi na waajiri kusoma vyema na kufahamu Sheria ya Utumishi wa Umma ya Mwaka 2011 kwa kuwa ndio msingi wa mambo yote yanayohusu sheria, maslahi, makosa na adhabu zake.
Dk.Shein aliwaeleza wafanyakazi hao kuwa Serikali ipo katika hatua za mwisho za kukamilisha Sera ya Usalala Kazini ili kuweka mfumo mzuri wa afya katika maeneo ya kazi kwa lengo la kuwakinga wafanayakazi na ajali na majanga mengine katika sehemu za kazi.
Kwa hivyo aliwataka watumishi wote nchini kuendelea kufanyakazi kwa mujibu wa Sheria na Kanuni za kazi zinavyoelekeza na kusisitiza kuwa ni lazima katika utendaji wao kuhakikisha kuwa wanatenda haki na kuwaheshimu wananchi kwa kuwa Serikali yote akiwemo yeye mwenyewe Mheshimiwa Rais wanawajibika kwa wananchi.
Katika hotuba yake hiyo Dk. Shein aliipongeza Wizara ya Nchi, Ofisi ya Rais, Kazi na Utumishi wa Umma kwa kazi nzuri inayofanya kuratibu na kuweka uhusiano mzuri kati ya Serikali, wafanyakazi na kusimamia ipasavyo Sera na Sheria mbalimbali zinazohusu kazi na ajira.
Kwa hivyo aliwahakikishia kuwa Serikali anayoiongoza inazingatia sana umuhimu wa uhusiano huo na siku zote itakuwa tayari kushirikiana nao kwa lengo la kuzitafutia ufumbuzi changamoto zinazowakabili wafanyakazi wote Unguja na Pemba.
Katika hatua nyingine Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi amewasihi wafanyakazi na wananchi kwa jumla kuhakikisha kuwa wanashiriki vyema katika uchaguzi mkuu ujao huku wakizingatia kuendeleza mafanikio ya kuimarisha amani, umoja na mshikamano.
“Halitakuwa jambo jema utaratibu huu wa kidemokrasia ukawa ni chanzo cha kuvuruga amani, umoja na mshikamano” Dk. Shein alisisitiza na kuongeza kuwa aliyedhamiria kutenda lake aseme na nafsi yake kwanza kabla hajafanya hivyo.
Kwa upande wake Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais, Kazi na Utumishi wa Umma, Mheshimiwa Haroun Ali Suleiman alieleza kuwa katika kukuza uelewa wa jamii kuhusu sheria za kazi, sheria za kazi za Zanzibar zimetafsiriwa kwa lugha ya Kiswahili na wizara hiyo kwa kushirikiana na Shirika la Kazi Duniani(ILO) imeziweka sheria hizo katika lugha nyepesi.
Waziri Haroun alibainisha kuwa Wizara yake inaendelea na zoezi la uwekaji wa taarifa za watumishi wa umma katika mfumo wa kieletroniki hatua ambayo itasaidia katika kuimarishaji wa kutunza kumbukumbu za taarifa zao na kulinda haki zao wakiwa kazini na baada ya kustaafu.
Aidha Wizara yake alisema imefanikiwa kupunguza migogoro ya kazi kutoka 179 mwaka 2012/2013 hadi migogoro 102 mwaka 2013/2014.
Awali akizungumza katika hafla hiyo Katibu Mkuu wa Shirikisho la Wafanyakazi Zanzibar-ZATUC Bwana Khamis Mwinyi Mohamed alimpongeza Mheshimiwa Rais kwa utayari wake wakati wowote kushirikiana na Shirikisho hilo kitendo ambacho kimezidi kujenga mahusiano mazuri kati ya Shirikisho na Serikali.
Aliipongeza Serikali kwa kutoa fursa kwa wafanyakzi kushiriki katika michakato mbalimbali ya masuala ya kitaifa hivyo kuwafanya kuwa sehemu ya maamuzi na matokeo yatokanayo na michakato hiyo.
Katibu Mkuu huyo aliiomba serikali kuangalia upya kodi zinazotozwa wafanyakazi katika mishahara pamoja na malipo ya viinua mgongo na pensheni.
Nae Mkurugenzi wa Chama cha Waajiri Zanzibar (ZANEMA) Bwana Salah Salim Salah alisisifu kuzidi kuimarika kwa mahusiano kati ya waajiri na wafanyakazi jambo ambalo limerahisisha utatuzi wa migogoro baina ya pande mbili hizo.
Hali hiyo imewezesha kuwepo na mawasiliano na mashauriano ya mara kwa mara kati ya pande hizo na kuondokana na yale yaliyotokea zaid ya miaka 126 huko nchini Marekani ambako wafanyakazi walipodai haki zao walikumbana na kadhia na vurugu zilizosababish baadhi yao kupoteza maisha.
Mkurugenzi huyo alieleza kuwa mwaka huu ni mwaka muhimu kwa wajiri na wafanyakazi kama walivyo wananch iwenginek kutokana na nchi yetu kuelekea Uchaguzi Mkuu kwa kuhakikisha uchaguzi huo haiwi chanzo cha vurugu ambazo zinaweza kuharibu nchi na uchumi wake.
Katika maadhmisho hayo Mheshimiwa Rais alikabidhi zawadi mbalimbali kwa watumishi bora kutoka ofisi na taasiii mbalimbali za umma.
No comments:
Post a Comment