Habari za Punde

Dk.Shein akutana na Balozi Gamala

Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk.Ali Mohamed Shein akisalimiana na Balozi Mteule wa wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania nchini Burundi Mhe,Rajab Gamala alipofika Ikulu Mjini Zanzibar kujitambulisha jana,[Picha na Ikulu.]
  
STATE HOUSE ZANZIBAR
OFFICE OF THE PRESS SECRETARY
PRESS RELEASE
  Zanzibar                                                                                                                              12.6.2015
---
RAIS  wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Ali Mohamed Shein amesema kuwa Zanzibar imekuwa na uhusiano na mashirikiano mazuri na  nchi za Maziwa Makuu hivyo ipo haja ya kuimarisha hatua hiyo kwa kuendelea kuutangaza utalii wa Zanzibar katika nchi hizo.

Dk. Shein aliyasema hayo leo, huko Ikulu mjini Zanzibar wakati alipofanya mazungumzo na Balozi Mteule wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania nchini Burundi Mhe. Rajab Hassan Gamaha ambaye alifika Ikulu kwa ajili ya kuaga na kupata baraka za Rais.

Katika mazungumzo hayo, Dk. Shein alimueleza Balozi huyo kuwa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar imechukua juhudi kubwa za kuiimarisha sekta ya utalii hapa nchini sambamba na kuimarisha vivutio vyake kwa wageni kutoka nchi mbali mbali duniani  zikiwemo nchi za Maziwa Makuu kama vile Burundi.

Dk. Shein alieleza kuwa ni imani yake kubwa kuwa migogoro iliyopo nchini humo hivi sasa itamalizika kwa msaada mkubwa wa viongozi wa nchi za Jumuiya ya Afrika Mashariki ambao wamekuwa wakichuku juhudi za makusudi za kuhakikisha migogoro iliyopo nchini humo inamalizika.

Alisema kuwa kuteuliwa kwa Balozi huyo kuiwakilisha Tanzania nchini humo ni hatua moja wapo ya Tanzania kuendelea kuimarisha uhusiano na ushirikiano wa kidugu, kidamu na kimipaka na Burundi.

Dk. Shein alisema kuwa hivi sasa wananchi walio wengi wa Burundi wameanza kujifunza lugha ya Kiswahili na Zanzibar ni sehemu yenye asili ya lugha hiyo, hivyo ipo haja ya kuwashajiisha wananchi wa Burundi kuja Zanzibar kujifunza lugha hiyo kwenye Chuo chake Kikuu cha Taifa cha Zanzibar (SUZA).

Katika maelezo yake Dk. Shein alisema kuwa heshima ya Tanzania nchini Burundi ni kubwa sana  hivyo ipo haja ya kuendeleza uhusiano na ushirikiano wa muda mrefu uliopo kati ya pande mbili hizo.

Kutokana na hatua hiyo, Dk. Shein alisisitiza kuwa kuna kila sababu za kuimarisha uhusiano na kiuchumi hasa katika uwekezaji kati ya Tanzania na Burundi kwa kuangalia zaidi fursa ziliopo nchini hasa kwa upande wa Zanzibar katika sekta ya utalii na hata sekta ya biashara.

Aidha, Dk. Shein alitumia fursa hiyo kumueleza Balozi Gamaha kuwa wakati ukifika Zanzibar itafanya uchaguzi wake ulio huru na haki huku akieleza matumaini yake kuwa viongozi wa vyama vya siasa watafuata matakwa ya Serikali katika kusimamia amani na utulivu.

Nae  Mhe. Rajab Hassan Gamaha, Balozi Mteule wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania nchini Burundi alieleza kuwa katika utendaji wake wa kazi nchini humo atahakikisha uhusiano na ushirikiabno kati ya Tanzania na Burundi unaumarika zaidi.

Balozi huyo nae alieleza matumaini yake kuwa nchi hiyo itafika siku itarejea katika hali yake ya amani na utulifu kutokana na juuhudi zinazochukuliwa na viongozi wa Afrika Mashariki katika kutatua migogoro nchini humo.

Balozi Gamaha, alisema kuwa wananchi wa Barundi na Tanzania wamekuwa na uhusiano na ushirikiano wa muda mrefu kwani tayari wapo baadhi ya Watanzania ambao wameekeza nchini Burundi pamoja na wengine wanaofanya biashara nchini humo.

Sambamba na hayo, Balozi huyo Mteule alimuhakikishia Dk. Shein kuwa atahakikisha anafanya kazi zake kwa uaminifu na bidii kubwa huku akiiombea Tanzania na Zanzibar kwa jumla kufanya uchaguzi mkuu ujao kwa amani na utulivu.

Aidha, Balozi Gamaha alieleza kuwa Sekta ya Utalii aghalabu huendana na sekta ya biashara hivyo kuimarika kwa sekta ya biashara kati ya Burundi na Tanzania ikiwemo Zanzibar kutasaidia kwa kiasi kikubwa kupanua soko la utalii la Zanzibar.

Alieleza matumaini yake kuwa sekta ya utalii inaweza kuimarika zaidi hapa Zanzibar kutokana na soko la nchi za Maziwa Makuu ikiwemo  Burundi.

Balozi Rajab Gamaha ameshawahi kuwa Balozi wa Tanzania nchini Uganda kabla ya kuwa Naibu Katibu Mkuu Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa, Balozi Gamaha anachukua nafasi ya Balozi Dk. Mwasi Nzagi ambaye amestaafu kwa mujibu wa Sheria.

Rajab Mkasaba, Ikulu Zanzibar

Postal Address: 2422 Tel.:0777427449. Fax: 024 2231822 
 E-mail: rajabmkasaba@yahoo.co.uk


No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.