Na Maryam Kidiko / Mwashungi Tahir-Maelezo Zanzibar .
Chama cha Wakulima ( A.F.P.) wamesikitishwa na kitendo cha wawakilishi wa Chama cha Wananchi (CUF) kutoka nje ya kikao cha Baraza la Wawakilishi ambacho kilikuwa kikijadili mswada wa kupitisha matumizi ya Serikali kwa mwaka 2015/2016.
Akizungumza na Waandishi wa habari katika Ukumbi wa Habari Maelezo Zanzibar Mwenyekiti wa chama hicho Said Soud Said amesema Chama cha CUF ni sehemu ya Serikali hivyo hawapaswi kufanya kitendo hicho.
Amesema chama hicho kimelaani vibaya kitendo hicho kwa chama cha CUF kwani kimeweza kuonesha picha mbaya katika Baraza la Wawakilishi kwakuwa wao ni Viongozi wakuu katika Serikali ya Mapinduzi hawakupaswa kuchukua hatua hiyo ambayo imewaacha jamii katika hali ngumu.
Aidha amesema kitendo hicho kimelaaniwa na kila mwananchi mpenda maendeleo na ambae anaumwa na nchi hii na pia inaonyesha dhahiri kuwa CUF hawawezi kuongoza pindi wakipata madaraka.
“Wazanzibar hawajazowea fujo kwani wamezowea kuwa nchi hii kuwa na amani na utulivu ambayo ni thamani yetu tunojivunia hapa nchini” alisema mwenyekiti huyo.
Pia aliitaka Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar kujenga Viwanda mbalimbali ili Vijana ambao waliomaliza elimu wapate ajira katika Viwanda hivyo.
Vile vile alimuomba Rais wa Zanzibar atumie busara na hekma ili uvunjifu wa amani usijetokea katika nchi hii ya Zanzibar na kwa wale ambao wanaotaka kuharibu amani ya Nchi wachukuliwe hatuwa za kisheria mara moja.
Sambamba na hayo amesema Wananchi wapatiwe elimu ya uraia ili waepuke tabia ya kuendeshwa na watu wasiotaka maendeleo ya Nchi.
IMETOLEWA NA MAELEZO ZANZIBAR.
No comments:
Post a Comment