Habari za Punde

Uhamiaji kushirikiana na vikosi vyaulinzi na usalama kudhibiti wahamiaji wasio rasmi

Na Haji Nassor, Pemba 

BAADA ya gazeti hili, kuchapisha habari juu ya wahamiaji wasio rasmi kuzitumia bandari bubu kuingia na kutoka nchini, sasa Idara ya Uhamiaji Zanzibar, imeibuka na kutaka kudhibiti bandari hizo kwa kushirikiana na vikosi vya ulinzi na usalama.

Wakati hayo yakijiri kwa upande wao wananchi wanaoishi ukanda wa bahari ya hindi Kisiwani Pemba, wameahidi kushirikiana na Idara ya uhamiaji juu ya wazo lake la kuimarisha ulinzi katika bandari hizo.

 Walisema kwa muda mrefu Idara hiyo imekuwa imesahau wajibu wake wa kushisirikia vikosi mbali mbali vikiwemo vya SMZ na wananchi husika, jambo ambalo lililosababisha uingiaji wa wageni kwa wingi kupitia bandari hizo.

Wakizungumza na mwandishi wa habari hizi kwa nyakati tofauti, wananchi hao walisema, suala la kudhibiti wahamiaji wasio rasmi, linapaswa kwa idara tofauti kushirikiani ikiwemo ya Uhamiaji, KMKM, masheha na wananchi husika wakiwemo wavuvi.

Walisema kama sasa Idara ya uhamiaji imeshajipanga na hilo, wao kama wananchi wako tayari maana athari ya wageni kutumia bandari bubu kuingia na kutoka ndani ya visiwa vya Unguja na Pemba humpata kila mmoja.

Mmoja wa wananchi hao Ali Khamis Haji wa shehia ya Ziwani Chake chake, alisema ni vyema kwa Idara hiyo kwanza kukaa na wananchi kwa kuwapa mbinu mwafaka ili kutoa taarifa pale wanapowashuhudia.

“Unajua sisi kama wananchi hatupendi kuona wageni, lakini hatuna elimu ya kujua tuzifikishe wapi taarifa husika, ambapo watachukua hatua thabiti’’,alisema.

Nae Hamad Kombo Mjaka wa shehia ya Gando alisema, wakati umefika kwa Idara ya uhamiaji kuziacha ofisi na kufika kwa wananchi hasa wanaoishi karibu na bandari bubu, ili kukaa nao na kuwapa maelekezo ya kitalaamu.


Kwa upande wake Hassan Juma Hassan wa Kangani Mkoani, alisema kutokana na uwingi wa bandari bubu uliopo Zanzibar, ni vyema kwa Idara hiyo sasa kuwa karibu na KMKM pamoja na wananchi wengine.

“Mbona magendo ya karafuu yamepungua sana na yalikuwa sugu, sasa hata wageni wanaoingia kwa kutumia bandari bubu wanaweza kukoma kama Idara hiyo ikishirikiana na wananchi’’,alifafanua.


Hivi karibuni afisa uhusiano wa Idara ya uhamiaji Zanzibar Muhsin Abdalla alinukuliwa na vyombo vya habari, kwamba wanatarajia kushirikiana na vyombo vyengine vya ulinzi, pamoja na masheha ili kuweka ulinzi maalumu kwenye bandari bubu ili kudhibiti wahamiaji wasio rasmi.

Uhamiaji ilisema kuelekea uchaguzi mkuu, na hata badae ni vyema nchi ikawa shuwari na hasa baada ya kuwepo taarifa kwamba bandari bubu zinatumiwa na wageni kwa lengo la kujiandikisha na kwa ajili ya uchaguzi mkuu.

Kwa upande wake afisa uhamiaji wilaya ya Mkoani Pemba Abdalla Shehe alisema suala la bandari bubu limezagaa na wakati umefika kwa jamii kushirikiana na taasisi husika.

“Hata wilaya yangu ya Mkoani, bandari bubu zipo na zimekuwa zikitumika vibaya kwa kupitia wahalifu na hata kutoroshea mazao ya taifa’’,alifafanua.

Mei 15 na 16 mwaka huu, gazeti hili lilitoa habari juu ya uwepo kwa bandari bubu zaidi ya 500 kisiwani Pemba, ambapo wahamiaji wasio rasmi huzitumia na wahalifu kutoka au kuingia kukimbia mkono wa sheria.

Katika habari hizo, zileleza kuwa ukosefu wa walinzi wa kutosha, kutokuwepo kwa ushirikiano baina ya vikosi vya ulinzi na wananchi kukosa uzalendo ndio sababu za bandari hizo kutumika kiholela.


Bandari bubu hapa visiwani zimekuwa zikitumiwa kama kawaida na baadhi ya wavuvi na wasafiriahaji magendo kama ya karafuu na kubainika kuwa pia wakati mwengine kuwatorosha wahalifu au kuwaingiza.

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.