Habari za Punde

Kulinda na kuhifadhi miundo mbinu ya umeme ni jukumu la wananchi wote

Na Shemsia Khamis, PEMBA

SHIRIKA la Umeme Zanzibar (ZECO) Tawi la Pemba limesema  jukumu la kulinda na kuhifadhi miundo mbinu ya Umeme ni la wananchi wote na sio Shirika hilo pekee  kama wanavyodhani baadhi ya watu.

Kauli hiyo ilitolewa na Meneja wa Shirika  hilo Pemba, Salum Massoud, alipokuwa akizungumza na waandishi wa habari  wakati  kazi ya kusambaza Waya baharini kwa ajili ya kupeleka umeme Kisiwa panza na Makoongwe wilaya ya mkaoni kisiwani Pemba ikiendelea.

Alisema   ni vyema wananchi wote wakawa mstari wa mbele katika kuhakikisha miundo mbinu ya umeme inakuwa salama muda wote, ili kuunga mkono juhudi za Serikali katika kuwasambazia huduma hiyo.

Alieleza  sio jambo la busara kwa wananchi kuthubutu kuharibu miundo mbinu hiyo kwa njia moja au nyengine, kwani ni kurudisha nyuma maendeleo yao na Serikali kwa ujumla.

Salim, alisema  ahadi ya Serikali ni kusambaza umeme katika visiwa vyote vidogo vidogo vya Unguja na Pemba, ndio maana wakaamua kuibua mradi maalumu wa kwa ajili ya kutekeleza ahadi hiyo.


‘’Lengo la Serikali, ni kuhakikisha kuwa wananchi wote wa mjini na vijijini wanapata huduma ya umeme, bila ya ubaguzi wa aina yoyote ile’’, alisema Meneja.

Alifahamisha  Waya huo umechukuwa kilomita 1.7 kutoka Chokocho hadi Kisiwapanza, ambapo Michenzani hadi Makoongwe umechukua kilomita 1.5, hivyo ni vyema wananchi wakawa makini kuulinda waya huo muda wote.

Akizungumzia matumaini yao, mara baada ya kukamilika zoezi hilo visiwani humo, alisema endapo Wananchi watashajihika kuunga Umeme ni kuongeza uzalishaji kwa Shirika na Serikali kwa ujumla.

Kwa upande wake, Sheha wa shehia ya Makoongwe Silima Hija Hassan, alisema  kufika kwa huduma ya umeme Kisiwani kwao  ni faraja iliyoje kwani walikuwa na hamu muda mrefu.

Alifahamisha  mara baada ya kukamilika kwa zoezi hilo Kisiwa chao kitakuwa cha aina yake  kwani hata shughuli za uzalishali zinaweza kuongezeka.

‘’Shughuli za uzalishaji zitaongezeka  maana wananchi watanunua Mafriza wataeka Samaki na hata juisi wanaweza kufanya kwa biashara’’, alisema Sheha.

Mmoja kati ya wananchi  wa Kisiwa hicho ,Omar Moh’d Salum, alisema wamekuwa wakiitafuta huduma ya umeme masafa marefu, hivyo kukamilika kwa zoezi hilo kutawaondoshea usumbufu.

Alieleleza  baadhi ya wananchi wanatumia umeme wa Sola lakini mara baada ya kufika umeme Kisiwani kwao, huduma hiyo itakuwa ya uhakika.


Waya huo uliosambazwa katika bahari kwa ajili ya kufikisha umeme Visiwani humo, umegharimu Tshilingi bilioni 1.5 na zoezi hilo linatarajiwa kukamilika baada ya siku kumi.

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.