Habari za Punde

Dk. Shein awaambia wavuvi na wakulima wa mwaniI: Kaeni mkao wa kula, neema inakuja

Na Mwandishi Wetu Pemba. 

MGOMBEA nafasi ya urais wa Zanzibar kupitia Chama cha Mapinduzi Dk. Ali Mohamed Shein ameahidi ndani ya miaka miwili kukamilisha mpango mkubwa wa kuimarisha sekta ya uvuvi utakaojumuisha kuwapatia wavuvi boti maalum za kufanyia shughuli za uvuvi.

Amesema mpango huo ambao matayarisho yake tayari yameanza utashirikisha sekta binafsi ambapo tayari makubaliano ya awali yamefanyika ambapo katika hatua ya awali boti 20 kumi zikiwa za mita 6 na nyingine 10 za mita 9 watapewa wavuvi kwa majaribio.

Akizugumza katika mkutano wa kampeni uliofanyika katika kiwanja cha Shamemata huko Micheweni, Mkoa wa Kaskazini Pemba, Dk. Shein alieleza kuwa endapo wavuvi watazikubali boti hizo baada ya majaribio boti nyingine zaidi zitatengenezwa na kupewa wavuvi.

Dk. Shein alifafanua kuwa baada hatua hiyo kukamilika itafuata hatua nyingine ya ujenzi wa boti za ukubwa wa zaidi ya mita 18 kwa ajili ya uvuvi wa bahari kuu hivyo kutoa fursa kwa wavuvi wa Zanzibar kuvuna rasilimali hiyo muhimu kwa uchumi wa nchi.

“Tunaamini kuwa tunaweza kuwawezesha kuvua samaki eneo la bahari kuu ndani ya miaka mitano kwa kushirikiana na kampuni moja kubwa ya kutengeneza boti na meli za uvuvi ya Sri Lanka” Dk. Shein aliwaambia wananchi hao waliokuwa wakimshangilia.

Katika mkutano huo Dk. Shein ambaye anagombea nafasi hiyo kwa mara ya pili baada ya kumalizika kipindi chake cha kwanza cha miaka mitano amewataka wananchi kumchagua tena ili kupata fursa ya kuendeleza mipango ya kujenga Zanzibar.



Mgombea huyo aliwahakikishia wakulima wa mwani ambao wengi wao ni kinamama kuwa serikali imejidhatiti kuhakikisha kuwa kilimo cha mwani aina ya ‘cottonii’ wenye thamani zaidi ambao majaribio yake yalifanyika katika baadhi ya vijiji vya wilaya ya Micheweni kinaimarishwa.

Aidha aliahidi katika kipindi kijacho wizara tatu (za Kilimo, Biashara na Uvuvi) zitashirikiana kuhakikisha kuwa mwani wa aina ya spinosum unapatiwa soko la uhakika na kwa bei muafaka ili wakulima waweze kufaidi jasho lao.

Kwa upande mwingine Dk. Shein amesema serikali atakayoiunda akichaguliwa tena itawapatia ndani ya miaka mitano kinamama wakulima wa mwani vihori 500 vya kubebea mwani baada ya serikali kuwapatia vihori 100 mwanzoni mwa mwaka huu.

Kuhusu ahadi zake alizozitoa wakati alipokuwa katika mkutano wake wa kampeni mwezi Oktoba mwaka 2010, Dk. Shein aliwaeleza wananchi hao kuwa ahadi hizo amezitekeleza na nyingine zimo katika maandalizi ya utekelezaji.

“Nimekamilisha ahadi zangu kwenu kuhusu barabara, maji na afya na kuhusu hili la uendelezaji wa eneo huru la kiuchumi la Micheweni limeshafanyiwa usanifu tayari kwa utekelezaji” Dk. Shein alibainisha.

Alifafanua kuwa hatua zimechukuliwa kuimarisha hospitali ya Micheweni ambapo maabara ya kisasa imejengwa yenye uwezo wa kuchunguza maradhi mengi,jengo la upasuaji na wodi mbalimbali za wagonjwa zimejengwa.

Alisema kilichobaki ni kuongeza baadhi ya majengo, baadhi ya vifaa pamoja na madaktari bingwa wa upasuaji, watoto na kinamama ili hospitali iweze kufikia kuwa hospitali ya wilaya.

Aliahidi kuimarisha vituo vya afya vya Kiuyu Mbuyuni na Maziwang’ombe kwa kuvipatia wahudumu zaidi wa afya na kuongeza vifaa.

Aliahidi katika kipindi kijacho ataongeza kasi ya usambazaji na uimarishaji wa wa huduma za jamii kama maji katika wilaya hiyo ambapo vijiji vya vya Kwansa, Bondeni, Mvuleni, Mkunguwachini, Kijogoo, Kijangwani, Chaleni na Sipwese vitapatiwa maji.

Kwa upande wa umeme vijiji vya Kijangwani, Sipwese na Mtukwao vitapatiwa huduma hiyo.          


No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.